Hamia kwenye habari

Mwisho wa Ulimwengu Utakuja Lini?

Mwisho wa Ulimwengu Utakuja Lini?

Jibu la Biblia

 Ili kujua mwisho wa ulimwengu, au mwisho wa dunia, utakuja wakati gani, ni muhimu kujua jinsi Biblia inavyotumia neno “ulimwengu.” Neno la Kigiriki koʹsmos, ambalo mara nyingi hutafsiriwa kuwa “ulimwengu,” humaanisha ulimwengu wa wanadamu, hasa ulimwengu ambao hautendi kupatana na mapenzi ya Mungu. (Yohana 15:18, 19; 2 Petro 2:5) Nyakati nyingine, koʹsmos hurejelea mfumo wa ulimwengu huu.​—1 Wakorintho 7:​31; 1 Yohana 2:​15, 16. a

“Mwisho wa dunia” ni nini?

 Maneno “mwisho wa dunia,” yanayotajwa katika tafsiri nyingi za Biblia, yanaweza pia kutafsiriwa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3; Union Version) Maneno hayo hayarejelei kuharibiwa kwa dunia au kwa wanadamu wote, bali yanarejelea mwisho wa mfumo wa ulimwengu huu.​—1 Yohana 2:​17.

 Biblia inafundisha kwamba “watenda-maovu watakatiliwa mbali” ili watu wema wafurahie maisha duniani. (Zaburi 37:9-11) Uharibifu huo utatukia wakati wa ile “dhiki kuu,” ambayo sehemu yake ya mwisho ni vita vya Har-Magedoni.​—Mathayo 24:21, 22; Ufunuo 16:14, 16.

Ulimwengu utakwisha lini?

 Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36, 42) Aliongezea kusema kwamba wakati huo utakuja bila kutazamiwa, “katika saa msiyofikiria.”​—Mathayo 24:44.

 Hata ingawa hatuwezi kujua siku na saa hususa, Yesu alitupa “ishara” yenye mambo mengi ambayo ingetambulisha kipindi kinachoongoza kwenye mwisho wa ulimwengu. (Mathayo 24:​3, 7-​14) Biblia inataja kipindi hicho kuwa “wakati wa mwisho,” na “siku za mwisho.”​—Danieli 12:4; 2 Timotheo 3:​1-5.

Je, kuna chochote kitakachobaki baada ya mwisho wa ulimwengu?

 Ndiyo. Dunia bado itakuwapo, kwa kuwa Biblia inasema kwamba “haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Na dunia itakuwa imejaa wanadamu, kama Biblia inavyoahidi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Mungu ataleta hali ambazo alikusudia awali:

a Neno la Kigiriki ai·onʹ linatafsiriwa pia katika Biblia fulani kuwa “ulimwengu.” Linapotafsiriwa hivyo, neno ai·onʹ linamaanisha jambo lilelile kama koʹsmos yaani, mfumo wa ulimwengu huu.