Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Lefèvre d’Étaples—Alipenda Watu wa Kawaida Wajue Neno la Mungu

Lefèvre d’Étaples—Alipenda Watu wa Kawaida Wajue Neno la Mungu

ASUBUI moja ya Siku ya Yenga, mwanzo-mwanzo mwa miaka ya 1520, wakaaji wa Meaux, muji mudogo wenye kuwa karibu ya muji wa Paris, walishangazwa sana na jambo lenye walisikia katika kanisa. Walikuwa wamesikia usomaji wa Vitabu vya Injili katika luga yao ya kizalikio, ni kusema, katika Kifaransa kuliko katika Kilatini!

Mutafsiri wa Biblia mwenye alisaidia jambo hilo lifanyike ni Jacques Lefèvre d’Étaples (katika Kilatini, Jacobus Faber Stapulensis), ambaye alimuandikia rafiki yake wa sana hivi: “Hauwezi kuwazia namna Mungu anaendelea kusaidia watu wengi kuelewa Neno lake.”

Wakati huo, Kanisa Katoliki na wasomi wa teolojia wa Paris walipinga kutumia tafsiri za Biblia katika luga za kawaida. Kwa hiyo, nini ilimuchochea Lefèvre kutafsiri Biblia katika Kifaransa? Na alifanya nini ili kusaidia watu wa kawaida kuelewa Neno la Mungu?

ALITAFUTA KUJUA MAANA YA KWELI YA MAANDIKO

Mbele ya kuwa mutafsiri wa Biblia, Lefèvre alikuwa amejitoa katika kazi ya kutafuta maana ya kweli ya maandishi mbalimbali ya zamani ya filozofia na teolojia. Alitambua kama mara nyingi maandishi ya zamani hayakuwa sawa kwa sababu kwa miaka mingi yalitafsiriwa mubaya, na watu waliingiza ndani makosa. Wakati alikuwa anatafuta kujua maana ya kweli ya maandishi ya zamani, alianza kujifunza sana Biblia ya Kilatini yenye Kanisa Katoliki lilikuwa linatumia. Biblia hiyo iliitwa Vulgate.

Kwa sababu ya kujifunza Maandiko kwa bidii, alifikia kusema hivi: “Kujifunza kweli kutoka kwa Mungu ndiyo kunaleta . . . furaha nyingi sana.” Kwa hiyo, Lefèvre aliacha kujifunza filozofia na akatumia nguvu yake yote ili kutafsiri Biblia.

Katika mwaka wa 1509, Lefèvre alichapisha maandishi yenye kulinganisha tafsiri tano mbalimbali za Kilatini za kitabu cha Zaburi, * kutia ndani mabadiliko yake mwenyewe ya Vulgate. Tofauti na wasomi wa teolojia wa wakati wake, alijikaza kutafsiri maandiko ya Biblia katika njia yenye kueleweka na yenye kuwa wazi. Namna yake ya kutafuta kujua maana ya maandiko ilisaidia sana watu wenye elimu ya Biblia na watu wenye kuleta marekebisho.—Soma kisanduku chenye kichwa “ Maandishi ya Lefèvre Yalikuwa na Matokeo Juu ya Martin Luther.”

Kisanduku chenye majina ya cheo ya Mungu katika Zaburi, kama vile yanapatikana katika Fivefold Psalter ya 1513

Lefèvre alikuwa Katoliki tangu kuzaliwa kwake, na alikuwa hakika kama mabadiliko yangetokea katika kanisa ikiwa tu watu wa kawaida wangefundishwa muzuri Maandiko. Wakati huo maandishi mengi matakatifu yalipatikana katika Kilatini. Kwa hiyo, namna gani yangeweza kuwaletea watu wa kawaida faida?

TAFSIRI YA BIBLIA YENYE WATU WOTE WANGEWEZA KUPATA

Utangulizi wa Vitabu vya Injili unahakikisha hamu yenye Lefèvre alikuwa nayo ya kusaidia watu wote wapate Biblia katika luga yao

Kwa sababu Lefèvre alipenda sana Neno la Mungu, aliamua kufanya yake yote ili watu wengi sana walipate. Ili kufikia kusudi hilo, katika Mwezi wa 6, 1523, alichapisha tafsiri ya Kifaransa ya Vitabu vya Injili katika vitabu viwili vidogo. Bei ya vitabu hivyo vidogo ilikuwa nusu ya bei ya Biblia yenye ilitumiwa sana wakati huo, na hilo lilifanya ikuwe rahisi kwa watu wenye feza kidogo waweze pia kupata Biblia.

Bila kukawia, watu walionyesha kama wanavifurahia sana. Watu wengi, wanaume na wanawake, walikuwa na hamu ya kusoma maneno ya Yesu katika luga yao. Kwa hiyo, kopi 1 200 zenye zilichapishwa kwanza ziliisha kisha tu miezi kidogo.

ALITETEA BIBLIA BILA WOGA

Katika maneno ya utangulizi ya Vitabu vya Injili, Lefèvre alifasiria kama alitafsiri vitabu hivyo katika Kifaransa ili “watu wa kawaida” wa kanisa “waweze kuwa hakika juu ya kweli yenye kuwa katika Vitabu vya Injili kama wale wenye kuwa navyo katika Kilatini.” Lakini sababu gani Lefèvre alitamani sana watu wa kawaida warudilie mambo yenye Biblia inafundisha?

