Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?

Mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini si ya siri, kwa kuwa vitabu vyao vinapatikana kwa wingi na katika mamia ya lugha. Ufuatao ni muhtasari wa baadhi ya imani zao kuu.

1. Biblia Mashahidi wanaamini kuwa “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Jason D. BeDuhn, ambaye ni profesa msaidizi wa masomo ya kidini, aliandika hivi: “[Mashahidi wa Yehova hujenga] imani yao na kutenda kulingana na yale wanayosoma moja kwa moja kutoka katika Biblia badala ya kuamua mapema kulingana na maoni yao mambo ambayo Biblia itasema.” Imani yao hutegemea Biblia; lakini hawaibadili ili ifaane na mapendezi yao. Pia wanatambua kuwa si kila kitu kilicho ndani ya Biblia kinachopaswa kueleweka kihalisi. Kwa mfano, siku saba za uumbaji ni za mfano na zinarejelea kipindi kirefu cha wakati.—Mwanzo 1:31; 2:4.

2. Muumba Mungu wa kweli amejipa jina la kibinafsi—Yehova (au Yahweh, kama linavyopatikana katika Biblia Jerusalem Bible ya Wakatoliki na baadhi ya wasomi wa kisasa wanavyotaka kuita jina hilo)—ili ajitofautishe na miungu ya uwongo. * (Zaburi 83:18) Jina hilo la Mungu katika Kiebrania linapatikana mara 7,000 katika maandishi ya awali ya Maandiko. Akikazia umuhimu wa jina hilo, Yesu alisema hivi katika sala ya kielelezo: “Jina lako litukuzwe.” (Mathayo 6:9, Union version) Mungu anataka watu wajitoe kwake kikamili. Hivyo, Mashahidi hawatumii sanamu katika ibada yao.—1 Yohana 5:21.

3. Yesu Kristo Yeye ni mwokozi, “Mwana wa Mungu,” na “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Yohana 1:34; Wakolosai 1:15; Matendo 5:31) Kwa kuwa aliumbwa, yeye si sehemu ya Utatu. Yesu alisema hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Yesu aliishi mbinguni kabla ya kuja duniani na akarudi mbinguni baada ya kifo chake cha kidhabihu na kufufuliwa. “Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia [kwake].”—Yohana 14:6.

4. Ufalme wa Mungu Hii ni serikali halisi ya kimbingu iliyo na Mfalme—Yesu Kristo—na watawala wenzi 144,000, ambao “wamenunuliwa kutoka duniani.” (Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3, 4; Danieli 2:44; 7:13, 14) Watatawala juu ya dunia ambayo haitakuwa na uovu wowote na itakayokaliwa na mamilioni ya watu wanamwogopa Mungu. —Methali 2:21, 22.

5. Dunia Mhubiri 1:4 inasema hivi: “Dunia hudumu daima.” (Union Version) Baada ya waovu kuharibiwa, dunia itafanywa kuwa paradiso na kujazwa na watu waadilifu watakaoishi milele. (Zaburi 37:10, 11, 29) Hivyo, maneno haya ambayo Yesu alisema katika sala ya kielelezo yatatimizwa, “mapenzi yako yatimizwe hapa duniani.”—Mathayo 6:10, Union Version.

6. Unabii wa Biblia ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Kwa hiyo, kile anachotabiri hutukia, kutia ndani unabii wa Biblia kuhusu mwisho wa ulimwengu huu. (Isaya 55:11; Mathayo 24:3-14) Nani watakaookoka uharibifu huo? Andiko la 1 Yohana 2:17 linasema hivi: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”

7. Mamlaka za serikali Yesu alisema hivi: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hutii sheria za nchi wakati hazipingani na sheria za Mungu.—Matendo 5:29; Waroma 13:1-3.

8. Kuhubiri Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme” itahubiriwa ulimwenguni pote kabla ya mwisho wa ulimwengu huu. (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanathamini sana pendeleo la kushiriki katika kazi hii ya kuokoa uhai. Bila shaka, watu wana uhuru wa kusikiliza au kukataa ujumbe huo. Biblia inasema hivi: “Yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.

9. Ubatizo Mashahidi wa Yehova huwabatiza wale tu ambao wamejifunza Biblia kwa undani na wako tayari kumtumikia Mungu wakiwa Mashahidi wake. (Waebrania 12:1) Wao huonyesha kuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu kwa kuzamishwa ndani ya maji.—Mathayo 3:13, 16; 28:19.

10. Tofauti kati ya waumini na makasisi “Ninyi nyote ni ndugu,” Yesu akawaambia wafuasi wake. (Mathayo 23:8) Katika siku za Wakristo wa karne ya kwanza, kutia ndani waandikaji wa Biblia, hakukuwa na kikundi cha makasisi. Mpangilio huo wa Biblia ndio unaofuatwa na Mashahidi wa Yehova leo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mashahidi wa Yehova hawakujitungia jina “Yehova.” Karne nyingi zilizopita, lugha kadhaa ambazo hazikutumiwa kuandika Biblia kutia ndani Kiingereza na Kijerumani, zilitumia jina la Mungu “Yehova.” Jambo la kusikitisha ni kwamba watafsiri wa kisasa wameliondoa jina la Mungu na badala yake kutumia majina ya cheo kama vile, “Mungu” na “Bwana,” hivyo wakimkosea heshima Mtungaji wa Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Baba ni mkuu kuliko mimi.”—Yohana 14:28

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14