Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

Mbona Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

Vijana Huuliza

Mbona Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

Allison, * kijana nchini Australia, huona kila Jumatatu (Siku ya 1) asubuhi shuleni kuwa wakati wenye kuchosha sana.

“Kila mtu huzungumzia mambo aliyofanya mwisho-juma,” anasema. “Wao hueleza mambo yenye kusisimua kama vile karamu walizohudhuria na waliwabusu wavulana wangapi—hata jinsi walivyokimbia polisi wasiwashike . . . Mambo hayo husikika kuwa yenye kuogopesha, lakini yenye kufurahisha sana! Wao hurudi nyumbani saa 11 asubuhi, na wazazi wao hawajali. Lakini mimi lazima niwe nimelala hata kabla wao hawajaanza kujifurahisha!

“Hata hivyo, baada ya kuniambia mambo waliyofanya mwisho-juma, wanafunzi wenzangu huanza kuniuliza nilifanya nini. Kwa kweli nilifanya nini? Nilienda kwenye mikutano ya Kikristo. Kisha nikashiriki katika utumishi. Ninahisi ni kana kwamba nilikosa mambo mengi yenye kufurahisha. Kwa hiyo, mimi huwaambia kwamba sikufanya lolote. Kisha wananiuliza kwa nini sikuambatana nao.

“Jumatatu inapokwisha unafikiri kwamba mambo yatatulia. Lakini wapi! Kufikia Jumanne (Siku ya 2) kila mtu anazungumza kuhusu mwisho-juma unaokuja! Mimi huketi tu na kuwasikiliza wakizungumza. Ninahisi ni kana kwamba nimetengwa!”

JE, WEWE hupatwa na hali kama hiyo kila Jumatatu asubuhi shuleni? Huenda ukahisi kwamba vijana wengine wanajifurahisha nje ya nyumba lakini wazazi wako wanakuzuia usitoke nje—au ni kana kwamba uko katika bustani yenye vifaa vingi vya kuchezea lakini huruhusiwi kuvitumia. Si eti unataka kufanya kila kitu ambacho vijana wenzako wanafanya. Ungependa tu kujifurahisha mara kwa mara! Kwa mfano, ni burudani gani ambayo wewe ungependa kujihusisha nayo mwisho-juma huu?

◯ kucheza dansi

◯ kwenda tamasha ya muziki

◯ kutazama sinema

◯ kwenda karamu

◯ jambo lingine ․․․․․

Unahitaji tafrija. (Mhubiri 3:1, 4) Kwa kweli, Muumba wako anataka ufurahie ujana wako. (Mhubiri 11:9) Na wazazi wako pia wanataka ujifurahishe, ingawa huenda usiamini hilo nyakati nyingine. Hata hivyo, huenda wazazi wako wakataka kujua mambo haya mawili: (1) utajihusisha na tafrija gani na (2) utaandamana na nani.

Lakini namna gani ikiwa rafiki zako wanakukaribisha kwenye tafrija lakini hujui wazazi wako watasema nini? Unapokabiliwa na uamuzi, Biblia inakutia moyo ufikirie faida na hasara ya uamuzi wako, na uchanganue matokeo. (Kumbukumbu la Torati 32:29; Methali 7:6-23) Ni uamuzi gani utakaofanya unapoalikwa kuandamana pamoja na rafiki zako?

UAMUZI A: USIOMBE RUHUSA—NENDA TU.

Sababu ya kufanya uamuzi huu: Unataka kuwaonyesha rafiki zako kwamba unajitegemea. Unahisi kwamba unajua mengi kuliko wazazi wako, au huoni kwamba wanajua kinachofaa.—Methali 15:5.

Matokeo: Rafiki zako watajua jambo fulani kukuhusu—kwamba unaweza kudanganya. Ikiwa unaweza kuwadanganya wazazi wako, basi pia unaweza kuwadanganya rafiki zako. Wazazi wako wakigundua, watahuzunika na kuhisi kwamba umewasaliti, na huenda ukanyimwa uhuru zaidi! Kukosa kuwatii wazazi wako na kuondoka tu ni uamuzi wa kipumbavu.—Methali 12:15.

UAMUZI B: USIOMBE RUHUSA—USIENDE.

Sababu ya kufanya uamuzi huu: Unafikiria kuhusu tafrija yenyewe na kuona kwamba haipatani na viwango vyako au kwamba baadhi ya wale waliokaribishwa si mashirika mazuri. (1 Wakorintho 15:33; Wafilipi 4:8) Kwa upande mwingine, ungependa kwenda lakini huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa.

Matokeo: Usipoenda kwa sababu unaona haifai kwenda, utakuwa na uhakika zaidi unapowajibu rafiki zako. Lakini usipoenda kwa sababu tu huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa, utashinda nyumbani ukiwa umenuna na ukihisi kwamba ni wewe tu ambaye hujifurahishi.

UAMUZI C: OMBA RUHUSA —KISHA SUBIRI JIBU.

Sababu ya kufanya uamuzi huu: Unatambua kwamba wazazi wako wana mamlaka juu yako na unaheshimu uamuzi wao. (Wakolosai 3:20) Unawapenda wazazi wako na hungependa kuwaumiza kwa kuwadanganya na kwenda tafrija bila kuwajulisha. (Methali 10:1) Pia una nafasi ya kueleza maoni yako.

Matokeo: Wazazi wako wanahisi kwamba unawapenda na kuwaheshimu. Na wanapoona kwamba ombi lako linafaa wanaweza kukubali.

