Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kwa Nini Ndoa Nyingi Zinavunjika?

Kwa Nini Ndoa Nyingi Zinavunjika?

Kwa Nini Ndoa Nyingi Zinavunjika?

‘Mafarisayo walimjia Yesu, wakikusudia kumjaribu na kusema: “Je, ni halali mwanamume kumtaliki mke wake kwa kila sababu?”’—Mathayo 19:3.

WATU fulani walioishi siku za Yesu walitaka kujua iwapo ndoa inaweza au inapaswa kudumu. Yesu aliwaambia hivi: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” * (Mathayo 19:4-6) Bila shaka, Mungu alikusudia ndoa zidumu.

Katika nchi nyingi leo, asilimia 40 au zaidi ya ndoa zote ‘hutenganishwa,’ na kuishia katika talaka. Je, mashauri ya Biblia kuhusu ndoa yamepitwa na wakati kabisa? Je, inawezekana kuwa ndoa zinavunjika kwa sababu mpango wenyewe una kasoro?

Fikiria mfano huu: Familia mbili zinanunua magari ya aina moja. Familia moja inalitunza gari lao vizuri na kuliendesha kwa uangalifu. Hivyo gari lao haliharibiki. Ile familia nyingine haitumii wakati wala nguvu kutunza gari lao, na wanaliendesha bila kujali. Gari hilo linaharibika na kuachwa. Ni nani anayepaswa kulaumiwa katika kisa hiki cha pili—gari lenyewe au wamiliki wake? Bila shaka, wamiliki wake ndio wanaopaswa kulaumiwa zaidi.

Vivyo hivyo, kuvunjika kwa ndoa nyingi si ishara ya kuwa mpango wa ndoa una kasoro fulani. Mamilioni ya ndoa zinazofaulu ni uthibitisho tosha kuwa ndoa zinaweza kufaulu. Ndoa hizo huchangia furaha na uthabiti kwa mume na mke, familia, na jamii. Lakini ndoa, kama vile gari, inahitaji kutunzwa vizuri ili idumu.

Hata kama ndoa yako imedumu kwa siku kadhaa au miaka mingi, mashauri ya Biblia kuhusu jinsi ya kutunza na kuimarisha ndoa yana matokeo mazuri. Ona mifano kadhaa katika kurasa zinazofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ Biblia inaruhusu talaka kwa msingi wa uzinzi.—Mathayo 19:9.