Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU

“Niliona, Lakini Sikuweza Kusikia”

“Niliona, Lakini Sikuweza Kusikia”

Nilikuwa na umri wa miaka miwili katika mwaka wa 1975 wakati mama yangu alitambua kwa mara ya kwanza kwamba kulikuwa jambo fulani lisilo la kawaida juu yangu. Mama alipokuwa ananibeba katika mikono yake, rafiki mumoja aliangusha chini kitu fulani kizito, na kilifanya kishindo kikubwa sana. Mama aliona kama sikushituka hata kidogo. Nilipokuwa na miaka mitatu bado sikuweza kusema. Kisha, familia yetu ilipata habari yenye kushitua sana, waganga walihakikisha kwamba nilikuwa kiziwi!

Nilipokuwa ningali mutoto muchanga, wazazi wangu walivunja ndoa yao, na Mama yangu akiwa peke yake alilazimika kunilea mimi na ndugu zangu wakubwa, ni kusema, ndugu zangu wanaume wawili na dada yangu. Wakati huo, katika inchi ya France, watoto waliokuwa viziwi hawakufundishwa namna wanavyofundishwa leo, na nyakati fulani, njia zilizotumiwa kuwafundisha ziliwaletea matatizo mengi. Hata hivyo, kuanzia utoto wangu nilikuwa na pendeleo ambalo viziwi wengine wengi hawana. Acheni niwaelezee.

Wakati nilikuwa na miaka mitano hivi

Kwa wakati fulani, walimu wengi waliamini kwamba watoto ambao ni viziwi walipaswa kulazimishwa kusema na kujaribu kusikia mambo ambayo mwalimu alisema kwa kuangalia namna midomo yake ilivyocheza​-cheza wakati alipokuwa akisema. Kwa kweli, katika inchi ya France, ambamo nilikomalia, luga ya ishara ilikatazwa kabisa kwenye masomo. Watoto fulani ambao walikuwa viziwi walifungiwa mikono kwenye migongo yao wakati mwalimu alipokuwa akifundisha.

Katika miaka michache ya kwanza-kwanza ya maisha yangu, kila juma nilikuwa ninapitisha saa nyingi pamoja na muganga anayesaidia watu kusema. Nilikuwa ninashikwa kwenye sehemu ya chini ya kidevu ao kwenye kichwa na kulazimishwa kutoa tena na tena sauti ambazo singeweza kusikia. Hata hivyo, sikuweza kuzungumuza na watoto wengine. Hiyo ilikuwa miaka ya mateso kwangu.

Kisha, nilipokuwa na miaka sita, nilitumwa kwenda kuishi na kusomea kwenye masomo ya watoto ambao walikuwa viziwi. Kwa mara ya kwanza, nilikutana na watoto wengine waliokuwa viziwi. Luga ya ishara ilikatazwa pia kwenye masomo hayo. Ikiwa tulijaribu kuzungumuza kwa kufanya ishara, mwalimu alitufunga vidole ao kutukokota nywele za kichwa. Hata hivyo, tulizungumuza kwa siri kwa kutumia alama ambazo sisi wenyewe tulitunga. Mwishowe, niliweza kuzungumuza na watoto wengine waliokuwa viziwi. Kwa hiyo, miaka ine ya furaha ikaanza.

Hata hivyo, nilipokuwa na miaka kumi, nilihamishwa kwenye masomo ya musingi pamoja na watoto wenye kusikia. Nilihuzunika sana! Nilifikiri kwamba watoto wengine wote viziwi walikuwa wamekufa na kwamba nilibaki peke yangu katika dunia. Kwa kufuata mashauri ya waganga, ambao waliogopa kwamba ningepoteza faida za matunzo ya kujua kusema niliyopata, watu wa familia yetu hawakujifunza luga ya ishara na sikuruhusiwa kujiunga na watoto ambao walikuwa viziwi. Mupaka sasa, ningali ninakumbuka wakati nilimutembelea muganga mumoja aliyekuwa akisaidia viziwi kusikia, na muganga huyo alikuwa na kitabu fulani cha luga ya ishara kwenye meza yake. Nilipoona picha za jalada ya kitabu hicho, nilionyesha kwa kidole kitabu hicho, na kusema “Ninataka kitabu hicho!” Muganga alificha haraka kitabu hicho. *

NINAANZA KUJIFUNZA BIBLIA

Mama alijikaza kutulea kulingana na kanuni za Kikristo. Alikuwa akitupeleka kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova wa kutaniko la Mérignac, karibu na Bordeaux. Nikiwa mutoto, sikuelewa mambo mengi kwenye mikutano. Hata hivyo, washiriki mbalimbali wa kutaniko walikuwa wanakaa pembeni yangu ili kuniandikia mambo yaliyokuwa yanafundishwa kwenye mikutano. Niliguswa moyo sana na upendo wao na namna walivyonishugulikia. Nyumbani, Mama alinifundisha Biblia, lakini sikuelewa kabisa mambo aliyokuwa akinifundisha. Katika njia fulani, nilijisikia kama nabii Danieli, ambaye, kisha kupokea unabii kutoka kwa malaika, alisema hivi: “Nikasikia, lakini sikuweza kuelewa.” (Danieli 12:8) Tofauti na Danieli, mimi “Niliona, lakini sikuweza kusikia.”

