Hamia kwenye habari

Nifanye Nini Ikiwa Ninachoshwa na Shule?

Nifanye Nini Ikiwa Ninachoshwa na Shule?

Unachohitaji

 Maoni yanayofaa kuhusu elimu. Jaribu kuona mambo kwa njia inayofaa. Si kila somo shuleni ambalo huenda likaonekana kuwa na manufaa ya siku za usoni—angalau kwa sasa huenda isionekane hivyo. Lakini, elimu ya jumla katika masomo mbalimbali itakusaidia kuuelewa ulimwengu unaokuzunguka. Itakusaidia “kuwa mambo yote kwa watu wa namna zote,” na kukuwezesha kuzungumza na watu wenye malezi mbalimbali. (1 Wakorintho 9:22) Angalau, utaboresha uwezo wako wa kufikiri, uwezo ambao bila shaka utakufaidi sana hatimaye.

Kwenda shule ni sawa na kukata miti ili kutengeneza njia—inawezekana, ukiwa na vifaa vinavyofaa

 Maoni yanayofaa kuhusu mwalimu wako. Ikiwa unaona mwalimu wenu hafundishi kwa njia yenye kupendeza, kazia fikira somo lenyewe, badala ya kumkazia fikira mwalimu. Kumbuka, huenda mwalimu wako amewafundisha wanafunzi wa madarasa mengine masomo yaleyale mara kadhaa au hata mamia ya mara. Kwa hiyo, huenda si rahisi kwake kufundisha kwa shauku jinsi alivyokuwa akifundisha mwanzoni alipoanza kazi ya ualimu.

 Pendekezo: Andika habari mnazofundishwa, omba habari zaidi kwa heshima, na uwe na maoni yanayofaa kuhusu somo lenyewe. Ukiwa na maoni yanayofaa, wengine pia watakuiga.

 Maoni yanayofaa kuhusu uwezo wako. Shule inaweza kukusaidia kukuza vipaji ambavyo hukujua unavyo. Paulo alimwandikia hivi Timotheo: “Ukiweke motomoto kile kipaji ulichopewa na Mungu.” (2 Timotheo 1:6, Biblia Habari Njema) Yaonekana kwamba Timotheo alikuwa amepewa kipaji fulani cha roho takatifu. Lakini “kipaji” hicho kilihitaji kukuzwa ili kisikae tu, au kupotea. Ni kweli kwamba uwezo wako wa kielimu hautoki moja kwa moja kwa Mungu. Hata hivyo, vipaji ulivyo navyo ni vyako wewe. Shule inaweza kukusaidia kugundua na kukuza uwezo ambao hukujua unao.