Hamia kwenye habari

Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?

Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?

Jibu la Biblia

 Hapana, Ufalme wa Mungu si hali fulani iliyomo katika mioyo ya Wakristo. a Biblia inataja mahali ambapo ufalme huo upo kwa kuuita “ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 4:​17, Biblia Habari Njema) Ona jinsi Biblia inavyoonyesha kwamba ufalme huo ni serikali halisi inayotawala kutoka mbinguni.

 Biblia haifundishi kwamba Ufalme wa mbinguni umo katika moyo wako katika maana ya kwamba unatawala kupitia moyo wa mtu. Badala yake, inaonyesha kwamba “neno la Ufalme” au “habari njema ya Ufalme” inaweza na inapaswa kugusa mioyo yetu.​—Mathayo 13:19; 24:14.

Maneno “ufalme wa Mungu umo ndani yenu” yanamaanisha nini?

 Tafsiri fulani za Biblia zimewafanya watu fulani wachanganyikiwe kuhusu mahali ambapo Ufalme upo kutokana na jinsi tafsiri hizo zinavyosema katika Luka 17:21. Kwa mfano, tafsiri ya Union Version inasema kwamba “ufalme wa Mungu umo ndani yenu.” Ili kuelewa mstari huo kwa usahihi, tunapaswa kuchunguza muktadha.

Ufalme wa Mungu haukuwa katika mioyo ya watu wakaidi, wauaji, na waliompinga Yesu

 Yesu alikuwa akizungumza na Mafarisayo, kikundi cha viongozi wa kidini waliompinga na walioshiriki katika mipango ya kumuua. (Mathayo 12:14; Luka 17:20) Je, inapatana na akili kufikiri kwamba Ufalme ulikuwa hali fulani iliyo ndani ya mioyo yao yenye ukaidi? Yesu aliwaambia: “Ndani mmejaa unafiki na uasi-sheria.”​—Mathayo 23:27, 28.

 Tafsiri nyingine hufafanua kwa usahihi maneno ya Yesu katika Luka 17:21: “Ufalme wa Mungu uko hapa pamoja nanyi.” (Italiki ni zetu; Contemporary English Version) “Ufalme wa Mungu umo katikati yenu.” (Tafsiri ya Ulimwengu Mpya) Ufalme wa mbinguni ulikuwa “pamoja” au “katikati” ya Mafarisayo, katika maana ya kwamba Yesu, yule aliyeteuliwa na Mungu ili kutawala akiwa Mfalme, alikuwa amesimama mbele yao.​—Luka 1:​32, 33.

a Dini nyingi za Kikristo zinafundisha kwamba Ufalme wa Mungu umo ndani ya mtu, au ndani ya moyo wa mtu. Kwa mfano, nchini Marekani, kanisa fulani la Baptisti (Southern Baptist Convention) lilisema kwamba Ufalme wa Mungu ni sehemu ya “utawala wa Mungu katika moyo na maisha ya mtu mmoja-mmoja.” Vivyo hivyo, katika kitabu chake Jesus of Nazareth, Papa Benedict wa 16 alisema kwamba “Ufalme wa Mungu unakuja kupitia moyo msikivu.”