Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Ninahangaikia Sura Yangu Kupita Kiasi?

Je, Ninahangaikia Sura Yangu Kupita Kiasi?

 Maswali: Je, ninahangaika kupita kiasi?

  1.   Kati ya sentensi zifuatazo, ni ipi inayoeleza jinsi unavyohisi?

    •  Sipendi hata kidogo jinsi ninavyoonekana.

    •  Nyakati nyingine mimi hupenda jinsi ninavyoonekana.

    •  Hakuna wakati ambapo mimi sipendi jinsi ninavyoonekana.

  2.   Ungependa kubadili nini hasa katika mwili wako?

    •  Kimo

    •  Uzito

    •  Umbo

    •  Nywele

    •  Rangi

    •  Ukubwa wa misuli

    •  Jambo lingine

  3.   Kamilisha sentensi ifuatayo.

     Mimi huaibika zaidi kuhusu mwili wangu . . .

    •  ninaposimama juu ya mashine ya kupimia uzito.

    •  ninapotazama kioo.

    •  ninapojilinganisha na wengine (marafiki, wanamitindo, waigizaji filamu).

  4.   Kamilisha sentensi ifuatayo.

     Mimi hupima uzito wangu . . .

    •  kila siku.

    •  kila juma.

    •  hata baada ya juma kupita.

  5.   Ni maneno gani yanayoelezea vizuri jinsi unavyohisi?

    •  Maoni yasiyofaa. (Mfano: “Kila mara ninapotazama kioo, ninaona umbo la mtu mnene kupita kiasi na asiyevutia. Hata nimewahi kujinyima chakula ili kupunguza uzito.”​—Serena.)

    •  Maoni yenye usawaziko. (Mfano: “Hakuwezi kosa kuwa na jambo ambalo hatupendi kuhusu mwili wetu, kwa hiyo tunahitaji tu kukubali mambo fulani. Ni upumbavu kuwa na hofu kuhusu jambo ambalo hatuwezi kubadili.”​—Natanya.)

 Biblia inatueleza tusijifikirie wenyewe zaidi “kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Waroma 12:3) Kwa hiyo, inafaa kwamba tujifikirie kwa kadiri fulani. Hiyo ndiyo sababu unapiga mswaki na kuhangaikia usafi wako.

 Lakini namna gani ikiwa mara nyingi unavunjika moyo kuhusu sura yako, labda hata kufikia hatua ya kufikiria sura yako kupita kiasi? Ikiwa ndivyo, huenda ukajiuliza . . .

 ‘Kwa nini nina maoni yasiyofaa kuhusu sura yangu?’

 Huenda kukawa na sababu kadhaa. Hizo zinatia ndani:

  •  Kuathiriwa na vyombo vya habari. “Vijana wanaonyeshwa picha nyingi sana zinazowafanya wahisi kwamba lazima wawe wembamba kabisa na wenye sura yenye kuvutia kila wakati. Kwa sababu hiyo, mtu asipofikia kiwango hicho, anajihisi kuwa anachukiza!”​—Kellie.

  •  Kuathiriwa na wazazi. “Nimetambua kwamba ikiwa mama anahangaikia sura yake kupita kiasi, mara nyingi binti yake huwa na maoni kama yake. Akina baba huwaathiri wana wao kwa njia hiyohiyo.”​—Rita.

  •  Kutojiheshimu. “Watu ambao wanahangaikia sana sura yao hutafuta kupongezwa na wengine kila wakati kuhusu jinsi wanavyoonekana. Inachosha kuwa na mtu kama huyo!”​—Jeanne.

 Hata sura yako iweje, huenda ukawa unajiuliza . . .

 ‘Je, nibadili sura yangu?’

 Fikiria kile ambacho vijana wenzako wanasema.

 “Huenda usifaulu kubadili kile ambacho hupendi katika sura yako, kwa hiyo ni jambo la busara kukubali kasoro zako. Ukifanya hivyo, huenda watu wengine hawatazitambua.”​—Rori.

 “Fanya yote uwezayo ili udumishe afya yako. Ikiwa una afya nzuri, utaonekana kama unavyopaswa kuonekana. Na ikiwa mtu hakupendi kwa sababu ya utu wako (anapendezwa tu na sura yako), huyo si rafiki yako.”​—Olivia.

 Jambo la msingi: Fanya yote uwezayo ili uwe na sura nzuri. Lakini usihangaikie mambo mengine. Kuhangaikia sura yako kupita kiasi kunaweza kuwa hatari. (Ona “ Hadithi ya Julia.”)

 Kwa upande mwingine, kuwa na usawaziko kutakusaidia kuwa na maoni yanayofaa kujihusu, kama msichana anayeitwa Erin alivyogundua. Anasema hivi: “Ni kweli kwamba mimi huwa na wasiwasi kuhusu sura yangu, lakini nimeona kwamba ninapokazia fikira mambo yasiyofaa, mimi hujihisi vibaya tu. Kwa hiyo, mimi hufanya mazoezi kwa ukawaida na kula vizuri. Sihangaikii mambo mengine.”

 Mabadiliko bora zaidi!

 Unapokuwa na mtazamo unaofaa kuhusu sura yako, utajihisi (na hata kuonekana) vizuri. Biblia inaweza kukusaidia. Inakutia moyo usitawishe sifa zifuatazo:

  •  Uradhi. “ Afadhali kuridhika na ulicho nacho kuliko kuhangaika kwa kutamani kitu kingine.”​—Mhubiri 6:9, Biblia Habari Njema.

  •  Usawaziko kuhusu kufanya mazoezi. “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.”​—1 Timotheo 4:8.

  •  Urembo wa ndani. “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.”​—1 Samweli 16:7.

 “Sura yetu huonyesha maoni yetu kuhusu sura yetu. Iwapo mtu ameridhika, wengine huona hilo na wanavutiwa naye mara moja.”​—Sarah.

 “Mtu mrembo anaweza kuvutia wengine upesi. Lakini mtu uliye kwa ndani na sifa zako nzuri ndiyo mambo ambayo watu watakumbuka hasa kukuhusu.”​—Phylicia.

 Ona pia Methali 11:22; Wakolosai 3:​10, 12; 1 Petro 3:​3, 4.