Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kudhibitije Matumizi Yangu ya Pesa?

Ninaweza Kudhibitije Matumizi Yangu ya Pesa?

 “Hivi karibuni niliingia dukani ili kuangalia tu bidhaa zinazouzwa. Hata hivyo, nilijikuta nimenunua bidhaa fulani ya bei ghali ambayo sikupanga kuinunua!”​—Colin.

 Colin anakubali kwamba ana tatizo la kushindwa kudhibiti matumizi yake ya pesa. Je, wewe una tatizo kama hilo? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia.

 Kwa nini udhibiti matumizi yako ya pesa?

 Uwongo: Ukikazia fikira jinsi unavyotumia pesa zako, utakosa uhuru.

 Ukweli: Kudhibiti matumizi yako ya pesa kutakupa uhuru mwingi sana. Kitabu I’m Broke! The Money Handbook kinasema hivi: “Kadiri unavyojifunza kuhifadhi pesa, ndivyo utakavyokuwa na pesa nyingi kwa ajili ya kununua vitu unavyotaka sasa na wakati ujao.”

 Zingatia: Kwa kudhibiti matumizi yako ya pesa . . .

  •   Utakuwa na pesa za kutosha wakati unapozihitaji. Tineja anayeitwa Inez anasema hivi: “Wakati ujao ninatamani kusafiri kwenda Amerika Kusini. Ninapohifadhi pesa zangu, ninajaribu kukumbuka lengo hilo.”

  •   Utakuwa na madeni machache (au hutakuwa nayo kabisa). Biblia inasema: “Mkopaji ni mtumwa wa mkopeshaji.” (Methali 22:7) Msichana anayeitwa Anna anasema hivi: “Madeni yanaweza kutawala maisha yako. Kutokuwa na madeni kunakusaidia kukazia fikira malengo yako.”

  •   Unajionyesha kwamba umekomaa. Vijana wanaodhibiti matumizi yao ya pesa wanajitayarisha vizuri kwa ajili ya kuwa watu wazima. Kijana mwenye umri wa miaka 20 anayeitwa Jean anasema hivi: “Hayo ni mazoezi mazuri kwa ajili ya wakati ujao, nitakapoanza kujitegemea. Ninajitahidi kutumia vizuri pesa zangu sasa, ili nifaulu kufanya hivyo wakati ujao.”

 Jambo kuu: Kitabu The Complete Guide to Personal Finance: For Teenagers and College Students kinasema hivi: “Kudhibiti matumizi yako ya pesa ndiyo hatua bora na ya kwanza ya kujitegemea. Kujifunza kutumia pesa zako vizuri ni kipawa ambacho kitakusaidia baadaye maishani.”

 Jinsi ya kudhibiti matumizi yako ya pesa

 Tambua udhaifu wako. Ikiwa kila wakati unajikuta huna pesa, jambo la kwanza ni kutambua jinsi unavyozitumia. Kwa baadhi ya watu, chanzo kikuu cha matumizi mabaya ya pesa ni kununua vitu mtandaoni. Kwa wengine, tatizo kubwa wanalokabili ni kununua vitu kidogo-kidogo na mwishowe wanajikuta hawana pesa mwisho wa mwezi!

 “Pesa hupotea unaponunua vitu vidogo-vidogo kila siku. Kila mwezi unaponunua zawadi mara kwa mara, unakunywa kahawa, unanunua kitu kilichopunguzwa bei, bila kutambua unajikuta umetumia pesa nyingi sana!”​—Hailey.

 Panga bajeti. Biblia inasema hivi: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.” (Methali 21:5) Unapopanga bajeti utahakikisha kwamba matumizi yako hayazidi kipato chako.

 “Ikiwa unatumia pesa nyingi kuliko kipato chako, chunguza jinsi unavyotumia pesa zako na uepuke kununua vitu usivyohitaji. Punguza orodha ya matumizi mpaka kipato chako kizidi matumizi yako.”​—Danielle.

 Fuata bajeti yako. Kuna njia nyingi unazoweza kutumia ili kufahamu jinsi unavyotumia pesa zako na kuepuka matumizi yasiyo ya lazima. Baadhi ya vijana wameona njia zifuatazo zinasaidia kuhifadhi pesa:

  •  “Kwa kawaida, ninaweka pesa benki mara baada ya kuzipata kwa sababu ninajua sitashawishiwa kuzitumia zikiwa huko.”​—David.

  •  “Ninapokwenda dukani, ninaenda na pesa ninazohitaji tu. Kwa hiyo siwezi kutumia pesa nyingi kuliko nilivyokusudia.”​—Ellen.

  •  “Kadiri ninavyotumia muda mrefu kabla ya kununua kitu, ndivyo ninavyopata muda wa kuamua ikiwa ninakihitaji au la.”​—Jesiah.

  •  “Siwezi kwenda katika kila tafrija! Ni sawa kusema hapana ikiwa sina pesa.”​—Jennifer.

 Jambo kuu: Kudhibiti matumizi ya pesa ni wajibu mzito. Colin aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii ameanza kutambua jambo hilo, anasema hivi: “Ikiwa siku moja nitakuwa kichwa cha familia, lazima nijifunze kuepuka kutumia pesa ovyoovyo! Ikiwa sasa nikiwa mseja nashindwa kutumia vizuri pesa zangu, sitaweza kufanya hivyo nikioa.”

Dokezo: “Mwambie mtu fulani achunguze bajeti yako, na umwombe awasiliane nawe mara kwa mara kuihusu. Kuwajibika ni jambo zuri!”​—Vanessa.