Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waroma 12:2—“Bali Mgeuzwe kwa Kufanya Upya Akili Yenu”

Waroma 12:2—“Bali Mgeuzwe kwa Kufanya Upya Akili Yenu”

 “Acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:2, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Warumi 12:2, Union Version.

Maana ya Waroma 12:2

 Wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanapaswa kuepuka uvutano usiofaa na kubadili utu wao. Mungu hawalazimishi kubadilika; wanafanya hivyo kwa sababu wanampenda na wanatambua kwamba matakwa yake ni yenye fadhili, yenye usawaziko, na yana faida.—Isaya 48:17.

 “Acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.” “Mfumo huu wa mambo,” yaani, jamii ya wanadamu pamoja na viwango vyake, mazoea, na tabia hazipatani na njia ya Mungu ya kufikiri wala viwango vyake. (1 Yohana 2:15-17) Unawashinikiza watu kila wakati, na hilo linaweza kuwafinyanga wabadili tabia zao na utu wao. Ili kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika, ni lazima mtu apambane na uvutano wa ulimwengu huu, la sivyo, atasitawisha tabia ambazo zitamdhuru yeye mwenyewe na zinazomchukiza Mungu.—Waefeso 2:1-3; 4:17-19.

 “Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.” Ni lazima mtu ajitahidi kubadili mtazamo wake na mawazo yake ya ndani. Tunatambua kwamba hilo ni badiliko kubwa kwa sababu ya neno la Kigiriki lililotumiwa hapa linalotafsiriwa “mgeuzwe,” linarejelea badiliko kama la kiwavi anayebadilika na kuwa kipepeo. Ni lazima wale wanaomwabudu Mungu wavae “utu mpya.”—Waefeso 4:23, 24; Wakolosai 3:9, 10.

 “Mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Mungu anataka wale wanaomwabudu wawe na uhakika kabisa kuhusu kile wanachoamini. Wanafanya hivyo kwa kujifunza Neno la Mungu, kutumia mambo wanayojifunza, na kufaidika kwa kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Hivyo, wanajithibitishia kwamba njia za Mungu ndizo bora.—Zaburi 34:8.

Muktadha wa Waroma 12:2

 Waroma sura ya 12, inaeleza mambo yanayohusika katika kumwabudu Mungu katika njia inayofaa. Ibada hiyo inagusa kila eneo katika maisha ya mtu na inataka kwamba mtu huyo atumie ‘nguvu zake za kufikiri’ badala ya kutenda kulingana na imani iliyopotoka au jinsi anavyohisi. (Waroma 12:1, 3) Sura hiyo inatoa shauri linalofaa la jinsi ya kuonyesha sifa kama za Mungu, jinsi ya kushughulika na wengine, na jinsi ya kuitikia tunapotendewa isivyofaa.—Waroma 12:9-21.