Hata hivyo, hatua kwa hatua nilijifunza kweli za musingi za Biblia. Nilisamini sana mambo niliyoelewa waziwazi na nilijikaza kuyatumikisha katika maisha yangu. Pia, nilijifunza mambo kwa kutazama mwenendo wa watu wengine. Kwa mufano, Biblia inatufundisha kuwa wenye subira na uvumilivu. (Yakobo 5:7, 8) Lakini sikuelewa kabisa maana ya kuwa mwenye subira na uvumilivu. Hata hivyo, kwa kuchunguza namna waamini wenzangu walivyoonyesha sifa hizo, niliweza kuelewa maana ya sifa ya subira na uvumilivu. Kwa kweli, kutaniko la Kikristo limekuwa musaada mukubwa kwangu.

NINAVUNJIKA MOYO SANA LAKINI JAMBO LISILOTAZAMIWA LINATOKEA

Stéphane aliyenisaidia kuielewa Biblia

Siku moja, nilipokuwa kijana, niliona kwenye barabara vijana fulani waliokuwa viziwi wakizungumuza katika luga ya ishara. Nilianza kukutana nao kwa siri na nikaanza kujifunza Luga ya Ishara ya France. Niliendelea kuhuzuria mikutano ya Kikristo, mahali ambapo Stéphane, Shahidi mumoja kijana alipendezwa na mimi. Alifanya bidii sana ili kuzungumuza na mimi na kwa hiyo nikajisikia moyoni kuwa ninamupenda sana. Hata hivyo, sikujua kwamba jambo fulani lenye kuvunja moyo lingetokea. Stéphane alikamatwa na kutiwa katika gereza kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi. Kwa kuwa Stéphane alikamatwa na kufungwa, nilivunjika moyo sana na mwishowe nikaacha kuhuzuria mikutano.

Miezi 11 baadaye, Stéphane aliachiliwa na kurudi nyumbani. Fikiria namna nilivyoshangaa nilipomuona anaanza kuzungumuza na mimi kwa kutumia luga ya ishara. Sikuamini mambo ambayo nilikuwa ninaona! Stéphane alijua namna gani luga hiyo? Alipokuwa katika gereza, alijifunza luga ya ishara ya France. Nilipokuwa nikichunguza namna Stéphane alivyokuwa akitumia mikono yake na ishara za uso, furaha yangu iliendelea kuongezeka nilipofikiria maana ya mambo hayo kwangu.

MWISHOWE NINAELEWA KWELI YA BIBLIA

Stéphane alianza kunifundisha Biblia. Tangu wakati huo na kuendelea, nilianza kukusanya pamoja kweli zote za Biblia ambazo nilikuwa nimejifunza zamani. Nilipokuwa mutoto, nilipenda kutazama picha nzuri zilizo katika vichapo vyetu, na nililinganisha watu waliokuwa kwenye picha hizo na kuchunguza kwa uangalifu mambo madogo-madogo ili kukazia habari hizo katika akili yangu. Nilijua mafundisho juu ya Abrahamu, “uzao” wake, na ‘umati mukubwa,’ lakini ilikuwa tu wakati mafundisho hayo yalielezwa katika luga ya ishara ndipo niliyaelewa vizuri zaidi. (Mwanzo 22:15-18; Ufunuo 7:9) Ilikuwa wazi kwamba nilikuwa sasa nimeipata luga yangu, luga inayogusa moyo wangu.

Kwa kuwa sasa nilielewa mambo yaliyofundishwa kwenye mikutano, moyo wangu uliguswa sana na kiu changu cha ujuzi kiliendelea kuongezeka. Nikisaidiwa na Stéphane, uelewaji wangu wa Biblia uliendelea kuongezeka, na katika mwaka wa 1992, nilijitoa kwa Yehova Mungu katika sala na kubatizwa. Hata hivyo, ijapokuwa nilikuwa nimefanya maendeleo fulani, ilikuwa vigumu kwangu kuzungumuza na watu wengine kwa sababu nilikuwa bado mwenye haya kwa kuwa tangu utoto wangu sikuzoea kuongea na watu.

