Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatimaye Amani Duniani!

Hatimaye Amani Duniani!

Hatimaye Amani Duniani!

WATU fulani wanaamini kwamba wanaweza kupata uhuru wa kisiasa na kuwa safi kiroho kupitia tu jeuri. Wanaamini kwamba viongozi wasiotakikana wanaweza kuondolewa tu kupitia jeuri. Pia serikali fulani hutumia vitisho ili kudumisha utengamano na kudhibiti raia zake. Lakini ikiwa ni kweli kwamba kutumia vitisho ndiyo njia bora ya kutawala na kuleta mabadiliko ya kijamii, basi mambo hayo yanapaswa kuleta amani, ufanisi, na utulivu. Baada ya muda, jeuri na hofu zinapaswa kupungua. Je, imekuwa hivyo?

Ukweli ni kwamba ugaidi hufanya watu wasiheshimu uhai na husababisha umwagaji wa damu na ukatili. Kwa sababu ya uchungu wanaohisi, mara nyingi wahasiriwa wa ugaidi hulipiza kisasi, jambo ambalo hufanya wakandamizwe zaidi, na hilo hufanya walipize kisasi tena.

Jeuri Haisuluhishi Matatizo Yetu

Kwa maelfu ya miaka, wanadamu wamekuwa wakijaribu kujisuluhishia matatizo yao ya kisiasa, kidini, na kijamii. Lakini hawajafua dafu. Ni kama vile isemavyo Biblia: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Yesu alisema: “Hekima husimama na kuanguka kwa matokeo [yake].” (Mathayo 11:19, The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Kanuni hizo za Biblia zinaweza kutumiwa kuonyesha kwamba ugaidi ni tumaini bandia. Badala ya kutokeza uhuru na furaha, ugaidi umetokeza kifo, taabu, na uharibifu. Matunda hayo yasiyofaa yalienea katika karne ya 20 na yanaanza kuenea pia katika karne ya 21. Watu wanasema kwamba badala ya kutatua matatizo, ugaidi ni mojawapo ya matatizo hayo.

“Kila siku mimi huomba kwamba mtu yeyote katika familia yetu au rafiki yangu asife . . . Labda tunahitaji muujiza.” Akasema msichana mmoja mchanga ambaye nchi yao ilikuwa imekumbwa na ugaidi. Maneno yake yanaunga mkono mkataa ambao watu wengi wamefikia: Wanadamu hawawezi kutatua matatizo yao. Ni Muumba wa mwanadamu peke yake anayeweza kutatua matatizo yanayoukumba ulimwengu sasa kutia ndani ugaidi. Lakini kwa nini tumtumaini Mungu?

Kwa Nini Tumtumaini Mungu?

Sababu moja ni kwamba akiwa Muumba, Yehova alitupa uhai naye anataka tuufurahie tukiwa na amani na uradhi. Nabii wa Mungu Isaya alichochewa kuandika: “Sasa, Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mfinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mkono wako.” (Isaya 64:8) Yehova ndiye Baba ya wanadamu wote, na watu wa mataifa yote ni wenye thamani kwake. Hapaswi kulaumiwa kwa ukosefu wa haki na chuki inayotokeza ugaidi. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi pindi moja: “Mungu wa kweli aliwafanya wanadamu wakiwa wanyoofu, lakini wao wenyewe wametafuta mipango mingi.” (Mhubiri 7:29) Ugaidi hautokezwi kwa sababu Mungu hana uwezo wa kuuzuia bali unatokezwa na uovu wa wanadamu na uvutano wa roho waovu.—Waefeso 6:11, 12.

Sababu nyingine ya kumtumaini Yehova ni kwamba kwa kuwa yeye amewaumba wanadamu, anaelewa vizuri kuliko mtu mwingine yeyote kile kinachosababisha matatizo ya wanadamu na jinsi yanavyopaswa kutatuliwa. Biblia inataja ukweli huo kwenye Methali 3:19: “Kwa hekima Yehova mwenyewe aliuweka msingi wa dunia. Aliziweka mbingu imara kwa utambuzi.” Akiwa na tumaini kamili katika Mungu, mwanamume fulani wa zamani za kale aliandika hivi: “Msaada wangu utatoka wapi? Msaada wangu unatoka kwa Yehova, Mtengenezaji wa mbingu na dunia.”—Zaburi 121:1, 2.

Kuna sababu ya tatu ya kumtumaini Mungu: Ana nguvu za kuzuia umwagaji wa damu. Katika wakati wa Noa ‘dunia ilijaa jeuri.’ (Mwanzo 6:11) Hukumu ya Mungu ilikuja kwa ghafula na ilikuwa kamili: “[Mungu] hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale . . . alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 2:5.