Sababu Inayoweza Kuwafanya Wazazi Wakatae

Namna gani wazazi wako wakikataa? Hilo linaweza kuvunja moyo sana. Hata hivyo, kuelewa maoni yao kunaweza kukusaidia kukabiliana na vizuizi vyao. Kwa mfano, wanaweza kukataa kwa sababu ya mambo yafuatayo.

Wana ujuzi na uzoefu mwingi zaidi. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ungependa kuogelea mahali palipo na waokoaji-uhai. Kwa nini? Kwa sababu unapokuwa ndani ya maji ukiogelea, huwezi kutambua hatari vizuri. Lakini waokoaji-uhai wako katika hali nzuri zaidi ya kutambua hatari.

Vivyo hivyo, kwa kuwa wazazi wako wana ujuzi na uzoefu zaidi, wanaweza kutambua hatari ambazo wewe huoni. Kama tu waokoaji-uhai, kusudi la wazazi wako si kukuzuia ujifurahishe bali wanataka kukusaidia uepuke hatari zinazoweza kukuzuia ufurahie maisha.

Wanakupenda. Wazazi wako wanataka sana kukulinda. Kwa kuwa wanakupenda wao hukubaliana na wewe wanapoweza kufanya hivyo lakini wanakuzuia mambo fulani wanapolazimika kufanya hivyo. Unapowaomba ruhusa kufanya jambo fulani, wao hujiuliza ikiwa wanaweza kukupa ruhusa na bado wakabiliane na matokeo ya uamuzi wao. Watasema ndiyo iwapo tu watakuwa na uhakika kwamba hakuna jambo baya litakalokupata.

Wasipokuwa na habari ya kutosha. Wazazi wenye upendo hutenda kwa tahadhari. Ikiwa hawaelewi jambo unalowaomba, au wakihisi kwamba kuna mambo fulani ambayo huwaelezi, kuna uwezekano mkubwa kwamba watasema la.

Jinsi ya Kuwafanya Wazazi Wako Waseme Ndiyo

Mambo manne yanahusika.

Unyoofu: Kwanza kabisa, unahitaji kujiuliza hivi kwa unyoofu: ‘Ni sababu gani hasa inayonifanya nitake kwenda? Je, ni tafrija yenyewe, au ni kwamba tu ninataka kuhisi kwamba ninapendwa na rafiki zangu? Je, ni kwa sababu mtu fulani ninayevutiwa naye atakuwepo?’ Kisha waambie wazazi wako ukweli. Wakati fulani hata wao walikuwa vijana, na wanakufahamu vizuri. Kwa hiyo, kuna uwezekano mkubwa kwamba watatambua nia yako. Watathamini sana kwamba umewaambia ukweli, nawe utafaidika kutokana na hekima yao. (Methali 7:1, 2) Kwa upande mwingine, ikiwa hutawaambia ukweli, kuna uwezekano mkubwa kwamba utaacha kuaminika na huenda wasikuruhusu uende.

Wakati unaofaa: Usiwaulize wazazi wako maswali mengi baada tu ya wao kufika nyumbani kutoka kazini au wanapokazia fikira mambo mengine. Zungumza nao wanapokuwa wametulia. Lakini usisubiri hadi dakika ya mwisho kisha uanze kuwalazimisha wakupe jibu. Wazazi wako hawatafurahi wakilazimishwa kutoa jibu haraka. Omba ruhusa mapema, na wazazi wako watathamini jambo hilo.

Kuwaridhisha: Usizungumzie mambo kijuujuu tu. Eleza kihususa jambo unalotaka kufanya. Wazazi huwa na wasiwasi wanapoambiwa “Sijui,” hasa ikiwa wameuliza: “Ni nani atakayekuwepo?” “Je, kutakuwa na mtu mzima wa kusimamia mambo?” au “Tafrija hiyo itakwisha saa ngapi?”

Mtazamo: Usiwaone wazazi wako kuwa maadui. Waone kuwa wako upande wako—na kwa kweli wao wako upande wako. Ukiwa na mtazamo huo, hutazungumza kana kwamba unazozana, nao watakuwa tayari kushirikiana nawe. Wakikataa, waulize sababu yao kwa heshima. Kwa mfano, wakisema huendi kwenye tamasha fulani, jaribu kutambua kinachowafanya wawe na wasiwasi. Je, wana wasiwasi kumhusu mwimbaji? kuhusu mahali tamasha yenyewe itafanyiwa? watu watakaokuwepo? au pesa za kiingilio? Epuka kusema mambo kama “Mbona hamniamini,” “Kila mtu anaenda,” au “Wazazi wa rafiki zangu wamewaruhusu waende!” Waonyeshe wazazi wako kwamba umekomaa kiasi cha kutosha kukubali uamuzi wao na kuuheshimu. Ukifanya hivyo watakuheshimu. Na wakati ujao, huenda wakafikiria kukupa ruhusa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina limebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

“Wazazi wangu wananiamini hasa kwa sababu nina rekodi nzuri ya kutenda kwa hekima. Mimi huzungumza nao waziwazi kuhusu rafiki zangu. Pia siogopi kuondoka kwenye karamu iwapo sipendezwi na mambo yanayotendeka.”

[Picha]

Kimberly

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Je, ungependa kujua maoni ya wazazi wako kuhusu mambo yaliyozungumziwa katika habari hii? Njia pekee unayoweza kujua maoni yao ni kwa kuwauliza! Wakati unaofaa, zungumza nao kuhusu wasiwasi wanaopata unapotaka kujifurahisha. Fikiria swali ambalo ungependa kuwauliza, kisha uliandike hapa chini.

․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama tu waokoaji-uhai, wazazi wako wanaweza kutambua vizuri hatari na kukuonya