NINAJIKAZA KUSHINDA HALI YANGU YA KUWA MWENYE HAYA

Mwishowe, kikundi chetu kidogo cha viziwi kiliunganishwa na kutaniko moja la huko Pessac, kijiji kilicho katika eneo la Bordeaux. Kujiunga na kutaniko hilo kulinisaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho. Ijapokuwa nilikuwa bado ninajikaza kushinda hali yangu ya kutoweza kuzungumuza na wengine, marafiki wangu ambao hawakuwa viziwi walikuwa waangalifu ili kuhakikisha kwamba nilielewa kila kitu. Gilles na Elodie, ambao ni bwana na bibi, walifanya bidii ya pekee ili kuzungumuza na mimi. Mara nyingi, walinialika nyumbani kwao kisha mikutano ili kula chakula pamoja ao kunywa kikombe cha kahawa na hivyo urafiki wetu ukakolea. Ni shangwe ao furaha kubwa sana kuwa kati ya watu wanaofuata njia za Mungu zenye upendo!

Bibi yangu Vanessa, ananisaidia kwelikweli

Katika kutaniko la Pessac, nilikutana na Vanessa, mwanamuke mwenye sura nzuri. Nilivutiwa na sifa yake ya kuwafikiria watu wengine na kufuatia haki. Hakuona hata kidogo kwamba hali yangu ya kuwa kiziwi ilikuwa kizuizi, lakini aliona hali yangu kuwa nafasi ya kujifunza namna ya kuongea na watu ambao ni viziwi. Nilipendezwa naye, na katika mwaka wa 2005 tulifunga ndoa. Hata kama ilikuwa vigumu kwangu kuzungumuza naye, Vanessa alinisaidia sana kushinda hali yangu ya kuwa mwenye haya na hivyo nikaanza kuongea waziwazi na watu. Kwa kweli, ninafurahia musaada wake ninapoendelea kutimiza madaraka yangu.

ZAWADI NYINGINE KUTOKA KWA YEHOVA

Katika mwaka huo tuliofunga ndoa, biro ya tawi ya France ya Mashahidi wa Yehova huko Louviers ilinialika kwa muda wa mwezi mumoja ili kuzoezwa kwa ajili ya kazi ya kutafsiri. Katika miaka ya hivi karibuni, biro hiyo ilikuwa ikifanya kazi kwa bidii sana ili kutoa vichapo vingi katika luga ya ishara ya France kwenye DVD. Lakini kwa kuwa kazi ilikuwa nyingi sana, kikundi cha kutafsiri luga ya ishara kilihitaji musaada.

Ninatoa hotuba yenye kutegemea Biblia katika Luga ya Ishara ya France

Mimi na Vanessa tuliona kwamba mimi kutumika kwenye biro ya tawi ni pendeleo kubwa sana na zawadi kutoka kwa Yehova Mungu, lakini ni lazima nikubali pia kwamba tulikuwa na wasiwasi. Mambo yangekuwa namna gani kuhusu kikundi chetu cha luga ya ishara? Tungefanya nini juu ya nyumba yetu? Je, Vanessa angepata kazi katika eneo hilo? Yehova alijibu maulizo hayo kwa njia ya ajabu sana. Kwa kweli, niliona upendo wa Yehova kunielekea mimi na Vanessa, na pia kuelekea watu ambao ni viziwi.

NINATEGEMEZWA NA WATU WENYE UMOJA

Kwa sababu nilihusika katika kazi ya kutafsiri, ninaelewa vizuri sana kazi yote inayofanywa ili kuwasaidia viziwi wajifunze kumujua Mungu. Na ni furaha kubwa kuona wafanyakazi wenzangu wakijikaza kuzungumuza na mimi. Ninaguswa moyo kuona namna wanavyojifunza ishara fulani-fulani ili kujaribu kuzungumuza na mimi. Sijisikie hata kidogo kuwa ninapuuzwa. Njia hizo zote za kuonyesha upendo zinahakikisha waziwazi umoja wa ajabu ulio kati ya watu wa Yehova.​—Zaburi 133:1.

Nikifanya kazi katika Idara ya Utafsiri kwenye biro ya tawi

Ninamushukuru Yehova kwa sababu kupitia kutaniko la Kikristo, sikuzote amehakikisha kwamba kumekuwa mutu wa kunisaidia. Ninasamini pia daraka ndogo ambalo nimepewa la kuwasaidia viziwi wenzangu kumujua Muumbaji wetu mwenye upendo na kumukaribia. Ninangojea wakati ambapo vizuizi vyote vinavyofanya iwe vigumu kupashana habari vitaondolewa na wakati watu wote watazungumuza ‘luga safi,’ ni kusema, ukweli juu ya Yehova Mungu na makusudi yake, tukiwa sehemu ya familia ya wanadamu yenye umoja.​—Sefania 3:9.

^ Ni katika mwaka wa 1991 ndipo serikali ya France iliruhusu kisheria kuanza kutumia luga ya ishara ili kuwafundisha watoto waliokuwa viziwi.