Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Marko 11:24—“Mnaposali na Kuomba Kitu, Aminini Kwamba Mmekipokea”

Marko 11:24—“Mnaposali na Kuomba Kitu, Aminini Kwamba Mmekipokea”

 “Ndiyo sababu ninawaambia, mambo yote mnayosali na kuomba, iweni na imani kwamba mmeyapokea, nanyi mtayapata.”​—Marko 11:24, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Kwa hiyo nawaambieni, mnaposali na kuomba kitu, aminini kwamba mmekipokea, nanyi mtapewa.”​—Marko 11:24, Biblia Habari Njema.

Maana ya Marko 11:24

 Kwa maneno hayo, Yesu aliwaonyesha wafuasi wake jinsi ilivyo muhimu kwao kuwa na imani nyingi katika nguvu za sala. Aliwahakikishia kwamba si eti Mungu anasikiliza sala tu, bali anazijibu pia. Mtu anayesali kwa unyoofu kupatana na mapenzi ya Mungu anaweza kuwa na uhakika kwamba kile anachoomba kitatimia. Ni kana kwamba tayari sala hiyo imeshajibiwa.

 Yesu alikazia umuhimu wa kusali kwa imani. Alieleza kwamba yule anayesali hapaswi “kuwa na shaka moyoni mwake” lakini anapaswa kuwa na “imani kwamba yale anayosema yatatukia.” (Marko 11:23) Kwa nini? Kwa sababu wale walio na shaka hawawezi kutarajia “kupokea kitu chochote kutoka kwa Yehova.” aYakobo 1:5-8.

 Mtu mwenye imani husali mara nyingi. (Luka 11:9, 10; Waroma 12:12) Kwa njia hiyo, anaonyesha kwamba kwa kweli anahitaji anachoomba na kwamba kwa kweli anaamini Mungu anaweza kujibu sala yake. Bila shaka, anakubali pia kwamba Mungu anaweza kuamua kujibu sala yake kwa njia tofauti na ile anayotarajia na anaweza kufanya hivyo wakati tofauti na ule anaotazamia.​—Waefeso 3:20; Waebrania 11:6.

 Hata hivyo, maneno ya Yesu hayamaanishi kwamba mtu yeyote anaweza kutarajia kupata chochote anachomwomba Mungu. Yesu alikuwa akizungumza na wafuasi wake, watu wenye imani waliokuwa wakifanya yote wawezayo ili kumwabudu Yehova Mungu kwa njia inayokubalika. Biblia inasema kwamba Yehova anasikiliza tu sala zinazotolewa kulingana na mapenzi yake. (1 Yohana 5:14) Hasikilizi sala za wale wanaopuuza kimakusudi viwango vyake na ambao wanafanya mambo mabaya bila kutubu. (Isaya 1:15; Mika 3:4; Yohana 9:31) Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu sala ambazo Mungu husikiliza, tazama video hii fupi.

Muktadha wa Marko 11:24

 Katika siku za mwisho za huduma yake duniani, Yesu alizungumza na wanafunzi wake kuhusu umuhimu wa kuonyesha imani yenye nguvu katika Mungu. Alikazia somo hilo kwa kutumia mfano. Alipokuwa akisafiri kwenda Yerusalemu, aliona mtini uliokuwa umechanua majani mapema. Hata hivyo, mti huo haukuwa na matunda yoyote, kwa hiyo Yesu akaulaani. (Marko 11:12-14) Mwonekano wenye kupumbaza wa mti huo ulilingana na jinsi taifa la kale la Israeli lilivyokuwa. Kwa nje walionekana kana kwamba wanamwabudu Mungu lakini kwa kweli hawakuwa na imani. (Mathayo 21:43) Muda mfupi baada ya hapo, mtini huo ulinyauka. Jambo hilo lilionyesha kile ambacho kingelipata taifa la Israeli lisilo na imani.​—Marko 11:19-21.

 Tofauti na hilo, Yesu alisadiki kwamba wafuasi wake wangesitawisha imani iliyohitajika kushinda changamoto na kutimiza mambo yenye kustaajabisha. (Marko 11:22, 23) Ushauri wa Yesu kuhusu sala ulitolewa kwa wakati unaofaa kwa sababu imani ya wafuasi wake ingejaribiwa baada ya muda mfupi. Wangelazimika kukabiliana na kifo cha Yesu na pia upinzani dhidi ya huduma yao ungeongezeka. (Luka 24:17-20; Matendo 5:17, 18, 40) Leo, wafuasi wa Yesu wanaweza pia kushinda changamoto mbalimbali wanapoonyesha imani katika Mungu na katika nguvu za sala.​—Yakobo 2:26.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Marko.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?