Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Yetu Itaokoka?

Je, Dunia Yetu Itaokoka?

Je, Dunia Yetu Itaokoka?

Gazeti Globe and Mail la Kanada linaripoti hivi: “Ingawa kwa miaka mingi wanadamu wameogopa ‘matendo ya Mungu’ kama vile mafuriko na ukame, sasa wanakabili jambo baya hata zaidi: ‘matendo ya wanadamu’ kuelekea dunia.” Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) lilitoa ripoti ndefu iliyowasihi watu watende kabla haijawa kuchelewa mno. Mkurugenzi mkuu wa shirika la UNEP, Klaus Toepfer, anasema hivi: “Tunajua mambo ya kutosha kutusaidia kutambua kile ambacho kitayapata mazingira na wakazi wa sayari hii ya buluu kufikia mwaka wa 2032 kwa kufanya mambo fulani au kutofanya mambo fulani.”

Maendeleo fulani yamepatikana tangu shirika la UNEP lianzishwe katika mwaka wa 1972. Kama ilivyoripotiwa katika gazeti The Toronto Star, “hewa na maji ya mito yameboreka huko Ulaya na Amerika Kaskazini, na tabaka la ozoni limeanza kurekebishwa kwa sababu ya kupunguka kwa uchafuzi wa kemikali.” Pia miradi ya kutunza misitu ya nchi kama vile Kanada, Finland, Norway, na Marekani, “itapunguza athari za ukataji wa miti kupita kiasi.” Hata hivyo, ripoti ya shirika la UNEP inasema kwamba iwapo uchumi utazidi kukua bila kuzuiwa na majiji yazidi kupanuka, hilo litaathiri vibaya viumbe na mimea. Gazeti Globe lilisema hivi: “Karibu nusu ya mito duniani imechafuliwa au maji yake kupunguka sana. Nchi 80 zilizo na asilimia 40 ya watu wa dunia zinakumbwa na upungufu mkubwa wa maji.”

Toepfer anaamini kwamba “hatua madhubuti sharti zichukuliwe ili kuboresha hali hiyo.” Anaongeza hivi: “Tunahitaji mikakati thabiti . . . miradi thabiti . . . na muhimu zaidi azimio la waziwazi.” Lakini kuna tumaini gani iwapo viongozi wa ulimwengu hawataki kuchukua hatua zitakazolinda masilahi ya dunia?

Uwe na hakika kwamba kuna mtu ambaye ametoa “azimio la waziwazi” ambaye atachukua “hatua madhubuti,” yaani Yehova Mungu. Kwa hakika ameazimia bila kugeuka kwamba ataingilia mambo na “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:18) Isitoshe, Mungu anatuhakikishia kwamba mifumo ya dunia itarejeshwa. Majangwa yatachanua maua. (Isaya 35:1) Chakula kitakuwa tele. Mito haitachafuliwa tena. (Zaburi 72:16; 98:8) Mungu anasema kwamba atabariki kila kitu kilicho hai duniani.—Zaburi 96:11, 12.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

NASA photo