Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Ni Nini Humfanya Mtu Kuwa Mwanamume Halisi?

Ni Nini Humfanya Mtu Kuwa Mwanamume Halisi?

“Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka mitatu. Nyakati nyingine mimi huwaonea wivu wavulana ambao wamelelewa na baba zao. Wao huonekana wakiwa na sifa ya kujiamini kuliko mimi.”​—Alex. *

“Uhusiano kati yangu na baba yangu si mzuri. Kwa hiyo nimelazimika kujifunza mimi mwenyewe jinsi ya kuwa mwanamume halisi.”​—Jonathan.

JE, UMEWAHI kuhisi kama vijana hao ambao wamenukuliwa hapo juu? Je, una wasiwasi kwamba hutajua jinsi ya kuwa mwanamume halisi? Ikiwa ndivyo, usikate tamaa!

Fikiria jinsi unavyoweza kushinda vikwazo viwili ambavyo hutokea mara kwa mara.

KIKWAZO CHA 1: Maoni yasiyofaa kuhusu sifa za mwanamume halisi

Mambo ambayo wengine husema:

  • Wanaume halisi ni sugu; hawapaswi kulia.

  • Wanaume halisi hawakubali yeyote awaongoze.

  • Wanaume ni bora kuliko wanawake.

Maoni yanayofaa: Kuna tofauti kubwa kati ya mwanamume halisi na mvulana. Lakini hilo halimaanishi kwamba mwanamume ni bora kuliko mwanamke. Unakuwa mwanamume halisi unapoacha tabia za kitoto. Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Kwa maneno mengine, kadiri unavyoacha kufikiri, kuzungumza, na kutenda kama mtoto na kuanza kufikiri, kuzungumza, na kutenda kama mtu mkomavu ndivyo unavyozidi kuthibitisha kwamba wewe ni mwanamume halisi. *

Jaribu kufanya hivi: Chukua karatasi na uandike majibu ya maswali yafuatayo:

  1. Ni katika njia gani tayari mimi nimefanya maendeleo katika kuondolea mbali “tabia za mtoto”?

  2. Ni mambo gani ninayoweza kufanyia maendeleo zaidi?

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa: Luka 7:36-50. Ona jinsi ambavyo Yesu alijithibitisha kuwa mwanamume halisi kwa (1) kutetea mambo ya kweli na (2) kuwatendea wengine​—kutia ndani wanawake—​kwa heshima.

“Ninavutiwa na sifa za rafiki yangu, Ken. Yeye ni mwanamume imara​—kimwili, kihisia, na kiroho—​lakini pia ni mtu mwenye fadhili. Mfano wake umenifundisha kwamba mwanamume halisi hawavunjii wengine heshima ili tu yeye aonekane kuwa bora zaidi.”​—Jonathan.

KIKWAZO CHA 2: Kulelewa bila baba

Mambo ambayo wengine husema:

  • Ikiwa hukulelewa na baba, hutawahi kamwe kujifunza jinsi ya kuwa mwanamume halisi.

  • Ikiwa baba yako alikuwa mtu mwenye sifa mbaya, lazima wewe pia utakuwa hivyo.

Maoni yanayofaa: Hata ikiwa hukuwa na baba au hakukuwekea mfano mzuri, hilo halimaanishi huwezi kuwa mwanamume halisi! Unaweza kushinda vikwazo hivyo. (2 Wakorintho 10:4) Unaweza kuchagua kufuata ushauri ambao Mfalme Daudi alimpa mwanaye Sulemani: “Uwe na nguvu na ujionyeshe kuwa mwanamume.”​—1 Wafalme 2:2.

Kusema kweli, inaweza kuwa vigumu kuishi na baba ambaye hakujali​—au hata bila baba kabisa. “Mtu anapolelewa bila baba anakuwa na pengo kubwa maishani,” anasema Alex, aliyenukuliwa kwenye utangulizi wa makala hii. “Nina umri wa miaka 25, lakini ninahisi kana kwamba sasa ninajifunza mambo ambayo nilipaswa kujifunza nilipokuwa bado mvulana mdogo.” Ikiwa wewe pia unahisi kama Alex, unaweza kufanya nini?

Jaribu kufanya hivi: Tafuta mtu ambaye atakuwa mshauri wako—mtu aliye na sifa za mwanamume halisi. * Muulize ni sifa gani ambazo anaona mwanamume halisi anapaswa kuwa nazo. Kisha muulize jinsi wewe unavyoweza kuiga sifa hizo pia.​—Methali 1:5.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa: Methali sura ya 1-9. Jaribu kutambua ushauri unaoweza kusaidia mvulana akue na kuwa mwanamume wa kiroho na mwenye hekima.

“Ninafurahi kwamba nimeanza kuwa mwanamume halisi. Ingawa natamani baba yangu angenisaidia kufanya maendeleo, bado nina uhakika kuwa nitafaulu kusitawisha sifa ninazohitaji. Si lazima nishindwe.”​—Jonathan.

 

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 24 Wazee katika kutaniko la Kikristo wanaweza kuwa washauri wazuri.

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Unafikiri ni sifa gani zinazomtambulisha mwanamume halisi? Kwa sasa nimekomaa kwa kadiri gani?