Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Umaarufu Mtandaoni Ni Muhimu Kadiri Gani?

Umaarufu Mtandaoni Ni Muhimu Kadiri Gani?

 Msichana fulani anayeitwa Elaine anasema hivi: “Nilipoona kwamba wanafunzi wenzangu walikuwa na mamia ya watu wanaowafuata kwenye mitandao ya kijamii, nilijiambia, ‘Kwa kweli, wao ni maarufu!’ Lazima nikiri kwamba niliwaonea wivu kidogo.”

 Je, umewahi kuhisi hivyo? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kuepuka mahangaiko ya kujaribu kuwa maarufu kwenye Intaneti.

 Kuna hatari zipi?

 Kwenye Methali 22:1, Biblia inasema kwamba “afadhali kuchagua jina jema kuliko mali nyingi.” Kwa hiyo, hakuna ubaya kutaka kuwa na sifa nzuri, au kutaka kupendwa.

 Lakini nyakati fulani tamaa ya kukubaliwa inaweza kubadilika kuwa tamaa ya kupata umaarufu. Je, kuna hatari ya kufanya hivyo? Onya, mwenye umri wa miaka 16, anaweza kusema ndiyo:

 “Nimewaona watu wakifanya mambo ya ajabu, kama vile kuruka kutoka kwenye orofa ya pili shuleni, ili tu wapate umaarufu.”

 Watu fulani hurekodi video ya mambo ya kipumbavu wanayofanya na kuiweka kwenye mtandao ili tu wengine wawatambue. Kwa mfano, baadhi ya vijana waliweka video kwenye mtandao iliyowaonyesha wakila sabuni zenye sumu, jambo ambalo hakuna mtu anayepaswa kamwe kufanya!

 Biblia inasema hivi: “Msifanye chochote . . . kwa majivuno ya bure.”—Wafilipi 2:3, Biblia Habari Njema.

 Jambo la kufikiria:

  •   Kupata umaarufu kwenye mtandao ni muhimu kadiri gani kwako?

  •   Je, unaweza kuhatarisha afya au uhai wako ili tu rafiki zako wakutambue au wakukubali?

 “Ndoto ya umaarufu”

 Si nyakati zote ambazo watu hufanya mambo hatari ili kujipatia umaarufu. Erica, mwenye umri wa miaka 22, anaeleza jinsi watu fulani hutumia mbinu nyingine:

 “Watu fulani huweka picha nyingi sana za maisha yao, ili kufanya ionekane kwamba wana marafiki wengi sana wa karibu ambao wanatumia wakati pamoja nao. Hilo huwafanya wengine wafikiri wao ni maarufu sana.”

 Cara, mwenye umri wa miaka 15, anasema kwamba watu fulani hutumia uwongo ili kufanya ionekane wao ni maarufu:

 “Nimewahi kuwaona watu wakipachika picha za uwongo ili tu waonekane kwamba walikuwa kwenye karamu fulani wakati kwa kweli walikuwa nyumbani.”

 Matthew, mwenye umri wa miaka 21, anakiri kwamba amewahi kufanya jambo kama hilo:

 “Niliweka picha fulani na kusema nilikuwa nimepanda juu ya Mlima Everest, ingawa sijawahi kwenda Asia hata mara moja!”

 Biblia inasema hivi: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

 Jambo la kufikiria:

  •   Unapotumia mitandao ya kijamii, je, wewe hutumia uwongo ili tu uwe maarufu?

  •    Je, picha na maelezo unayoweka yanaonyesha jinsi ulivyo kikweli na viwango vyako?

 Wafuasi na alama ya kupenda ni muhimu kadiri gani?

 Watu wengi huamini kwamba umaarufu kwenye mtandao unategemea kuwa na wafuasi wengi na alama nyingi za watu kupenda walichopachika. Matthew, aliyenukuliwa awali, anakiri kwamba zamani alihisi hivyo:

 “Ningewauliza watu, ‘Wewe una wafuasi wangapi?’ au ‘Ni kiasi gani cha juu zaidi ambacho umewahi kupata za alama ya kupendwa?’ Ili kuongeza idadi ya wafuasi, ningewafuata watu ambao hata sikuwajua, nikitarajia kwamba wangenifuata pia. Nilisitawisha pupa ya kupata umaarufu, na mtandao wa kijamii ulichochea pupa hiyo.”

Umaarufu mtandaoni ni kama chakula kisicho na lishe—huenda kikafaa kwa muda mfupi lakini hakitoshelezi mahitaji yako

 Maria, mwenye umri wa miaka 25, anasema kwamba watu fulani hupima thamani yao kwa idadi ya wafuasi na alama za kupendwa wanazopokea:

 “Msichana anapoweka picha yake na isipate alama nyingi kwamba watu wanaipenda, atakata kauli kwamba yeye si mrembo. Bila shaka, huo ni uamuzi usiofaa, lakini watu wengi katika hali hiyo wangeitikia kama yeye. Ni kana kwamba wanajinyanyasa kwenye mtandao.”

 Biblia inasema hivi: “Tusiwe tukijisifu, tusichochee mashindano kati yetu, wala tusioneane wivu.”—Wagalatia 5:26.

 Jambo la kufikiria:

  •   Ikiwa unatumia mitandao ya kijamii, je, wewe huona inakuchochea ujilinganishe na wengine?

  •   Je, wewe huona idadi ya wafuasi kuwa muhimu kuliko kuwa na marafiki wanaokujali kikweli?