Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa Fungu la Kumi?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa Fungu la Kumi?

Jibu la Biblia

 Ili kutoa michango ya kutegemeza ibada ya kweli, Waisraeli wa kale waliamriwa watoe fungu la kumi la mapato yao ya kila mwaka. Mungu aliwaambia hivi: “Ni lazima mtoe sehemu ya kumi [“zaka ya fungu la kumi,” Union Version] ya mazao ya shambani yanayotokana na mbegu zenu mwaka baada ya mwaka.”—Kumbukumbu la Torati 14:22.

 Amri ya kutoa fungu la kumi ilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa, sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale. Wakristo hawajafungwa kisheria kufuata Sheria ya Musa hivyo si takwa kwao kutoa fungu la kumi. (Wakolosai 2:13, 14) Badala yake, kila Mkristo anapaswa kutoa mchango wa kifedha “kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:7.

 Fungu la Kumi Katika Biblia​—“Agano la Kale”

 Fungu la kumi linatajwa mara kadhaa katika sehemu ya Biblia inayojulikana kama Agano la Kale. Linaonekana hasa katika kipindi baada ya Sheria ya Musa kutolewa kwa taifa la Israeli kupitia Musa. Hata hivyo, linaonekana mara chache baada ya kipindi hicho.

Kabla ya Sheria ya Musa

 Mtu wa kwanza anayetajwa katika Biblia kutoa fungu la kumi ni Abramu (Abrahamu). (Mwanzo 14:18-20; Waebrania 7:4) Inaonekana kwamba Abramu alimpa mfalme na kuhani wa Salemu fungu la kumi mara moja tu kama zawadi. Hakuna uthibitisho katika Biblia unaoonyesha kwamba Abrahamu au watoto wake waliwahi kutoa fungu la kumi tena.

 Mtu wa pili anayetajwa katika Biblia kuwa alitoa fungu la kumi ni Yakobo, mjukuu wa Abrahamu. Aliahidi kwamba ikiwa Mungu angembariki, basi angempa Mungu “sehemu ya kumi ya vitu vyote” alivyopokea. (Mwanzo 28:20-22) Kulingana na wasomi fulani wa Biblia, huenda Yakobo alilipa fungu hilo la kumi kwa kutoa dhabihu za wanyama. Ingawa Yakobo alitimiza kiapo hicho, hakuwalazimisha washiriki wa familia yake kutoa fungu hilo la kumi.

Chini ya Sheria ya Musa

 Waisraeli wa kale waliamriwa watoe fungu la kumi kama njia ya kutegemeza utendaji wao wa kidini.

  •   Fungu la kumi liliwaandalia mahitaji ya lazima wafanyakazi wa wakati wote wa kidini—Walawi, kutia ndani makuhani—kwa kuwa hawakuwa na ardhi ya kulima. (Hesabu 18:20, 21) Walawi ambao hawakuwa makuhani walipokea fungu la kumi kutoka kwa watu kisha walitoa “sehemu ya kumi kutoka katika sehemu hiyo ya kumi” kwa ajili ya makuhani.—Hesabu 18:26-29.

  •   Inaonekana kwamba kulikuwa na pindi nyingine ya pili ambapo fungu la kumi lilipaswa kutolewa, na Walawi pamoja na wasio Walawi walifaidika. (Kumbukumbu la Torati 14:22, 23) Familia za Waisraeli zilitumia uandalizi huo kulipokuwa na sherehe za pekee, na katika miaka fulani waliokuwa maskini sana waligawiwa sehemu fulani ya kilichotolewa ili wapate chakula.—Kumbukumbu la Torati 14:28, 29; 26:12.

 Fungu la kumi lilihesabiwaje? Waisraeli waliweka kando sehemu ya kumi ya mavuno ya mwaka mzima. (Mambo ya Walawi 27:30) Iwapo wangechagua kulipa fungu hilo la kumi kwa pesa badala ya mavuno, walipaswa kuongeza thamani yake kwa asilimia 20. (Mambo ya Walawi 27:31) Pia waliamriwa kutoa “sehemu ya kumi ya mifugo na ya kundi.”—Mambo ya Walawi 27:32.

