Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kufanya Mambo Mengi kwa Wakati Mmoja?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kufanya Mambo Mengi kwa Wakati Mmoja?

 Una uwezo wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja?

 Je, unaweza kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja? Watu wengi wanafikiri kwamba watoto wanaolelewa katika maeneo yaliyoendelea kiteknolojia, ambao wakati mwingine wanaitwa “wazao wa kidijitali,” wana uwezo mzuri zaidi wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja kuliko watu wenye umri mkubwa zaidi ambao walijifunza kuhusu teknolojia baadaye maishani. Je, hilo ni kweli?

 KWELI au SI KWELI

  •   Ukifanya mambo mengi kwa wakati mmoja utayafanya kwa muda mfupi zaidi.

  •   Ukifanya mazoezi, unaweza kuboresha uwezo wako wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja.

  •   Vijana wana uwezo mkubwa wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja kuliko watu wenye umri mkubwa zaidi.

 Ikiwa umejibu “kweli” kwa mojawapo ya mambo yaliyotajwa, huenda umedanganywa kuamini kwamba unaweza kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja.

 Uwongo kuhusu kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja

 Je, unaamini kwamba unaweza kufanya mambo mawili kwa wakati mmoja? Huenda ukafaulu kufanya mambo fulani kwa wakati mmoja bila kuchanganyikiwa ikiwa jambo moja halihitaji uangalifu mkubwa. Kwa mfano, unaweza kusikiliza muziki huku ukisafisha chumba chako.

 Lakini ukifanya mambo mawili yanayohitaji uangalifu mkubwa kwa wakati mmoja, hutafanya yote vizuri. Labda ndiyo sababu msichana anayeitwa Katherine alisema hivi kuhusu kufanya mambo mawili kwa wakati mmoja: “Ni uwezo wa kuharibu kila kitu kwa wakati mmoja.”

 “Nilikuwa nikiongea na mtu fulani kisha nikapokea ujumbe kwenye simu ambao nilihitaji kuujibu. Nilijaribu kufanya mambo yote mawili kwa wakati mmoja. Matokeo ni kwamba sikusikia jambo ambalo yule mtu alikuwa akiniambia na nilikosea maandishi kwenye ujumbe niliotuma.”—Caleb.

 Sherry Turkle ambaye ni mtaalamu wa teknolojia aliandika hivi: “Tunapodhani kwamba tunafanya mambo mengi kwa wakati mmoja, . . . uwezo wetu unapungua kila tunapoanza kufanya jambo lingine la ziada wakati huohuo. Mfumo wetu wa neva husisimka na tunahisi kwamba tunafanya kazi vizuri zaidi ingawa kwa kweli tunafanya vibaya zaidi.” a

 “Wakati mwingine ninadhani kwamba ninafanya vizuri ninapoandika ujumbe kwenye simu na wakati huohuo kuzungumza na mtu fulani, kisha ninajikuta nikimwambia mtu huyo jibu la ujumbe wa simu au ninaandika kwenye ujumbe wa simu jambo ambalo nilipaswa kumwambia mtu ninayezungumza naye!”—Tamara.

 Watu wanaojaribu kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja wanaweza kufanya maisha yao yawe magumu zaidi. Kwa mfano, wanatumia muda mwingi zaidi kumaliza kazi za shuleni. Au huenda wakatumia muda kufanya tena kazi ambazo walidhani wamemaliza. Vyovyote vile, watu wanaofanya mambo mengi kwa wakati mmoja hukosa muda wa kufanya mambo wanayopenda kufanya!

 Ndio sababu Thomas Kersting, daktari na mshauri wa shule alisema hivi: “Kama ubongo unaweza kulinganishwa na kabati la kuhifadhi faili kwa mpangilio mzuri, basi ubongo wa watu wanaofanya mambo mengi kwa wakati mmoja ni kama kabati lenye karatasi zilizotapakaa kila mahali.” b

 “Kadiri unavyofanya mambo mengi kwa wakati mmoja, ndivyo unavyozidi kupuuza habari muhimu. Mwishowe huenda ukajiletea kazi nyingi zaidi na kupoteza muda ambao ulidhani kwamba utaokoa.”—Teresa.

Kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja ni kama kuendesha gari kwenye barabara mbili kwa wakati mmoja

 Njia bora zaidi

  •   Jizoeze kukazia fikira jambo moja kwa wakati mmoja. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, hasa ikiwa umezoea kufanya mambo kadhaa kwa wakati mmoja—kwa mfano kusoma huku ukiandika ujumbe kwenye simu. Lakini Biblia inasema “mhakikishe mambo muhimu zaidi.” (Wafilipi 1:10) Kazi unazopaswa kufanya zinatofautiana inapohusu umuhimu wake. Basi amua kazi ambayo utafanya kwanza, na ukazie fikira kazi hiyo hadi utakapoimaliza kabisa.

     “Akili isiyo na mpangilio ni kama mtoto mchanga; lazima uikataze kufanya mambo fulani, ingawa huenda ikawa rahisi kuiacha ifanye kile inachotaka.”—Maria.

  •   Ondoa mambo yanayoweza kukukengeusha. Je, unashawishiwa kuangalia simu yako unaposoma? Basi iweke kwenye chumba kingine. Zima televisheni, na hata usifikirie kuhusu mitandao ya kijamii! Biblia inasema: ‘Tumia vizuri kabisa wakati wako.’—Wakolosai 4:5.

     “Nimegundua kwamba ni vizuri zaidi kwangu kukazia fikira jambo moja kwa wakati mmoja. Ninapofanya hivyo ninapata furaha zaidi ninapofuta jambo hilo kwenye orodha ya mambo ninayopaswa kufanya na kuanza kufanya jambo linalofuata. Hilo hufanya niridhike sana.”—Onya.

  •   Usikengeuke wakati wa mazungumzo. Kutumia simu unapozungumza na mtu mwingine hakupunguzi tu uwezo wako bali pia ni kukosa adabu. Biblia inatushauri kwamba tuwatendee wengine kama tunavyotaka watutendee.—Mathayo 7:12.

     “Wakati fulani ninapozungumza na dada yangu, yeye humwandikia mtu fulani ujumbe kwenye simu au kufanya jambo lingine kwenye simu yake. Hilo huniudhi sana! Lakini ukweli ni kwamba wakati mwingine mimi hufanya hivyo pia!”—David.

a Kutoka kwenye kitabu Reclaiming Conversation.

b Kutoka kwenye kitabu Disconnected