Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | ELDAR NEBOLSIN

Mpiga Piano Stadi Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Mpiga Piano Stadi Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Eldar Nebolsin ni mpiga piano wa kimataifa kutoka Uzbekistan. Amepiga piano akishirikiana na okestra jijini London, Moscow, St. Petersburg, New York, Paris, Rome, Sydney, Tokyo, na Vienna. Eldar alilelewa katika Muungano wa Sovieti na wazazi walioamini kwamba hakuna Mungu. Lakini baadaye alifikia mkataa kwamba wanadamu waliumbwa na Mungu mwenye upendo. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji kuhusu kazi yake ya muziki na imani yake katika Mungu.

Ulikujaje kuwa mwanamuziki?

Wazazi wangu ni wapiga piano. Walianza kunifundisha kupiga piano nilipokuwa na umri wa miaka mitano. Baadaye, nilipata masomo maalumu ya muziki katika shule ya watoto wenye vipawa huko Tashkent.

Hebu tueleze ugumu wa kupiga piano ukishirikiana na okestra.

Hakuna okestra mbili zinazofanana. Hizo ni kama ala kubwa za muziki zinazopigwa na viongozi wao. Labda ugumu mkubwa kwa mpiga piano ni kufuatana na mwelekezo wa kiongozi. Ni kama mazungumzo kati ya marafiki—badala ya mtu mmoja tu kutawala mazungumzo wakati wote, kila mmoja anapaswa kusikiliza mwingine anapoongea. Kwa kawaida, una nafasi moja au mbili tu za kufanya mazoezi na kujenga uhusiano huo kabla ya kwenda jukwaani.

Unatumia wakati mwingi kadiri gani kufanya mazoezi?

Angalau saa tatu kwa siku—na ikiwa muziki una sehemu fulani ngumu ninalazimika kutumia muda mwingi zaidi. Pia, mimi huchunguza muundo wa muziki ninaotayarisha—bila hata kupiga piano yenyewe. Pia mimi husikiliza muziki mwingine wa mtungaji huyohuyo ili niweze kuelewa vizuri muziki wake ninaotaka kupiga.

Mpiga piano bora anaweza kutambuliwaje?

Anatambuliwa kwa uwezo wake wa kufanya piano “iimbe.” Acha nifafanue. Piano ni ala inayotoa sauti ikibonyezwa. Sauti inayotokezwa baada ya noti kubonyezwa inaweza kupungua—tofauti na sauti ya mwanadamu au ala za kupulizwa ambazo zinaweza kudumisha kiwango kilekile cha  sauti au hata kuongeza sauti. Tatizo kubwa analokabili mpiga piano ni kuzuia sauti ya noti iliyobonyezwa kufifia. Wanafanya hivyo kwa kuchezesha vidole na vifundo vya mikono kwa ustadi, na wakati huohuo wakitumia kikanyagio cha upande wa kulia cha piano ambacho huongeza muda wa sauti ya noti iliyobonyezwa na kubadili uzito wa noti hiyo. Wapiga piano wanapokuwa stadi kabisa kutumia mbinu hizo ngumu, wanaweza kufanya piano itoe sauti kama ya filimbi, baragumu, au kama sauti ya okestra. Pia wanaweza kuifanya itokeze sauti inayofanana na ala bora kabisa ya muziki, yaani, sauti ya mwanadamu.

Ni wazi kwamba unapenda sana muziki.

Kwa maoni yangu, muziki ndiyo njia ya kueleza na kuonyesha hisia ambazo si rahisi kuzieleza kwa maneno au ambazo hata haziwezi kuelezeka.

Ni nini kilichokufanya upendezwe na mambo ya kiroho?

Siku zote nyumba yetu ilikuwa na vitabu vingi ambavyo baba yangu alivileta kutoka Moscow. Kitabu kilichonivutia sana kilikuwa na hadithi za Biblia kuhusu mambo yalivyokuwa mwanzoni na yale yaliyowapata Waisraeli. Kitabu kingine nilichokipenda kilikuwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. * Nilivutiwa na jinsi kitabu hicho kilivyoeleza mafundisho ya Biblia kwa njia iliyoeleweka. Mwaka wa 1991 nilipohamia Hispania kujifunza muziki, nilikibeba na kukisoma mara kadhaa. Niligundua imani ambayo haitegemei tu hisia bali pia inapatana na akili na uthibitisho wenye kusadikisha.

Fundisho lililonivutia sana lilikuwa ahadi ya Biblia kwamba wanadamu wanaweza kuishi milele duniani. Ahadi hiyo ilipatana sana na akili! Mpaka wakati huo bado sikuwa nimekutana na Mashahidi wa Yehova. Lakini niliazimia kwamba nikikutana nao, nitaomba wanifundishe Biblia.

Ulikutanaje na Mashahidi?

Siku chache baada ya kufanya azimio hilo, niliwaona wanawake wawili wakiwa na Biblia mikononi mwao. Nilijiambia ‘Wanafanana na watu niliosoma kuwahusu katika kitabu changu. Wanahubiri kama Wakristo katika nyakati za Biblia walivyofanya.’ Punde si punde, nilikuwa nikijifunza Biblia na Shahidi mmoja. Leo, shangwe yangu kubwa ni kuwasaidia wengine wajifunze kuhusu Muumba wetu.

Nini kilichokusadikisha uamini kuwa kuna Muumba?

Muziki ndio ulionisadikisha. Karibu kila mtu hupenda muziki, jambo ambalo wanyama hawawezi kufanya. Muziki unaweza kueleza shangwe, uhakika, upendo, au hisia nyingine yoyote ambayo mtu anaweza kupata. Kiasili sisi huvutiwa na mdundo wa muziki. Hata hivyo, je, muziki ni muhimu ili wanadamu waendelee kuishi? Je, unatimiza fungu lolote katika “kusalimika kwa viumbe bora,” kama wanamageuzi wanavyofundisha? Sidhani. Kwa maoni yangu, haipatani na akili kuamini kwamba ubongo wa mwanadamu, wenye uwezo wa kutunga na kufurahia muziki kama ule wa Mozart na Beethoven, ulitokana na mageuzi. Wazo linalopatana na akili zaidi ni kwamba ubongo wetu umebuniwa na Muumba mwenye hekima na upendo.

Biblia ni kama muziki uliopangwa kwa ustadi wa hali ya juu na wenye ujumbe unaogusa mioyo ya wanadamu wote

Nini kilichokufanya uamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu?

Biblia ni mkusanyiko wa vitabu vidogo-vidogo 66 vilivyoandikwa kwa zaidi ya miaka 1,600 na wanaume wapatao 40. Nilijiuliza, ‘Ni nani anayeweza kuwa aliongoza kuandikwa kwa kitabu hicho kilichoandikwa kwa ustadi na upatano kabisa?’ Inapatana na akili kuamini kwamba ni Mungu. Kwa maoni yangu, Biblia ni kama muziki uliopangwa kwa ustadi wa hali ya juu na wenye ujumbe unaogusa mioyo ya wanadamu wote.

^ fu. 15 Sasa Mashahidi wa Yehova wanatumia kitabu cha kujifunzia Biblia kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kitabu hicho kinaweza kupatikana katika Tovuti ya www.ps8318.com.