Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jinsi ya Kuanza Kuaminiana Tena

Jinsi ya Kuanza Kuaminiana Tena

Siri ya Furaha ya Familia

Jinsi ya Kuanza Kuaminiana Tena

Steve *: “Sikuwahi kuwazia kwamba Jodi angefanya uzinzi. Niliacha kumwamini kabisa. Siwezi kueleza jinsi ilivyokuwa vigumu kwangu kumsamehe.”

Jodi: “Ninaelewa kwa nini Steve aliacha kuniamini. Ilinichukua miaka mingi kumthibitishia jinsi ninavyojuta.”

BIBLIA inawapa nafasi wenzi wa ndoa ambao wenzi wao wamefanya uzinzi kuamua ikiwa watawataliki au la. * (Mathayo 19:9) Steve aliyetajwa hapo juu, aliamua kutomtaliki mke wake. Yeye na Jodi waliamua kuokoa ndoa yao. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, waligundua kwamba jambo hilo lilimaanisha mengi zaidi ya kuishi pamoja tu. Kwa nini? Kwa sababu, kama maelezo yao yanavyoonyesha, ukosefu wa uaminifu wa Jodi ulifanya wasiaminiane. Kwa kuwa, kuaminiana ni jambo muhimu ili kuwa na furaha katika ndoa, wote wawili walihitaji kujitahidi kuanza kuaminiana tena.

Ikiwa wewe na mwenzi wako mnajitahidi kuokoa ndoa yenu baada ya kukabiliwa na tatizo kubwa kama uzinzi, bila shaka hali hiyo si rahisi. Baada ya kujua kwamba mwenzi wako amefanya uzinzi, huenda kwa muda fulani ikawa vigumu kukabiliana na hali hiyo Lakini mnaweza kufaulu! Mnawezaje kuanza tena kuaminiana? Hekima inayopatikana katika Biblia inaweza kuwasaidia. Fikiria madokezo manne yafuatayo.

1 Iweni Wanyoofu. “Sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo, semeni kweli,” akaandika mtume Paulo. (Waefeso 4:25) Kusema uwongo, kusema ukweli nusunusu, na kunyamaza kunaweza kufanya msiaminiane. Kwa hiyo, mnahitaji kuzungumza kwa uhuru na kwa unyoofu.

Mwanzoni, kwa sababu ya kukasirika sana, huenda wewe na mwenzi wako mkashindwa kuzungumzia ukosefu huo wa uaminifu. Hata hivyo, mwishowe mtahitaji kuzungumza waziwazi kuhusu kilichotokea. Mnaweza kuamua kwamba hamtazungumzia kila kitu kwa undani, lakini si jambo la hekima kuepuka kuzungumzia tatizo hilo. “Mwanzoni, niliona kuwa jambo lenye kuchukiza na vigumu kwangu kuzungumza kuhusu tatizo hilo,” anasema Jodi, aliyetajwa hapo juu. “Nilijuta sana kuhusu kosa langu na nilitaka tu kusahau kabisa.” Hata hivyo, kwa sababu hawakuwasiliana, hilo lilisababisha matatizo. Kwa nini? Steve anasema, “Kwa kuwa Jodi hakutaka kuzungumzia kosa alilofanya, niliendelea kuwa na shaka.” Akikumbuka hali hiyo, Jodi anakubali hivi: “Kutozungumzia tatizo hilo na mume wangu kulifanya iwe vigumu kuanza kuaminiana tena.”

Ni wazi kwamba, inaumiza hisia kuzungumzia usaliti katika ndoa. Debbie, ambaye mume wake, Paul, alifanya uzinzi na karani wake, anasema hivi: “Nilijiuliza maswali mengi sana. Inawezekanaje? Kwa nini? Walizungumza kuhusu nini? Niliumia sana kihisia kwa sababu niliendelea kufikiria jambo hilo na kujiuliza maswali mengi kadiri muda ulivyopita.” Paul anasema: “Kama inavyoeleweka, mara kwa mara mimi na Debbie tuligombana tulipokuwa tukizungumza. Lakini baadaye, tuliombana msamaha. Mazungumzo hayo ya unyoofu yalitufanya tuwe na uhusiano wa karibu zaidi.”

Mnawezaje kupunguza mzozano katika mazungumzo yenu? Kumbuka kwamba lengo lako kuu, si kumwadhibu mwenzi wako, lakini ni kujifunza kutokana na tatizo lililowapata na kuimarisha ndoa yenu. Kwa mfano, Chul Soo na mke wake, Mi Young, walianza kuchunguza uhusiano wao wakifikiria kilichosababisha Chul Soo afanye uzinzi. “Niligundua kwamba nilikuwa ninajishughulisha sana na mambo yangu ya kibinafsi,” anasema Chul Soo. “Pia, nilitaka kuwapendeza wengine na kufanya mambo waliyotaka nifanye. Nilikuwa nikitumia wakati wangu mwingi pamoja nao na kuwapa uangalifu. Jambo hilo lilifanya nisitumie wakati mwingi pamoja na mke wangu.” Kufikiria mambo hayo kwa undani kuliwasaidia Chul Soo na Mi Young wafanye marekebisho ambayo, baada ya muda, yaliwasaidia kuimarisha ndoa yao.

