Kulingana na Mathayo 10:1-42

  • Mitume 12 (1-4)

  • Maagizo kwa ajili ya huduma (5-15)

  • Wanafunzi watateswa (16-25)

  • Mwogope Mungu, si wanadamu (26-31)

  • Sikuleta amani, bali upanga (32-39)

  • Kuwakaribisha wanafunzi wa Yesu (40-42)

10  Basi akawaita wanafunzi wake 12 na kuwapa mamlaka ya kuwafukuza roho waovu+ na kuponya kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.  Haya ndiyo majina ya wale mitume 12:+ Simoni, aitwaye Petro,+ na Andrea+ ndugu yake; Yakobo na Yohana+ wana wa Zebedayo;  Filipo na Bartholomayo;+ Tomasi+ na Mathayo+ mkusanya kodi; Yakobo mwana wa Alfayo; Thadayo;  Simoni Mkananayo;* na Yuda Iskariote, ambaye baadaye alimsaliti.+  Yesu akawatuma hao 12 na kuwaagiza:+ “Msiende katika barabara ya mataifa, wala msiingie katika jiji lolote la Wasamaria;+  badala yake, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.+  Mnapoenda, hubirini mkisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’+  Ponyeni wagonjwa,+ fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, fukuzeni roho waovu. Mlipokea bure, toeni bure.  Msichukue dhahabu, fedha, wala shaba kwenye mishipi yenu ya pesa,+ 10  wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili,* wala viatu, wala fimbo,+ kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake.+ 11  “Mtakapoingia katika jiji au kijiji chochote, tafuteni humo mtu anayestahili, na mkae humo mpaka mtakapoondoka.+ 12  Mnapoingia katika nyumba, wasalimuni watu wa nyumba hiyo. 13  Ikiwa nyumba hiyo inastahili, amani mnayoitakia na iwe juu yake;+ lakini kama haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi. 14  Popote pale ambapo mtu hawakaribishi au kusikiliza maneno yenu, mnapotoka katika nyumba hiyo au jiji hilo, kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu.+ 15  Kwa kweli ninawaambia, katika Siku ya Hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa Sodoma na Gomora+ kuliko kwa jiji hilo. 16  “Tazama! Ninawatuma kama kondoo katikati ya mbwamwitu; kwa hiyo iweni waangalifu* kama nyoka na wasio na hatia kama njiwa.+ 17  Jihadharini na watu, kwa maana watawapeleka mahakamani+ na kuwapiga mijeledi+ katika masinagogi+ yao. 18  Nanyi mtapelekwa mbele ya magavana na wafalme+ kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.+ 19  Hata hivyo, mtakapopelekwa, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo;+ 20  kwa maana si ninyi tu mnaosema, bali ni roho ya Baba yenu inayosema kupitia ninyi.+ 21  Zaidi ya hayo, mtu atamtoa ndugu yake auawe, na baba atamtoa mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe.+ 22  Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu,+ lakini yule atakayevumilia* mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.+ 23  Mnapoteswa katika jiji moja, kimbilieni jiji lingine;+ kwa kweli ninawaambia, hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika. 24  “Mwanafunzi hamzidi mwalimu wake, wala mtumwa hamzidi bwana wake.+ 25  Inatosha mwanafunzi kuwa kama mwalimu wake, na mtumwa kuwa kama bwana wake.+ Ikiwa watu wamemwita bwana wa nyumba Beelzebuli,*+ namna gani watu wa nyumbani mwake? 26  Basi msiwaogope, kwa maana hakuna jambo lolote lililofunikwa ambalo halitafunuliwa, na hakuna siri yoyote ambayo haitafichuliwa.+ 27  Jambo ninalowaambia gizani, lisemeni nuruni, na jambo mnalosikia likinong’onwa, lihubirini juu ya paa za nyumba.+ 28  Na msiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi;*+ badala yake, mwogopeni yule anayeweza kuangamiza nafsi na mwili katika Gehena.*+ 29  Shore wawili huuzwa kwa sarafu ya thamani ndogo,* sivyo? Lakini hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua.+ 30  Lakini hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa. 31  Kwa hiyo msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.+ 32  “Basi kila mtu anayenikiri mbele ya watu,+ mimi pia nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni.+ 33  Lakini yeyote anayenikana mbele ya watu, mimi pia nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.+ 34  Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani, sikuja kuleta amani, bali upanga.+ 35  Kwa maana nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu dhidi ya baba yake, binti dhidi ya mama yake, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe wake.+ 36  Kwa kweli, adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake. 37  Yeyote anayempenda baba au mama kuliko anavyonipenda hanistahili; na yeyote anayempenda mwana au binti kuliko anavyonipenda hanistahili.+ 38  Na yeyote asiyechukua mti wake wa mateso* na kunifuata hanistahili.+ 39  Yeyote anayeipata nafsi yake* ataipoteza, na yeyote anayeipoteza nafsi yake* kwa ajili yangu ataipata.+ 40  “Yeyote anayewapokea ninyi ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea mimi anampokea pia Yule aliyenituma.+ 41  Yeyote anayempokea nabii kwa sababu ni nabii atapata thawabu ya nabii,+ na yeyote anayempokea mtu mwadilifu kwa sababu ni mwadilifu atapata thawabu ya mtu mwadilifu. 42  Na yeyote anayempa mmoja wa hawa wadogo kikombe tu cha maji baridi ya kunywa kwa sababu ni mwanafunzi wangu, kwa kweli ninawaambia, hatapoteza kamwe thawabu yake.”+

Maelezo ya Chini

Au “mwenye bidii.”
Au “vazi la ziada.”
Au “iweni wenye kujihadhari.”
Au “anayevumilia.”
Jina lingine la Shetani, mkuu, au mtawala, wa roho waovu.
Au “uhai,” yaani, tumaini la kuishi.
Angalia Kamusi.
Tnn., “kwa sarafu moja ya asarioni. ” Angalia Nyongeza B14.
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “uhai wake.”
Au “uhai wake.”