Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Wazazi

Maoni ya Wazazi

Maoni ya Wazazi

Unaweza kuwasaidia watoto wako jinsi gani waone thamani ya kuwa watiifu kadiri wanavyokua? Unaweza kutumia njia gani kuwafundisha stadi zenye thamani kadiri wanavyoendelea kuwa watu wazima? Ona mambo ambayo wazazi fulani kutoka sehemu zote ulimwenguni wamesema.

KAZI ZA NYUMBANI NA KUSHIRIKIANA NA WENGINE

“Tunapokula pamoja na kuzungumzia mambo yaliyotukia siku nzima, kila mtoto anajifunza kuwa msikivu. Wanapotuona tukisikiliza kwa makini, hilo linawasaidia kuheshimiana na kujiheshimu wenyewe.”—Richard, Uingereza.

“Inavutia kama nini kuwatazama watoto wetu wakitendeana kwa heshima na kuona wakijaribu kusuluhisha mizozo kati yao wenyewe bila ya kutuhusisha. Pia, wao huwasiliana kwa uhuru na watu wazima.”—John, Afrika Kusini.

“Mimi si mkamilifu, na wakati mwingine ninawaumiza hisia watoto wangu bila kukusudia. Ninapofanya hivyo, ni muhimu sana niwaombe msamaha kwa kosa nililofanya.”—Janelle, Australia.

“Tunawazoeza watoto wetu kufanya kazi za nyumbani. Kuwafundisha kufanya mambo yanayowafaidi wengine husaidia familia iishi vizuri na kwa amani na hufanya watoto wetu wahisi wametimiza jambo fulani muhimu.”—Clive, Australia.

“Si rahisi, lakini ni muhimu kuwafundisha kuwaelewa wengine, kuwaheshimu, na kusamehe.”—Yuko, Japani.

USAFI NA AFYA

“Watoto wetu walipokuwa wadogo, tuliwafundisha kuoga na tulifanya wafurahie jambo hilo kwa kutumia sabuni zilizokuwa na maumbo mbalimbali, sabuni ya maji iliyo kwenye chupa yenye picha za katuni fulani, na sifongo zenye maumbo ya wanyama wadogo.”—Edgar, Mexico.

“Tulipokuwa tukiishi mahali ambapo hakukuwa na maji ya bomba, nilihakikisha kwamba kuna sabuni na mtungi wa maji mahali ambapo kila mmoja wetu angeweza kuosha mikono kabla ya kuingia nyumbani.”—Endurance, Nigeria.

“Tunawapa watoto vyakula vyenye lishe nzuri kila siku, na kuwaeleza kwa nini mlo kama huo ni muhimu. Watoto hutaka sana kujua vyakula mbalimbali vinatayarishwa kwa njia gani, kwa hiyo mimi huwaomba wanisaidie kutayarisha mlo. Wakati tunaotumia pamoja kupika husaidia tupate nafasi zaidi za kuwasiliana.”—Sandra, Uingereza.

“Mazoezi ni muhimu sana, na tukiwa wazazi, tunajitahidi kuweka mfano mzuri. Watoto wetu hufurahi tunapokimbia, tunapoogelea, tunapocheza mpira pamoja au kuendesha baiskeli pamoja tukiwa familia. Mbali na kujifunza kwamba mazoezi ni muhimu, wameona pia yanafurahisha.”—Keren, Australia.

“Jambo ambalo watoto wanahitaji hasa ni kutumia wakati pamoja na wazazi wao. Hakuna jambo linaloweza kuchukua mahali pake—si pesa, zawadi, wala kutalii. Mimi hufanya kazi saa za asubuhi tu wakati ambapo watoto wako shuleni. Halafu alasiri mimi hutenga wakati wa kuwa pamoja nao.”—Romina, Italia.

NIDHAMU

“Tumegundua kwamba kuna njia nyingi zinazofaa za kutoa nidhamu; inategemea hali. Nyakati nyingine, nidhamu inaweza kutia ndani kuzungumzia mambo kwa uzito na mtoto, na wakati mwingine huenda ukahitaji kumzuia asifanye mambo fulani anayopenda.”—Ogbiti, Nigeria.

“Sisi huwaomba watoto wetu warudie maagizo tuliyowapa ili kuhakikisha wameyaelewa vizuri. Halafu tunahakikisha kwamba tumefanya kama tulivyosema. Ikiwa tunataka watoto wetu watii maagizo tunayowapa, ni lazima tuhakikishe kwamba tunatoa nidhamu tuliyosema tutawapa wanapokosa kutii.”—Clive, Australia.

“Mimi huinama ninapowarekebisha watoto wangu ili niwe sawa na kimo chao, na mbinu hiyo ina mafanikio. Kufanya hivyo kunawafanya wanisikilize kwa makini kabisa. Pia kunawasaidia waone ishara zangu za uso zinazokazia maneno ninayowaambia.”—Jennifer, Australia.

“Sisi huepuka kuwaambia watoto wetu, ‘Hakuna wakati wewe unatusikiliza,’ hata kama huo ndio ukweli wa mambo. Pia, hatukemei mtoto mbele ya wenzake. Tunawanong’onezea au tunawapeleka kando na kuongea nao wakiwa peke yao.”—Rudi, Msumbiji.

