Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Ni Nini Kinachoweza Kuwasaidia Vijana Walioshuka Moyo?

Ni Nini Kinachoweza Kuwasaidia Vijana Walioshuka Moyo?

BINTI anayeitwa Anna, * anasema hivi: “Ninaposhuka moyo ninakosa hamu ya kufanya chochote, hata mambo ambayo kwa kawaida huwa napenda kufanya. Kitu pekee ninachotaka ni kulala. Mara nyingi ninahisi kwamba watu hawanipendi, sina thamani, na mimi ni mzigo kwa wengine.”

Julia anakumbuka hivi: “Nilifikiria kujiua. Kusema kweli sikutaka kufa. Nilitaka tu kuepuka hisia mbaya nilizokuwa nazo. Kwa kawaida mimi ni mwenye kujali sana, lakini ninaposhuka moyo, sijali yeyote wala kitu chochote.”

Anna na Julia walikuwa na umri wa miaka 13 na 14 hivi waliposhuka moyo kwa mara ya kwanza. Ni kawaida kwa vijana kuhisi vibaya nyakati fulani, lakini tofauti na hilo, Anna na Julia walishuka moyo kwa majuma au hata miezi kadhaa. Anna anasema kwamba, kushuka moyo “ni kama kufungiwa kwenye shimo kubwa lenye giza na lisilokuwa na mlango wa kutokea.” Anaongeza hivi: “Unahisi kama unarukwa na akili, na kwamba umebadilika kabisa tofauti na ulivyokuwa zamani.”

Watu wengi wamepatwa na hali kama ya Anna na Julia. Idadi ya vijana wanaoshuka moyo inaongezeka kwa kasi sana. Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) linasema kwamba, kushuka moyo ni “chanzo kikuu cha magonjwa na ulemavu kwa wavulana na wasichana wenye umri kati ya miaka 10 na 19.”

Dalili za kushuka moyo zinaweza kuonekana wakati wa kubalehe na zinahusisha mabadiliko katika mazoea ya kulala, hamu ya kula, na kuongezeka au kupungua uzito. Pia, mtu anaweza kuanza kuhisi hana tumaini lolote, huzuni, na kwamba hafai kitu. Ishara zingine ni kama kujitenga na wengine, kushindwa kukazia fikira au kupoteza kumbukumbu, kutaka kujiua, na kuonyesha dalili ambazo hazihusiani na ugonjwa wowote. Wataalamu wa afya wanapohisi kwamba mtu ameshuka moyo, wao huchunguza ikiwa mtu huyo ameonyesha dalili zaidi ya moja zinazodumu kwa majuma kadhaa na ambazo zinaathiri maisha yake ya kila siku.

MAMBO YANAYOWEZA KUSABABISHA KIJANA ASHUKE MOYO

Kulingana na WHO, “kushuka moyo husababishwa na muunganiko tata wa hali za kijamii, kisaikolojia, na kibiolojia.” Hali hizo zinatia ndani mambo yafuatayo.

Matatizo ya kibiolojia na matumizi ya dawa. Kama ilivyokuwa katika kisa cha Julia, mara nyingi tatizo la kushuka moyo huwapata watu kadhaa katika familia moja, jambo linalodokeza kwamba chembe za urithi zinahusika, labda kwa kuathiri utendaji wa kemikali kwenye ubongo. Visababishi vingine ni; ugonjwa wa moyo, mabadiliko ya viwango vya homoni, na matumizi ya dawa za kulevya. Dawa za kulevya zikitumiwa kwa muda mrefu zinaweza kuongeza uwezekano wa mtu kushuka moyo. *

Mkazo. Ingawa mkazo kidogo unaweza kuwa na manufaa, kuwa na mkazo kwa muda mrefu kunaweza kumdhuru mtu kimwili na kisaikolojia, na nyakati nyingine hata kusababisha kijana mwenye matatizo ya kibiolojia ashuke moyo. Pamoja na yote hayo, bado sababu hususa zinazofanya watu washuke moyo hazifahamiki vizuri na zinaweza kuhusisha mambo mbalimbali kama ilivyotajwa awali.

