Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yohana 15:13—“Hakuna Upendo Mkuu Zaidi”

Yohana 15:13—“Hakuna Upendo Mkuu Zaidi”

 “Hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.”—Yohana 15:13, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu ataoye uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.—Yohane 15:13, Biblia Habari Njema.

Maana ya Yohana 15:13

 Yesu alitaka kuwasaidia wafuasi wake waelewe kwamba upendo wao unapaswa kuwa na nguvu hivi kwamba watakuwa tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.

 Katika mstari wa 12, Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda.” (Yohana 15:12) Yesu aliwaonyesha upendo wa aina gani? Upendo usio na ubinafsi, upendo wa kujidhabihu. Wakati wa huduma yake hapa duniani, alitanguliza mahitaji na mapendezi ya wafuasi wake na si yake mwenyewe. Aliwaponya watu magonjwa yao na akawafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. a Hata alifanya kazi zilizoonekana kuwa za hali ya chini, ili kuwanufaisha wengine. (Mathayo 9:35; Luka 22:27; Yohana 13:3-5) Lakini kwenye Yohana 15:13, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu tendo kubwa zaidi la upendo. Kwa kweli, saa chache tu baada ya kusema maneno hayo, alionyesha upendo huo mkubwa zaidi alipotoa kwa hiari “uhai wake uwe fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28; 22:39) Kwa hiyo alionyesha kwa njia ya pekee kwamba aliwapenda wengine kuliko jinsi alivyojipenda mwenyewe.

 Yesu anawapenda wanadamu. Lakini anawapenda hata zaidi wale wanaofuata mafundisho yake. Aliwaona wanafunzi wake kuwa rafiki zake wa karibu kwa sababu walitii maagizo yake na walishikamana naye katika majaribu yake. (Luka 22:28; Yohana 15:14, 15) Kwa sababu hiyo, alichochewa hata zaidi kudhabihu uhai wake kwa ajili yao.

 Wakristo wa karne ya kwanza waliishi kupatana na maneno ya Yesu na walikuwa tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake. (1 Yohana 3:16) Kwa hiyo, upendo usio na ubinafsi—upendo ambao Yesu alionyesha—ungekuwa ishara kuu ambayo ingewatambulisha Wakristo wa kweli.—Yohana 13:34, 35.

Muktadha wa Yohana 15:13

 Sura ya 13 hadi 17 ya Injili ya Yohana ni rekodi ya ushauri ambao Yesu aliwapa mitume wake 11 waaminifu kabla ya kifo chake na sala yake ya mwisho pamoja nao. Alikufa saa chache baadaye. Katika sura ya 15, Yesu anawalinganisha wafuasi wake na matunda ya mzabibu ili kuonyesha kwamba wanahitaji kukaa katika muungano pamoja naye na kujithibitisha kuwa wafuasi wake. Yesu aliwahimiza ‘waendelee kuzaa matunda mengi.’ (Yohana 15:1-5, 8) Njia moja ya kuzaa matunda ni kuwaonyesha wengine upendo wa kujidhabihu, kutia ndani kuwapa ujumbe ambao Yesu alihubiri, yaani, “habari njema ya Ufalme wa Mungu.”—Luka 4:43; Yohana 15:10, 17.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Yohana.

a Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo mbinguni. Mungu alianzisha Ufalme huo ili utawale dunia na kutimiza mapenzi yake kwa ajili ya dunia. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Ili kupata habari zaidi, soma makala yenye kichwa, “Ufalme wa Mungu Ni Nini?