“Ni rahisi kuwaongoza watoto, na wanapenda kuwaiga wengine. Kwa sababu hiyo, ni lazima tuwalinde wasiathiriwe na watoto wenzao shuleni, vyombo vya habari, na watu wengine katika jamii na tuwasaidie wakuze tabia nzuri zinazotegemea kanuni zinazofaa. Kanuni bora za mwenendo huwasaidia wakatae kitu chochote chenye madhara.”—Grégoire, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

“Ni lazima nidhamu itolewe kwa uthabiti, kwa haki, na bila kubadilika-badilika. Ni lazima watoto waelewe matokeo mabaya ya kuvunja sheria na wajue kwamba unamaanisha kile unachosema.”—Owen, Uingereza.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

“Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

MASIMULIZI YA FAMILIA

Kufanikiwa Ukiwa Mzazi Asiye na Mwenzi

Mahojiano na Lucinda Forster

Ni hali gani ngumu zaidi unayokabili ukiwa mzazi asiye na mwenzi?

Kuwa mzazi si jambo rahisi, lakini nikiwa mzazi asiye na mwenzi ni vigumu sana kwangu kupangia jinsi nitakavyotumia wakati na nguvu zangu. Inachukua muda kuwafundisha kanuni na sheria na bado nipate nafasi ya kupumzika na kucheka nao. Mara nyingi ninalazimika kudhabihu wakati wangu wa kupumzika ili nifanye kazi za nyumbani.

Wewe hudumisha mawasiliano mazuri na binti zako jinsi gani?

Wazazi wanapotalikiana, watoto wanaweza kuanza kuhisi kwamba hawana usalama na kuwa na hasira. Matatizo yanapotokea, ninaona kwamba ni muhimu kuwatazama usoni na kuongea nao kwa utulivu. Mimi husubiri hadi kila mtu anapotulia, kisha ninajaribu kuwaeleza jambo linalonihangaisha bila kulifanya lionekane kama jambo kubwa sana. Mimi huwaomba maoni, kisha ninawasikiliza kwa makini, na kuwaonyesha kwamba ninajali sana hisia zao. Ninawaonyesha ninapendezwa na mambo yao ya shule na kuwapongeza kwa wanayotimiza. Sikuzote sisi hula pamoja mezani katika mazingira yaliyotulia tukiwa tumestarehe kabisa. Pia kila mara ninawaambia jinsi ninavyowapenda sana.

Wewe hutoa nidhamu jinsi gani?

Watoto wanahitaji mipaka iliyo wazi, na ni muhimu kuhakikisha kwamba haibadiliki-badiliki. Ninajaribu kuwa mwenye fadhili lakini thabiti. Ni lazima nizungumze na watoto wangu na niwaeleze kwa nini tabia fulani ni mbaya. Ninajaribu pia kuwauliza maswali ili nijue maoni yao kuhusu jambo walilofanya kabla ya kuwaadhibu. Ikiwa nimewakosea—kwa mfano, ikiwa niliwaelewa vibaya—ninawaomba msamaha.

Unatumia njia gani kuwafundisha watoto wako kuwaheshimu watu wengine?

Mimi huwakumbusha jambo ambalo Yesu alifundisha—watendee wengine kama vile unavyotaka utendewe. (Luka 6:31) Ninawatia moyo wasuluhishe matatizo yao wenyewe kwa wenyewe kadiri wanavyoweza, na ninawafundisha umuhimu wa kujibu kwa upole na kwa fadhili wanapokasirishwa.

Ninyi hufanya nini wakati wa mapumziko?

Si kila mara tunaweza kugharimia kwenda likizo mbali, kwa hiyo tunatafuta katika magazeti mambo tunayoweza kufanya ambayo hayatatugharimu sana. Tunapanga tafrija au tunatembelea maeneo yanayokuzwa mimea michanga. Tunapanda mboga kwenye bustani yetu na kufurahia kuzichuma kwa ajili ya kupika. Tafrija ni muhimu, hata kama tutatembelea tu bustani iliyo karibu na nyumbani.

Mmepata shangwe na thawabu gani?

Limekuwa jambo gumu kwetu kuishi katika familia yenye mzazi mmoja, lakini tuna uhusiano mzuri, na tumejifunza kuthamini baraka tulizo nazo. Ninafurahi ninapoona jinsi kila mtoto anavyokua na kusitawisha utu wa kipekee. Wanataka kuwa karibu nami, na ninathamini ushirika wao. Wanatambua haraka kama nimefurahi au nimehuzunika, na mara nyingine wananikumbatia ili kunihakikishia kwamba wananipenda. Mimi hufurahi sana wanaponionyesha upendo. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba tumejionea upendo wa Muumba anayetujali ambaye ametutegemeza katika hali nyingi ngumu. Biblia imeniimarisha niendelee kujitahidi kuwa mzazi bora.—Isaya 41:13.

[Picha]

Lucinda pamoja na binti zake, Brie na Shae