Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Mwenye Subira Zaidi

Jinsi ya Kuwa Mwenye Subira Zaidi

BAADA ya kusoma makala zilizotangulia, huenda ukakubali kwamba kadiri ulivyo mwenye subira ndivyo unavyokuwa na afya nzuri, unavyofanya maamuzi mazuri, na kuwa na marafiki wazuri. Kwa hiyo, unawezaje kuwa mwenye subira zaidi? Chunguza mapendekezo yafuatayo.

Tambua visababishi:

Kuna mambo au hali mbalimbali zinazoweza kumfanya mtu akose subira. Ni nini hasa hukufanya wewe ukose subira? Je, ni watu fulani hususa? Huenda mwenzi wa ndoa, wazazi, au watoto wako wakawa ndio hasa wanaokufanya ukose subira maishani. Au je, wewe hukosa subira kwa sababu ya wakati? Kwa mfano, je, wewe hukosa subira unapolazimika kuwangoja wengine au ikiwa umechelewa? Je, wewe hukosa subira unapokuwa umechoka, una njaa, una usingizi, au uko chini ya mkazo fulani? Je, wewe hukosa subira hasa unapokuwa nyumbani au kazini?

Kujua mambo yanayokufanya ukose subira kutakusaidiaje? Zamani za kale, Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.” (Methali 22:3, Biblia Habari Njema) Kupatana na methali hiyo ya kale ya Biblia, ikiwa utaona kimbele kwamba jambo fulani litakufanya ukose subira, huenda ukazuia hilo lisitokee. Huenda mwanzoni ikakubidi ujitahidi sana kuwa mwenye subira zaidi, lakini baada ya muda, kuwa na subira kunaweza kuwa jambo la kawaida kwako.

Rahisisha maisha yako:

Profesa Noreen Herzfeld, ambaye hufundisha sayansi ya kompyuta katika Chuo Kikuu cha Saint John’s huko Minnesota, Marekani anasema kwamba “watu hawawezi kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja. Ubongo hauwezi kukazia fikira mambo mbalimbali wakati uleule.” Anaongezea hivi: “Baada ya muda, kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja hupunguza uwezo wetu wa kukaza fikira, kuwa makini, na mwishowe hilo huharibu sifa nzuri kama vile subira, uthabiti, uwezo wa kufanya maamuzi mazuri, na kutatua matatizo.”

Ni vigumu kuwa mwenye subira unapokuwa na mkazo kwa sababu ya kuwa na mambo mengi ya kufanya, sehemu nyingi unazotazamiwa kwenda, na watu wengi wa kuwasiliana nao. Dakt. Jennifer Hartstein, aliyetajwa hapo awali katika mfululizo huu anaonya hivi: “Kimsingi, mkazo ndicho kisababishi cha ukosefu wa subira.”

Msemo unaojulikana sana unasema, “subira huvuta heri.” Kwa hiyo, tenga wakati wa kufurahia maisha. Tenga wakati wa kuanzisha urafiki wa karibu na watu wachache badala ya kuwa na urafiki wa kijuujuu na watu wengi. Pangia wakati wako na ufahamu mambo ya kutanguliza. Jihadhari na vifaa vya kiteknolojia na mambo mengine yanayopoteza wakati.

Ili kurahisisha maisha yako, huenda ikafaa kuchunguza ratiba yako ya kila siku. Ni utendaji gani unaopaswa kupunguza au kuondoa? Methali moja ya Biblia inasema: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu . . . , wakati wa kuweka na wakati wa kutupa.” (Mhubiri 3: 1, 6) Huenda sasa ndio wakati wa kuondoa mambo yanayochukua wakati mwingi hivi kwamba unakuwa na shughuli nyingi zinazokufanya ukose subira.

Ona mambo kihalisi:

Ona maisha kwa njia halisi. Kwanza kabisa, katika maisha ya kila siku, mambo hayafanyiki haraka kama tunavyotaka. Huwezi kutarajia mambo yatendeke wakati ambapo wewe unataka yatendeke. Unahitaji subira.

Pili, kumbuka kwamba si kila wakati unaweza kudhibiti hali zako. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, wala wenye nguvu wanaoshinda katika pigano, wala pia wenye hekima wanaopata chakula, wala pia wenye uelewaji wanaokuwa na utajiri, wala wenye ujuzi wanaopata kibali; kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote. Kwa maana mwanadamu pia hajui wakati wake.”​—Mhubiri 9:11, 12.

Badala ya kukosa subira kwa sababu ya hali ambazo huwezi kudhibiti, jaribu kutambua mambo ambayo wewe unaweza kudhibiti. Kwa mfano, badala ya kukasirika kwa sababu basi limechelewa, tafuta njia nyingine ya usafiri. Huenda hata ikawa afadhali kutembea badala ya kukosa subira na kukasirika. Ikiwa ni lazima ungojee, tumia wakati huo kufanya jambo la maana, kama vile kusoma kitu fulani au kuandika mambo unayopanga kufanya.

Ukweli wa mambo ni kwamba hakuna faida ya kuwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo huwezi kudhibiti. Biblia inasema hivi kwa kufaa: “Ni nani miongoni mwenu ambaye kwa kusumbuka anaweza kujiongeza maisha yake hata kwa saa moja?”​—Luka 12:25, Neno—​Biblia Takatifu.

Sitawisha urafiki pamoja na Mungu:

Watu wengi wanaoiamini Biblia wamegundua kwamba wanaweza kuwa na subira wanapofuata kanuni zake. Biblia inasema kwamba mtu aliye na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu ana mwelekeo wa kuonyesha subira pamoja na sifa nyingine muhimu kama vile upendo, shangwe, amani, upole, na kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Biblia inaahidi hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” (Wafilipi 4:6, 7) Soma Biblia na ujifunze jinsi unavyoweza kuwa mwenye subira zaidi na kuishi bila mahangaiko.