Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanyeje Ninapopewa Ushauri Unaoumiza Hisia?

Nifanyeje Ninapopewa Ushauri Unaoumiza Hisia?

 Jichunguze

 Nyakati nyingine, sote tunahitaji ushauri, yaani maagizo yatakayotusaidia kuboresha kazi au mtazamo wetu. Kuhusu jambo hilo, fikiria hali zifuatazo.

  1.  Mwalimu wako anakuambia hukufanya vizuri katika mradi fulani wa masomo. Anasema: “Unahitaji kutumia muda mwingi zaidi kufanya utafiti.”

     Utafanyaje ukipewa ushauri huo unaoumiza hisia?

    1.   Utaukataa. (‘Huyu mwalimu huwa hanipendi.’)

    2.   Utaukubali. (‘Nitatumia ushauri wake katika mradi unaofuata.’)

  2.  Mama yako anakuambia kwamba chumba chako ni kichafu—ingawa umetoka tu kukisafisha.

     Utafanyaje ukipewa ushauri huo unaoumiza hisia?

    1.   Utaukataa. (‘Sikuzote mama haridhiki.’)

    2.   Utaukubali. (‘Ni kweli nilipaswa kufanya usafi kwa makini zaidi.’)

  3.  Mdogo wako wa kike anakuambia hapendi jinsi unavyomwambia jambo la kufanya kila mara.

     Utafanyaje ukipewa ushauri huo unaoumiza hisia zako?

    1.   Utaukataa. (‘Yeye ni nani mpaka aniambie hivyo?’)

    2.   Nitaukubali. (‘Nafikiri ninaweza kumtendea vizuri zaidi.’)

 Baadhi ya vijana wanaweza kulinganishwa na glasi—wao ni dhaifu sana hivi kwamba wanaweza kuvunjika upesi wanapopewa ushauri wowote mdogo unaowaumiza hisia. Je, wewe uko hivyo? Ikiwa ndivyo, basi unakosa nafasi muhimu sana maishani! Kwa nini? Kwa sababu kujifunza kukubali ushauri unaoumiza hisia ni ustadi muhimu ambao utakusaidia sasa na pia utakapokuwa mtu mzima.

Usikatae ushauri unaohitaji kusikia kwa sababu tu hutaki kuusikia

 Kwa nini ninahitaji ushauri ambao unaumiza hisia?

  •   Kwa sababu wewe si mkamilifu. Biblia inasema: “Sisi sote hufanya makosa mara nyingi.” (Yakobo 3:2, maelezo ya chini) Hiyo ndiyo sababu kila mtu anahitaji ushauri hata kama unamuumiza hisia.

     “Mimi hujitahidi kukumbuka kwamba sote si wakamilifu na kwamba ni jambo la kawaida kufanya makosa maishani. Basi ninaporekebishwa, mimi hujitahidi kujifunza kutokana na ushauri huo na kuepuka kurudia kosa hilo.”—David.

  •   Kwa sababu unaweza kuboresha uwezo wako. Biblia inasema: “Mfundishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima.” (Methali 9:9) Ushauri unaoumiza hisia unaweza kukusaidia—ikiwa utaukubali.

     “Sikupenda kupewa ushauri hasa ikiwa uliniumiza hisia. Nilifikiri ushauri huo uliniaibisha. Lakini sasa ninaukubali hata ninaomba ushauri. Ningependa kujua ni wapi ninapoweza kufanya marekebisho.”—Selena.

 Bila shaka, unaweza kuomba ushauri ambao huenda utakuumiza hisia. Lakini unaposhauriwa bila kutarajia, hali inaweza kuwa tofauti. “Nilipatwa na hofu na kuvunjika moyo,” anasema Natalie, anapokumbuka wakati alipopokea kadi yenye ushauri ambao hakuwa ameomba. “Nilijitahidi sana kufanya mambo vizuri, lakini matokeo niliyopata ni ushauri ulioniumiza!”

 Je, umewahi kupatwa na jambo kama hilo? Ikiwa ndivyo, unawezaje kushughulika na hali hiyo?

 Ninawezaje kukubali ushauri unaoumiza hisia?

  •   Sikiliza.

     Biblia inasema: “Mtu mwenye ujuzi huyazuia maneno yake, na mtu mwenye utambuzi atabaki mtulivu.” (Methali 17:27) Usimkatize mtu anayezungumza na wewe. Usijibu kwa hasira na kusema jambo ambalo utajutia baadaye!

     “Ninapokosolewa, mimi huwa na mwelekeo wa kujitetea. Badala yake, ninapaswa kujifunza kutokana na ushauri huo na kufanya mambo kwa njia bora wakati ujao.”—Sara.

  •   Kazia fikira ushauri, si mtu anayetoa ushauri.

     Huenda ukashawishiwa kuangalia kasoro za mtu anayekukosoa. Lakini ni bora kufuata ushauri wa Biblia na kuwa “mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.” (Yakobo 1:19) Kwa kawaida kuna ukweli fulani katika ushauri unaopewa. Usikose kupokea ushauri unaohitaji kusikia kwa sababu tu hutaki kuusikia.

     “Nilikuwa nikikasirika kila mara wazazi wangu waliponirekebisha na kusema, ‘Ninajua, ninajua.’ Lakini ninapowasikiliza na kufuata ushauri wao, ninapata matokeo bora.”—Edward.

  •   Uwe na maoni yaliyosawazika kujihusu.

     Unapopewa ushauri wenye kuumiza haimaanisha kwamba wewe ni mjinga. Inamaanisha kwamba wewe hukosea, kama watu wengine. Hata mtu anayekushauri anahitaji kukosolewa mara kwa mara. Kwa kweli, Biblia inasema: “Hakuna mtu mwadilifu duniani anayefanya mema sikuzote na hatendi dhambi kamwe.”—Mhubiri 7:20.

     “Rafiki yangu alinipa ushauri ulioniumiza ambao sikudhani niliuhitaji. Nilimshukuru kwa kuwa mnyoofu, lakini niliudhika. Hata hivyo, baada ya muda nilitambua kwamba ushauri wake ulikuwa na ukweli fulani. Kupitia ushauri wake, nilitambua jambo nililohitaji kufanyia kazi—jambo ambalo singetambua bila msaada wake.”—Sophia.

  •   Jiwekee mradi wa kufanya marekebisho.

     Biblia inasema kwamba mtu “mwerevu hukubali kurekebishwa.” (Methali 15:5) Ukikubali ushauri, utasahau hisia zozote za kuumiza na kujitahidi kufanyia marekebisho mambo uliyoshauriwa. Andika hatua utakazochukua, na uweke rekodi ya maendeleo yako kwa miezi kadhaa.

     “Kukubali ushauri kunahusiana na unyoofu kwa sababu unapaswa kuwa mnyoofu ili kukubali makosa yako, kuomba msamaha, na ujifunze jinsi ya kufanya marekebisho.”—Emma.

 Jambo la msingi: Biblia inasema: “Kama chuma kinavyonoa chuma, ndivyo mtu anavyomnoa rafiki yake.” (Methali 27:17) Ushauri unaojenga ni kifaa kinachoweza kukunoa, sasa na utakapokuwa mtu mzima.