 Ili kutambua fungu la kumi la mifugo yao, Waisraeli waliteua kila mnyama wa kumi aliyetoka zizini mwao. Sheria ilisema kwamba hawakupaswa kuchunguza au kubadili wanyama hao walioteuliwa, wala hawakupaswa kubadili fungu la kumi la mifugo kwa pesa. (Mambo ya Walawi 27:32, 33) Hata hivyo, fungu la kumi lililotolewa mara ya pili katika sherehe zao za kila mwaka lingeweza kubadilishwa kwa pesa. Uandalizi huo ulifanya iwe rahisi zaidi kwa Waisraeli waliolazimika kusafiri mbali sana ili kuhudhuria sherehe hizo.—Kumbukumbu la Torati 14:25, 26.

 Waisraeli walitoa fungu la kumi lini? Waisraeli walitoa fungu la kumi kila mwaka. (Kumbukumbu la Torati 14:22) Hata hivyo, mwaka wa saba hali ilikuwa tofauti. Mwaka huo ulikuwa wa Sabato, au mwaka wa kupumzika, wakati ambapo Waisraeli hawakulima mimea yoyote. (Mambo ya Walawi 25:4, 5) Kwa sababu hiyo ya pekee, fungu la kumi halikukusanywa wakati wa mavuno. Baada ya kila mwaka wa tatu na wa sita wa mzunguko wa Sabato ya miaka saba, Waisraeli walitoa fungu la kumi mara ya pili ili maskini na Walawi wafaidike kutokana nalo.—Kumbukumbu la Torati 14:28, 29.

 Kulikuwa na adhabu gani kwa kukosa kutoa fungu la kumi? Sheria ya Musa haikusema kwamba mtu angeadhibiwa. Waisraeli walipaswa kutoa fungu la kumi kwa sababu walijua ndilo jambo linalofaa, si kwa sababu wangeadhibiwa ikiwa wangekosa kufanya hivyo. Waisraeli walipaswa kutangaza mbele za Mungu kwamba walikuwa wametoa fungu la kumi na kumwomba Mungu baraka kwa sababu walifanya hivyo. (Kumbukumbu la Torati 26:12-15) Kwa maoni ya Mungu, kukosa kutoa fungu la kumi kulikuwa sawa na kumwibia.—Malaki 3:8, 9.

 Je, fungu la kumi lilikuwa mzigo mzito? Hapana. Mungu aliahidi taifa hilo kwamba ikiwa wangetoa fungu la kumi, angewamwagia baraka hivi kwamba hawangekosa chochote. (Malaki 3:10) Kwa upande mwingine, taifa liliteseka kwa sababu ya kukosa kutoa fungu la kumi. Walipoteza baraka za Mungu. Pia, kwa kuwa makuhani na Walawi wangelazimika kufanya kazi ili kuandaa mahitaji yao wenyewe, hawangeweza kukazia fikira kazi yao ya kulisaidia taifa la Israeli kumwabudu Mungu.—Nehemia 13:10; Malaki 3:7.

 Fungu la Kumi Katika Biblia​—“Agano Jipya”

 Wakati wa maisha ya Yesu akiwa mwanadamu, bado fungu la kumi lilikuwa takwa kwa wale waliomwabudu Mungu. Hata hivyo, takwa hilo liliondolewa baada ya Yesu kufa.

Wakati wa Yesu

 Katika ile sehemu ya Biblia inayojulikana sana kuwa Agano Jipya, tunasoma kwamba Waisraeli waliendelea kutoa fungu la kumi Yesu alipokuwa duniani. Alikubali kwamba kutoa fungu la kumi kulikuwa takwa kwao, lakini aliwashutumu viongozi wa kidini waliozingatia kutoa fungu la kumi lakini ‘walipuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki, rehema, na uaminifu.’—Mathayo 23:23.

Baada ya kifo cha Yesu

 Fungu la kumi halikuwa takwa tena baada ya kifo cha Yesu. Kifo cha Yesu cha kidhabihu kilifutilia mbali, au kuondoa kabisa, Sheria ya Musa, kutia ndani “amri ya kukusanya sehemu za kumi.”—Waebrania 7:5, 18; Waefeso 2:13-15; Wakolosai 2:13, 14.