Huenda mkazo unaoweza kusababisha kijana ashuke moyo ukatokana na wazazi kutalikiana au kutengana, kifo cha mpendwa, kutendewa vibaya kimwili au kingono, aksidenti mbaya, ugonjwa, au mtoto kuwa mzito kujifunza, hasa ikiwa anahisi kwamba anabaguliwa. Pia, mkazo unaweza kusababishwa na matarajio ya juu sana kutoka kwa wazazi, labda inapohusu masuala ya elimu. Uonevu shuleni, wasiwasi kuhusu wakati ujao, uhusiano mbaya na mzazi aliyeshuka moyo, na watoto kushindwa kuelewa hisia na matendo ya wazazi wao ni baadhi ya mambo yanayoweza kuwasababishia mkazo pia. Kijana anaweza kufanya nini ili akabiliane na kushuka moyo?

TUNZA AKILI NA MWILI WAKO

Kwa kawaida, mtu aliyeshuka moyo kupita kiasi anahitaji matibabu na ushauri kutoka kwa wataalamu wa afya ya akili. * Yesu Kristo alisema hivi: “Wale walio na nguvu hawahitaji tabibu, bali wale walio wagonjwa wanamhitaji.” (Marko 2:17) Ugonjwa unaweza kuathiri sehemu yoyote ile ya mwili wetu kutia ndani ubongo! Ni vizuri pia kubadili mtindo wa maisha kwa sababu kuna uhusiano mkubwa kati ya ubongo na mwili wetu.

Ikiwa umeshuka moyo, chukua hatua madhubuti zitakazokusaidia kutunza afya ya mwili na akili yako. Kwa mfano, kula vyakula vyenye lishe, lala vya kutosha, na uwe na kawaida ya kufanya mazoezi. Mazoezi huchochea uzalishaji wa kemikali zinazoweza kukufanya ujihisi vizuri, kukuchangamsha, na kuboresha usingizi wako. Ikiwezekana, jaribu kutambua dalili za mapema za kushuka moyo kisha upange jinsi utakavyoshughulikia hali hiyo. Zungumza na mtu unayemwamini. Kuwa na marafiki na washiriki wa karibu wa familia wanaokuunga mkono kutakusaidia unaposhuka moyo au hata kupunguza madhara ya tatizo hilo. Andika mawazo na hisia zako kwenye daftari. Zoea hilo lilimsaidia sana Julia, aliyetajwa awali. Zaidi ya yote, hakikisha unatosheleza uhitaji wako wa kiroho. Hilo linaweza kuboresha mtazamo wako wa maisha kwa kiwango kikubwa sana. Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Kula vizuri, fanya mazoezi, na ulale vya kutosha

Utafarijika ikiwa utatosheleza uhitaji wako wa kiroho

Anna na Julia wamefaidika kwa kufuata ushauri wa Yesu. Anna anasema: “Utendaji wa kiroho huniwezesha kukazia fikira watu wengine badala ya matatizo yangu. Hilo si rahisi siku zote, lakini kufanya hivyo huongeza furaha yangu.” Julia anapata faraja kwa kusali na kusoma Biblia. Anasema hivi: “Kummiminia Mungu moyo wangu hufanya nitulie. Na Biblia hunisaidia kuona kwamba nina thamani machoni pa Mungu, naye ananijali kikweli. Pia, kusoma Biblia hunifanya niwe na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao.”

Akiwa Muumba wetu, Yehova Mungu anaelewa kikamili jinsi malezi yetu, mambo tuliyopitia maishani, na chembe zetu za urithi zinavyoathiri mtazamo na hisia zetu. Hivyo, anaweza kutoa faraja na msaada unaohitajika, labda kwa kumtumia mwanadamu mwenzetu mwenye huruma na anayeweza kuelewa vizuri hali zetu. Isitoshe, wakati ujao, Mungu ataponya magonjwa yote, ya kimwili na ya akili. Andiko la Isaya 33:24 linasema: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”

Naam, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Ahadi hii inafariji na kutia moyo sana! Ikiwa ungependa kujifunza zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu, tafadhali tembelea tovuti yetu ya jw.org/sw. Katika tovuti hiyo unaweza kusoma tafsiri nzuri ya Biblia na pia kupata makala zenye habari mbalimbali kutia ndani zinazohusu kushuka moyo.

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 10 Ni muhimu kuchunguzwa kwa makini na wataalamu, kwa kuwa kuna vitu vingi vinavyoweza kuathiri hisia za mtu, kama vile magonjwa, matibabu, na dawa za kulevya.

^ fu. 14 Gazeti la Amkeni! halipendekezi mazoezi au matibabu fulani hususa.