JARIBU KUFANYA HIVI: Ikiwa wewe ndiye uliyefanya uzinzi, epuka kutoa udhuru au kumlaumu mwenzi wako. Kubali matokeo ya matendo yako na uchungu uliosababisha. Ikiwa wewe ndiye uliyekosewa, usimpigie kelele mwenzi wako wala kutumia matusi. Ukiepuka kuzungumza kwa njia hiyo, utamtia moyo mwenzi wako aendelee kuongea nawe waziwazi.​—Waefeso 4:32.

2 Shirikianeni. Biblia inasema: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja.” Kwa nini? “Kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.” (Mhubiri 4:9, 10) Kanuni hiyo inafaa hasa mnapojitahidi kuanza kuaminiana tena.

Mkishirikiana, wewe na mwenzi wako, mnaweza kufanikiwa kuaminiana tena. Hata hivyo, nyote wawili mnahitaji kujitolea kabisa kuokoa ndoa yenu. Ikiwa utajaribu kurekebisha jambo hilo ukiwa peke yako, utakuwa unajiletea matatizo mengi hata zaidi. Unahitaji kumwona mwenzi wako kuwa mshirika wako.

Steve na Jodi waligundua jambo hilo. Jodi anasema “Ilituchukua muda fulani, lakini mimi na Steve tulishirikiana na kuimarisha ndoa yetu. Niliazimia kwamba sitawahi kumuumiza hivyo tena. Ingawa Steve aliumia sana kihisia, aliazimia kutoruhusu ndoa yetu ivunjike. Kila siku, nilijaribu kumhakikishia kwamba mimi ni mwaminifu, naye aliendelea kunionyesha upendo. Kwa sababu hiyo, nitaendelea kumshukuru kila wakati.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Pamoja, azimieni kushirikiana katika kufanya mwaminiane tena.

3 Acha Tabia za Zamani. Baada ya kuwaonya wasikilizaji wake kuhusu uzinzi, Yesu aliwashauri hivi: “Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe.” (Mathayo 5:27-29) Ikiwa wewe ndiye uliyemkosea mwenzi wako, je, unaweza kufikiri kuhusu matendo au mitazamo unayoweza kung’oa na kutupilia mbali ili kuokoa ndoa yako?

Ni wazi kwamba unahitaji kukata uhusiano na yule mtu uliyefanya naye uzinzi. * (Methali 6:32; 1 Wakorintho 15:33) Paul, aliyetajwa hapo mwanzoni, alibadili ratiba yake ya kazi na nambari yake ya simu ili asiweze kuwasiliana na yule mwanamke aliyefanya naye uzinzi. Hata hivyo, juhudi hizo zote hazikumwezesha kuacha kuwasiliana naye kabisa. Paul alikuwa ameazimia kumfanya mke wake aanze kumwamini tena hivi kwamba aliamua kuacha kazi yake. Na akaacha kutumia simu yake akawa akitumia ya mke wake. Je, mambo hayo yote yalikuwa na faida yoyote? Debbie, mke wake, anasema: “Miaka sita imepita sasa, lakini mara kwa mara huwa nina wasiwasi kwamba huenda huyo mwanamke akajaribu kuwasiliana naye tena. Lakini sasa nina uhakika kwamba Paul hawezi kuanguka katika mtego huo.”

Ikiwa wewe ndiye uliyefanya makosa, unapaswa pia kubadili utu wako. Kwa mfano, huenda unapenda kuwachezea wengine kimapenzi, au huenda unafurahia kuwazia ukiwa na uhusiano wa kimapenzi na watu wengine. Ikiwa ni hivyo, ‘vua utu wa zamani pamoja na mazoea yake.’ Badili tabia za zamani na uwe na mazoea ambayo yatafanya mwezi wako akuamini kabisa. (Wakolosai 3:9, 10) Je, malezi yako yanafanya iwe vigumu kwako kuonyesha upendo? Ingawa huenda ikawa vigumu mwanzoni, usisite kumwonyesha upendo na kumfanya akuamini. Steve anasema: “Mara kwa mara Jodi alinionyesha upendo kwa kunigusa kwa mkono wake, na mara nyingi alisema ‘nakupenda.’”

Kwa muda fulani, huenda itakuwa jambo lenye busara kumwambia mwenzi wako kila kitu unachofanya kila siku. Mi Young, aliyetajwa mwanzoni anasema: “Chul Soo alihakikisha kwamba aliniambia kila kitu kilichotokea kila siku, hata mambo ambayo hayakuwa muhimu kabisa, ili kuthibitisha kwamba hafichi jambo lolote.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Zungumzieni mambo ambayo yanaweza kuwasaidia muanze kuaminiana tena. Andikeni mambo hayo na mjitahidi kuyatimiza. Pia, katika ratiba yenu ongezeni mambo ambayo mnaweza kufurahia kufanya pamoja.