Lefèvre alijua muzuri kama mafundisho na filozofia za wanadamu zilikuwa na matokeo ya mubaya juu ya Kanisa Katoliki. (Marko 7:7; Wakolosai 2:8) Na alikuwa hakika kama wakati ulikuwa umefika ili Maandiko ya Vitabu vya Injili “yatangazwe bila makosa katika dunia yote, ili watu wasidanganywe tena na mafundisho ya wanadamu.”

Lefèvre alijikaza pia kuonyesha wazi mawazo yenye makosa ya watu wenye walipinga Biblia itafsiriwe katika Kifaransa. Alionyesha unafiki wao kwa kusema hivi: “Namna gani watafundisha [watu] kushika mambo yote yenye Yesu Kristo aliamuru ikiwa hawapendi watu wa kawaida waone na kujisomea Injili ya Mungu katika luga yao?”—Waroma 10:14.

Haiko jambo la kushangaza kwamba, bila kukawia wasomi wa teolojia kwenye masomo ya juu ya Paris yenye kuitwa Sorbonne, walijaribu kumunyamazisha Lefèvre. Katika Mwezi wa 8, 1523, walipinga tafsiri za Biblia katika luga za kienyeji na maelezo mbalimbali yenye yalitolewa juu ya Biblia, na kuziona kuwa “hatari kwa kanisa.” Kama Mufalme François wa Kwanza wa Ufaransa hangemusaidia, Lefèvre angehukumiwa kuwa muasi-imani.

ALIBAKI “KIMYA,” LAKINI ALIMALIZA KAZI YAKE YA KUTAFSIRI

Lefèvre hakuruhusu mambo mabaya yenye watu walisema juu ya kazi yake yamuzuie kutafsiri Biblia. Katika mwaka wa 1524, kisha kumaliza kutafsiri Maandiko ya Kigiriki (yenye kuitwa pia Agano Jipya), alitafsiri pia kitabu cha Zaburi katika Kifaransa ili waamini waweze kusali “kwa kujitoa kabisa na kwa moyo wote.”

Mara moja, wasomi wa teolojia kwenye masomo ya juu ya Sorbonne walichunguza tafsiri ya Lefèvre kwa uangalifu sana. Bila kukawia, waliamuru kwamba tafsiri yake ya Maandiko ya Kigiriki ichomwe mbele ya watu, na wakaonyesha wazi kuwa maandishi mengine fulani “yanaunga mukono uasi wa Luther.” Wakati wasomi hao walimuomba ajitetee, Lefèvre aliamua kubaki “kimya” na akakimbilia katika muji wa Strasbourg. Huko, aliendelea kutafsiri Biblia kwa uficho. Hata ikiwa watu fulani waliona kama uamuzi wenye alikamata ulionyesha kwamba alikuwa mwenye woga, aliona kama hiyo ndiyo ilikuwa njia ya muzuri ya kujibu watu wenye hawaone “lulu” za kweli ya Biblia kuwa za maana.—Mathayo 7:6.

Mwaka moja hivi kisha Lefèvre kukimbia, Mufalme François wa Kwanza alimuweka kuwa mwalimu wa mutoto wake wa miaka ine, mwenye kuitwa Charles. Kazi hiyo ilipatia Lefèvre wakati mwingi wa kumaliza tafsiri yake ya Biblia. Katika mwaka wa 1530, tafsiri yake ya Biblia nzima ilichapishwa katika muji wa Anvers, inchi ya Belgique, kwa ruhusa ya Mutawala Charles wa Tano. *

ALIKUWA NA MATUMAINI MAKUBWA, LAKINI HAYAKUTIMIA

Muda wa maisha yake yote, Lefèvre alitumaini kwamba kanisa lingeacha kufuata desturi za wanadamu na kurudilia ujuzi wa kweli wa Maandiko. Aliamini sana “haki ya kila Mukristo ya kusoma na kujifunza Biblia yeye mwenyewe.” Ndiyo sababu alifanya yake yote ili watu wote waweze kupata Biblia. Hata kama tamaa yake ya kuona mabadiliko katika kanisa haikutimia, uriti wenye Lefèvre aliacha, ni kusema, kusaidia watu wa kawaida kujua Neno la Mungu, hauwezi kupingwa.

^ fu. 8 Maandishi hayo yenye yaliitwa Fivefold Psalter yalikuwa na tafsiri tano za Zaburi; kila tafsiri ilikuwa katika sehemu yake. Maandishi hayo yalikuwa pia na kisanduku chenye majina ya cheo ya Mungu, na Tetragramatoni, herufi ine za Kiebrania zenye kuwakilisha jina la Mungu.

^ fu. 21 Miaka tano kisha hapo, katika mwaka wa 1535, mutafsiri Mufaransa mwenye kuitwa Olivétan, alichapisha tafsiri yake ya Biblia yenye kutegemea luga za kwanza-kwanza. Alitegemea sana tafsiri ya Lefèvre wakati alikuwa anatafsiri Maandiko ya Kigiriki.