Biblia inataja jambo ambalo tunapaswa kujifunza kutokana na Gharika ya siku za Noa: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.” (2 Petro 2:9) Mungu anaweza kutofautisha kati ya watu wanaopenda kuishi maisha bora na wale wanaofanya maisha ya wengine yawe machungu. Amewaweka akiba wale wanaofanya maisha ya wengine yawe machungu kwa ajili ya “kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” Lakini kwa wote wanaopenda amani, anatayarisha dunia mpya ambamo uadilifu utakaa.—2 Petro 3:7, 13.

Amani ya Kudumu Duniani!

Mara nyingi waandikaji wa Biblia walitumia neno “dunia” kumaanisha wanadamu. Kwa mfano, andiko la Mwanzo 11:1 linasema kwamba “dunia yote,” yaani, wanadamu wote waliokuwa hai wakati huo, walizungumza lugha moja. Mtume Petro alimaanisha hilo alipoandika kuhusu “dunia mpya.” Yehova Mungu atafanya upya jamii ya kibinadamu katika njia ya kwamba jeuri na chuki itaondolewa kabisa na badala yake uadilifu na haki “zitakaa” duniani. Biblia inatuambia hivi katika unabii wa Mika 4:3: “Naye hakika atafanya hukumu kati ya vikundi vingi vya watu, na kunyoosha mambo kuhusu mataifa yenye nguvu yaliyo mbali. Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”

Watu wataishije unabii huo utakapotimizwa? Andiko la Mika 4:4 linasema: “Nao wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” Katika dunia hiyo itakayokuwa Paradiso hakuna mtu atakayeishi kwa woga wa kushambuliwa na magaidi. Je, unaweza kuamini ahadi hiyo? Ndiyo, “kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.”—Mika 4:4.

Kwa hiyo, huku vitisho vya ugaidi vikiendelea kuongezeka na mataifa kuishi kwa woga kwa sababu ya jeuri, suluhisho kwa watu wanaopenda amani ni kumtumaini Yehova. Hakuna tatizo asiloweza kutatua. Ataondoa majeraha, kuteseka, na hata kifo. Biblia inasema: “Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Nchi nyingi nzuri ambazo sasa zimejaa taabu na woga kwa sababu ya ugaidi, hivi karibuni zitakuwa na amani tele. Amani hiyo, iliyoahidiwa na Mungu “asiyeweza kusema uwongo,” ndiyo wanadamu wanahitaji haraka.—Tito 1:2; Waebrania 6:17, 18.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

BADALA YA KUTUMIA RISASI NA MABOMU . . .

Yafuatayo ni maelezo ya watu waliokuwa wakiamini kwamba matendo ya jeuri yanaweza kutokeza mabadiliko ya kisiasa.

▪ “Niliposoma vitabu vya historia, niligundua kwamba sikuzote wafalme na wakuu wa serikali wamewakandamiza maskini. Ningeweza kuhisi jinsi watu wa hali ya chini walivyoteseka. Nilipofikiria jinsi mambo hayo mabaya yanavyoweza kukomeshwa, nilikata kauli kwamba tutahitaji kupigana, kutumia silaha ili kulipiza kisasi.”—Ramon. *

▪ “Nilipigana kwa kutumia silaha. Kusudi langu lilikuwa kukaidi mamlaka zilizokuwapo na kuanzisha jamii ambayo itaondoa ukosefu wa usawa uliopo ulimwenguni.”—Lucian.

▪ “Tangu nilipokuwa mtoto, nilikerwa na ukosefu wa haki. Hilo lilitia ndani umaskini, uhalifu, elimu duni, na ukosefu wa huduma za afya. Niliamini kwamba kwa kutumia silaha, watu wote wangeweza kupata elimu, huduma za afya, nyumba na kazi. Pia niliamini kwamba mtu yeyote asiye na adabu na asiyemheshimu jirani yake anapaswa kuadhibiwa.”—Peter.

▪ “Mimi na mume wangu tulikuwa wanachama wa shirika fulani la siri lililochochea uasi wenye jeuri. Tulitumaini kwamba tungeanzisha serikali ambayo ingeleta hali nzuri, utengamano na usawa kwa wote. Tulihisi kwamba kupinga serikali ndiyo njia pekee ya kupata haki katika nchi yetu.”—Lourdes.

Watu hao walijaribu kusaidia wanadamu wanaoteseka kwa kutumia nguvu. Lakini walipojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, walitambua kwamba Neno la Mungu lina suluhisho bora. Biblia inasema hivi kwenye Yakobo 1:20: “Kwa maana ghadhabu ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” Biblia Habari Njema inasema: “Mwenye hasira hawezi kutimiza matakwa ya Mungu yaliyo ya haki.”

Ni utawala wa Mungu tu unaoweza kubadili jamii ya kibinadamu. Unabii wa Biblia kama ule unaopatikana katika Mathayo sura 24 na 2 Timotheo 3:1-5 unaonyesha kwamba serikali ya Mungu iko karibu kutekeleza jambo hilo. Tunakutia moyo uchunguze kweli hizo kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Majina yamebadilishwa.