4 Tambueni Wakati wa Kusonga Mbele. Msiamue haraka kwamba wakati umefika wa kuanza kuishi kana kwamba mmerudia hali ya kawaida. Andiko la Methali 21:5 linaonya hivi: “Kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” Itawachukua muda mrefu—labda miaka kadhaa—ili muweze kuaminiana kabisa.

Ikiwa wewe ndiye mwenzi uliyekosewa, jipe muda wa kusamehe kabisa. Mi Young anasema: “Nilifikiri kwamba mke alipaswa kumsamehe mume wake aliyefanya uzinzi. Sikuelewa kwa nini mke angeendelea kumkasirikia mume wake kwa muda mrefu. Hata hivyo, mume wangu alipofanya uzinzi, nilielewa kwa nini ni vigumu kusamehe.” Kuaminiana na kusamehe ni mambo yatakayokuja polepole.

Andiko la Mhubiri 3:1-3 linasema kwamba kuna “wakati wa kuponya.” Huenda mwanzoni ukahisi kwamba njia nzuri ni kutomweleza mwenzi wako kuhusu hisia zako. Hata hivyo, kunyamaza kabisa hakutasaidia uanze kumwamini mwenzi wako tena. Ili kurekebisha uhusiano wenu, msamehe mwenzi wako na uonyeshe kwamba umemsamehe kwa kumweleza maoni na hisia zako za ndani. Pia, mtie moyo akueleze mambo anayofurahia na wasiwasi wake.

Usiwe na kinyongo. Jitahidi sana kushinda hisia hizo. (Waefeso 4:32) Huenda ukafaidika ukitafakari mfano wa Mungu mwenyewe. Waisraeli wa kale walipogeuka na kuacha kumwabudu, Mungu aliumia sana. Yehova alijifananisha na mwenzi wa ndoa ambaye mwenzi wake alikuwa amefanya uzinzi. (Yeremia 3:8, 9; 9:2) Lakini hakuendelea “kufungia kinyongo mpaka wakati usio na kipimo.” (Yeremia 3:12) Watu wake walipomrudia wakiwa wametubu kikweli, aliwasamehe.

Mwishowe, nyote wawili mkiridhika kwamba mmefanya marekebisho yanayohitajika katika uhusiano wenu, mtaanza kuhisi mkiwa salama. Kisha, badala ya kuanza kufikiri wakati wote kuhusu kuokoa ndoa yenu tu, mnaweza kukazia fikira miradi mingine. Hata hivyo, tengeni wakati wa kuchanganua maendeleo ambayo mmefanya. Msiridhike tu na mambo ambayo mmetimiza. Shughulikieni mambo madogo-madogo ambayo huenda yakawazuia msifanye maendeleo, na mwendelee kuhakikishiana uwajibikaji wenu.​—Wagalatia 6:9.

JARIBU KUFANYA HIVI: Badala ya kujaribu kurudisha ndoa yenu vile ilivyokuwa mwanzoni, jiwazieni ni kana kwamba mnajenga uhusiano mpya na ulio imara zaidi.

Mnaweza Kufaulu

Mnapohisi kwamba hamtafaulu kumbukeni: Mungu ndiye mwanzilishi wa mpango wa ndoa. (Mathayo 19:4-6) Hivyo, kupitia msaada wake mnaweza kufanya ndoa yenu ifaulu. Wenzi wote waliotajwa hapo juu walifuata mashauri ya Biblia yenye hekima na wakafaulu kuokoa ndoa zao.

Miaka 20 imepita tangu Steve na Jodi walipopatwa na tatizo katika uhusiano wao. Steve anaeleza hivi kuhusu juhudi za kuokoa ndoa yao: “Tulifanya mabadiliko muhimu tulipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Msaada tuliopata ulikuwa wenye thamani sana na ulitusaidia kukabiliana vyema na wakati huo mgumu.” Jodi anasema: “Nahisi kwamba tumebarikiwa sana kwa kuweza kuvumilia wakati huo mgumu. Kwa kujifunza Biblia pamoja na mume wangu, na kujitahidi sana, sasa tuna ndoa nzuri.”

[Maelezo ya Chini]

^ Majina yamebadilishwa.

^ Ili kupata msaada katika kufanya maamuzi kama hayo, ona gazeti la Amkeni! la Aprili 22, 1999, ukurasa wa 6, na Agosti 8, 1995, ukurasa wa 10 na 11.

^ Ikiwa kwa muda fulani hutaweza kukatiza mawasiliano (labda mkiwa kazini), unapaswa kuhakikisha mnawasiliana inapokuwa lazima tu. Pia, unapaswa kuwasiliana naye kukiwa na watu wengine na uhakikishe mwenzi wako anajua.

JIULIZE . . .

▪ Kwa nini niliamua kutovunja ndoa yangu baada ya mwenzi wangu kufanya uzinzi?

▪ Ninaona mwenzi wangu akiwa na sifa gani nzuri?

▪ Nilionyeshaje upendo kupitia mambo madogo-madogo tulipokuwa tukichumbiana, na ninawezaje kufanya hivyo tena?