Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Nitazamie Nini Katika Ndoa?​—Sehemu ya 1

Nitazamie Nini Katika Ndoa?​—Sehemu ya 1

“Tunapokuwa pamoja mimi huwa na furaha sana! Ninasubiri kwa hamu wakati tutakapooana!”

“Hatupatani kwa njia yoyote. Badala ya kuwa wenzi wa ndoa, sisi ni kama tu watu wanaoishi katika nyumba moja. Ninajihisi mpweke sana!”

HUENDA tayari umekisia kwamba taarifa ya kwanza iliyo juu ilisemwa na msichana ambaye hajaolewa; taarifa ya pili ilisemwa na mtu ambaye amefunga ndoa. Lakini huenda usitambue kwamba taarifa zote hizo ni za mtu yuleyule.

Ni nini kilichobadilika? Ikiwa unatazamia kufunga ndoa wakati fulani, unaweza kufanya nini ili ndoto ya kuwa na uhusiano mzuri wa kimahaba isigeuke na kuwa ndoa yenye msukosuko?

Ukweli wa mambo: Kuwa na furaha katika ndoa kunategemea hasa yale unayotazamia katika ndoa hiyo.

Makala hii​—pamoja na makala ya “Vijana Huuliza” katika toleo la mwezi ujao la Amkeni!​—itakusaidia kuwa na matarajio halisi.

Ni mambo gani halisi unayoweza kutarajia unapofunga ndoa? Kwa ufupi, unaweza:

  1.  Kutarajia kupata faida

  2.  Kutarajia kupata magumu

  3.  Kutarajia mambo yasiyotazamiwa

Acha tuchunguze mambo hayo kwa undani moja baada ya lingine.

TARAJIA KUPATA FAIDA

Biblia inazungumza kuhusu ndoa kwa njia inayofaa. (Methali 18:22) Unaweza kutarajia faida zifuatazo.

Mwenzi. Biblia inasema kwamba muda fulani baada ya yule mtu wa kwanza, Adamu kuumbwa, Mungu alisema: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake,” na baada ya hapo Mungu akamuumba Hawa awe mwandamani wa Adamu. (Mwanzo 2:18) Mungu alimuumba kila mmoja wao akiwa na sifa za pekee ili kwamba wawe tofauti, lakini waweze pia kupatana. Kwa hiyo, mume na mke ni wenzi wanaofaana kabisa.—Methali 5:18.

Ushirikiano. Biblia inasema: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja. . . . Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.” (Mhubiri 4:9, 10) Hilo ni kweli kuhusu ndoa. “Lazima mshirikiane na kuwa wanyenyekevu na pia kuwa tayari kukubali maoni ya mwenzako mara kwa mara,” anasema mwanamke aliyeolewa hivi karibuni anayeitwa Brenda. *

Uhusiano wa karibu. Biblia inasema: “Mume na ampe mke wake haki yake; lakini mke pia na amfanyie vivyo hivyo mume wake.” (1 Wakorintho 7:3) Unapofunga ndoa, unaweza kufurahia kufanya ngono bila kuwa na wasiwasi au kujuta kama inavyokuwa mara nyingi mtu anapofanya ngono kabla ya ndoa.​—Methali 7:22, 23; 1 Wakorintho 7:8, 9.

Jambo kuu: Ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Yakobo 1:17) Unapofuata kanuni zake, unaweza kutazamia kuwa na maisha ya ndoa yenye kuthawabisha sana.

Jambo la kufikiria: Je, maoni yako kuhusu ndoa yameathiriwa na vielelezo vibaya ambayo umejionea—labda katika familia yenu? Ikiwa ndivyo, ni vielelezo gani vinavyofaa ambavyo unaweza kufikiria na kuiga?

TARAJIA KUPATA MAGUMU

Biblia inaelezea hali halisi ya ndoa. (1 Wakorintho 7:28) Yafuatayo ni baadhi ya magumu unayoweza kutarajia.

Mizozo. Hakuna watu wawili wanaofanana kabisa. Tunafanana tu katika maana ya kwamba sote hatujakamilika. (Waroma 3:23) Kwa hiyo, mara kwa mara mume na mke watazozana, hata ikiwa wanapatana katika mambo mengi kadiri gani. Nyakati nyingine wanaweza hata kusema mambo yasiyopendeza ambayo watajutia baadaye. “Mtu asiyejikwaa katika kunena, . . . ni mtu mkamilifu,” inasema Biblia. (Yakobo 3:2, Union Version) Badala ya kujaribu kuepuka mizozo yote, wenzi wa ndoa waliofanikiwa hujifunza jinsi ya kuizungumzia na kuishughulikia inapotokea.

Kukatishwa tamaa. “Kuna sinema na programu nyingi sana za televisheni zinazomwonyesha msichana akimpata mvulana ‘anayemfaa zaidi’ kisha wanaishi raha mstarehe,” anasema msichana anayeitwa Karen. Ndoa yao isipokuwa kama hiyo inayoigizwa katika vitabu na sinema, wenzi wanaweza kukata tamaa. Bila shaka, baada ya kufunga ndoa, wenzi watagundua udhaifu na tabia nyingine zisizopendeza kuhusu kila mmoja wao. Jambo kuu ni kukumbuka kwamba upendo wa kweli “huvumilia mambo yote”​—kutia ndani kukatishwa tamaa.​—1 Wakorintho 13:4, 7.

Mahangaiko. Biblia inasema kwamba watu waliooana “huhangaikia mambo ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 7:33, 34) Ni kawaida kuwa na mahangaiko hayo na huenda hata yakafaa. Kwa mfano, huenda ikawa vigumu kulipia gharama za lazima. Huenda mume na mke wakahitajika kufanya kazi ili tu waweze kulipia chakula, mavazi, na mahali pa kuishi. Lakini mnaweza kufaulu mkisaidiana kuandaa mahitaji ya familia yenu.​—1 Timotheo 5:8.

Jambo kuu: Ikiwa uchumba unaweza kulinganishwa na kurusha tiara, ndoa ni kama kuendesha ndege. Unahitaji ustadi na jitihada nyingi zaidi kushughulika na magumu yanapotokea​—lakini unaweza kufaulu.

Jambo la kufikiria: Unashughulikiaje mizozo sasa kati yako na wazazi au na ndugu na dada zako? Unapokatishwa tamaa, je, unaweza kudumisha maoni yanayofaa kuhusu hali yako? Unashughulikaje na mahangaiko?

KATIKA MAKALA INAYOFUATA YA “VIJANA HUULIZA” . . . Kanuni za Biblia zinaweza kukusaidiaje kutarajia mambo yasiyotazamiwa?

 

^ fu. 17 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.