Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Kutumia Sanamu Katika Ibada?

Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Kutumia Sanamu Katika Ibada?

Maoni ya Biblia

Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Kutumia Sanamu Katika Ibada?

Sanamu za kuwasaidia watu kusali hutumiwa sana na Wabudha, Wahindu, Waislamu, Wayahudi, Wakatoliki, na Wafuasi wa Kanisa Othodoksi la Mashariki. Hivyo, mamilioni ya watu katika karibu nchi zote wanaamini kwamba vitu hivyo huwasaidia kumkaribia Mungu, kupata kibali, au baraka zake. Biblia inafundisha nini?

ZOEA la kutumia sanamu kuwasaidia watu kusali lilianza maelfu ya miaka iliyopita. Kwa mfano, katika sehemu fulani ya Ninawi ya kale, wachimbuzi wa vitu vya kale walifukua “sanamu mbili za kike zilizokuwa na mabawa zikiwa zimesimama mbele ya mti mtakatifu zikisali; zilikuwa . . . zimeshika shada la maua au rozari kwenye [mkono] wa kushoto.”—The Catholic Encyclopedia.

Rozari hutimiza kusudi gani? Ensaiklopidia hiyo inajibu hivi: “Wakati wowote sala inahitaji kurudiwa mara nyingi, lazima mtu atafute msaada kupitia kifaa fulani ambacho hakichoshi kama kuhesabu vidole.”

Magurudumu ya sala hurahisisha sala za kurudia. Kila mara gurudumu linapozungushwa kwa mkono, upepo, maji, au umeme, hilo huonwa na yule anayelizungusha kuwa sawa na kutoa sala moja. Mara nyingine magurudumu ya sala hutumiwa pamoja na maneno ya kidini yanayorudiwa-rudiwa. Chunguza jinsi Mungu anavyohisi kuhusu vitu kama hivyo.

“Msiseme Mambo Yaleyale Tena na Tena”

Yesu Kristo ambaye anatambuliwa na mamilioni ya watu wasio Wakristo kuwa nabii wa Mungu, alieleza maoni ya Muumba kuhusu kurudia sala, akisema: “Lakini mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.” *Mathayo 6:7.

Hivyo basi, ikiwa Mungu anatukataza tusiseme “mambo yaleyale tena na tena,” je, vifaa vinavyotumiwa kusaidia mtu kurudia sala tena na tena havingekuwa jambo lisilofaa machoni pake? Kwa kupatana na hilo, hakuna mahali popote ambapo Biblia inataja kwamba mtumishi mwaminifu wa Mungu wa kweli alitumia rozari, magurudumu ya sala, au kitu kingine kama hicho katika ibada. Tunaweza kuelewa ni kwa nini Mungu alikataza matumizi ya vitu hivyo katika ibada tukijua sala ni nini na ina kusudi gani.

Sala Zinazompendeza Mungu

Katika sala ya mfano, Yesu alimtaja Mungu kwa usahihi kuwa “Baba yetu.” Ni kweli kwamba Muumba wetu si kitu kisichoeleweka kinachopaswa kutulizwa kupitia nyimbo za uchawi, desturi, au maneno ya kidini yanayorudiwa-rudiwa. Badala ya hivyo, yeye ni Baba mwenye upendo na anataka tumtambue kwa njia hiyo na tumpende. Yesu alisema: “Ninampenda Baba.” (Yohana 14:31) Nabii mmoja katika Israeli la kale alisema hivi: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu.”—Isaya 64:8.

Tunawezaje kumkaribia Yehova akiwa Baba yetu wa kiroho? (Yakobo 4:8) Kama ilivyo katika mahusiano mengine, tunamkaribia Mungu kwa kuzungumza naye na kumsikiliza. Mungu “huzungumza” nasi kupitia Biblia, Neno lake lililoandikwa, ambamo yeye hutufunulia utendaji na utu wake, na pia kusudi lake kwa wanadamu. (2 Timotheo 3:16) Nasi huzungumza na Mungu kupitia sala. Bila shaka, sala kama hiyo inapaswa kutolewa kwa unyoofu na kutoka moyoni, si kwa njia ya kidesturi tu.

Fikiria hili: Katika familia yenye upendo, watoto wenye akili timamu huzungumzaje na wazazi wao? Je, wanasema maneno yaleyale tena na tena, labda wakihesabu mara ambazo wamerudia maneno hayo kwa kutumia kifaa fulani? La hasha! Badala yake, wanazungumza maneno yanayoeleweka, kwa heshima, na kutoka moyoni.

Sala kwa Mungu zinapaswa kuwa hivyo. Ni kweli kwamba tunaweza kuzungumza na Mungu kuhusu jambo lolote linalotuhangaisha. Wafilipi 4:6, 7 inasema: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu . . . itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” Kwa kawaida, tunapohangaishwa na jambo fulani, huenda tukasali kulihusu mara nyingi. Lakini kufanya hivyo si sawa na kurudia maneno yaleyale tena na tena.—Mathayo 7:7-11.

Biblia ina mifano mingi ya sala zinazompendeza Mungu, kutia ndani zaburi, nyimbo, na sala zilizotolewa na Yesu mwenyewe. * (Maneno ya utangulizi ya Zaburi 17 na 86; Luka 10:21, 22; 22:40-44) Mojawapo ya sala hizo inapatikana kwenye Yohana sura ya 17. Tenga dakika chache kusoma sala hiyo. Unapofanya hivyo, ona jinsi Yesu alivyomwagia Mungu mambo yaliyokuwa moyoni mwake. Ona pia kwamba sala yake haikuwa na ubinafsi, jinsi ilivyoonyesha upendo wake mwingi kwa wafuasi wake. “Baba Mtakatifu,” akasema, “uwalinde kwa sababu ya yule mwovu,” Shetani.—Yohana 17:11, 15.

Je, kuna jambo lolote linaloonyesha kuwa maneno ya Yesu hayakuwa na hisia au yalikuwa ya kidesturi tu? Hakuna! Ni mfano mzuri kama nini aliotuwekea! Naam wale wanaotaka kumkaribia Mungu wanapaswa kuujua utu wake vizuri. Kisha, kwa kuchochewa na upendo unaotegemea ujuzi huo, ni lazima wakatae desturi za kidini na mazoea yasiyompendeza Mungu. Yehova anawaambia hivi watu kama hao: “Nitakuwa baba kwenu, nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu.”—2 Wakorintho 6:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Katika sala yake ya mfano, Yesu hakusema: “Ni lazima basi msali sala hii,” jambo ambalo lingepingana na yale aliyokuwa ametoka tu kusema. Badala yake alisema: “Basi, ninyi msali hivi.” (Mathayo 6:9-13) Alikuwa akitaka kufundisha somo gani? Kama vile sala ya mfano inavyofunua, tunapaswa kutanguliza mambo ya kiroho badala ya mambo ya kimwili.

^ fu. 15 Ingawa zaburi ziliimbwa katika pindi fulani, hazikusemwa kwa kurudia-rudia kama maneno ya kidini yanayorudiwa tena na tena, wala hazikutumiwa katika desturi zilizohusisha rozari au magurudumu ya sala.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, shauri la Yesu kuhusu sala za kurudiwa-rudiwa linahusu matumizi ya rozari na magurudumu ya sala?—Mathayo 6:7.

▪ Sala zetu zinapaswa kufunua nini kuhusu maoni yetu kumhusu Mungu?—Isaya 64:8.

▪ Tukikataa uwongo wa kidini, Mungu atatuonaje?—2 Wakorintho 6:17, 18.