Hamia kwenye habari

Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Nikishuka Moyo?

Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Nikishuka Moyo?

Jibu la Biblia

 Ndiyo, kwa sababu msaada bora zaidi hutoka kwa “Mungu, Ambaye huwafariji na kuwatia moyo na kuwaburudisha na kuwachangamsha walioshuka moyo.”​—2 Wakorintho 7:6, The Amplified Bible.

Msaada ambao Mungu huwapa walioshuka moyo

  •   Nguvu. Mungu ‘hukuburudisha na kukuchangamsha’ si kwa kuondoa matatizo yako, bali kwa kujibu sala zako unapoomba nguvu za kukabiliana na tatizo lako. (Wafilipi 4:13) Unaweza kuwa na uhakika kwamba yuko tayari kukusikiliza, kwa kuwa Biblia inasema: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Zaburi 34:18) Kwa kweli, Mungu anaweza kusikiliza sala zako za kuomba msaada hata ikiwa unashindwa kumweleza vizuri hisia zako.​—Waroma 8:26, 27.

  •   Mifano mizuri. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisali hivi kwa Mungu: “Toka upeo wa unyonge wangu, nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu.” Mtunga-zaburi huyu alikabiliana na mshuko wa moyo kwa kukumbuka kwamba Mungu hataki tulemewe na hisia za hatia. Badala yake, alimwambia Mungu hivi: “Kama ee Mwenyezi-Mungu ungekumbuka maovu yetu nani ee Bwana, angeweza kusalimika? Lakini kwako twapata msamaha, ili sisi tukuheshimu.”​—Zaburi 130:1, 3, 4, Biblia Habari Njema.

  •   Tumaini. Mbali na kutufariji sasa, Mungu ameahidi kuondoa matatizo yote yanayotufanya tushuke moyo. Wakati atakapotimiza ahadi hiyo, “mambo ya zamani [kutia ndani kushuka moyo] hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.”​—Isaya 65:17.

 Taarifa: Ingawa Mashahidi wa Yehova wanakubali msaada ambao Mungu huandaa, wao pia hutafuta matibabu ya magonjwa kama vile kushuka moyo sana. (Marko 2:17) Hata hivyo, hatupendekezi matibabu yoyote hususa; kila mtu anapaswa kufanya uamuzi wake kuhusiana na matibabu.