Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Ufanye nini Unaposhauriwa?

Ufanye nini Unaposhauriwa?

KIKWAZO

“Mtu anapokushauri, kwa kweli anakuambia umekosea. Na sijawahi kumsikia mtu akisema, ‘Ninapenda kukosolewa!’”—Amy, 17. *

Mtu anayekataa kushauriwa ni kama rubani anayekataa mwongozo kutoka kwenye uwanja wa ndege anaweza kusababisha aksidenti.

Je, wakati mwingine unashindwa kukubali unaposhauriwa na wazazi wako, walimu, au watu wengine? Kama ni hivyo, basi makala hii itakusaidia.

UNACHOPASWA KUJUA

Kila mtu anahitaji kushauriwa.

“Sisi sote hujikwaa mara nyingi.”—Yakobo 3:2.

“Mtu hapaswi kuaibika anaposhauriwa baada ya kufanya makosa.”—Jessica.

Unaposhauriwa haimaanishi kwamba wewe ni mtu mbaya.

“Yeye ambaye Yehova * anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.”Methali 3:12.

“Mtu anaponishauri ninajaribu kuwazia jinsi ilivyokuwa vigumu kwake kunishauri na jinsi anavyonipenda kwa kunipa mawaidha.”—Tamara.

Ushauri unaweza kukusaidia uwe mtu mzuri zaidi.

“Sikiliza nidhamu upate kuwa na hekima.”Methali 8:33.

“Mtu anahitaji ushauri ili akomae. Ushauri unakusaidia kujua jinsi wengine wanavyokuona na unakusaidia kuacha tabia zinazoudhi ambazo huenda hukujua kama unazo.”—Deanne.

 UNACHOWEZA KUFANYA

Jaribu kuona mambo kihalisi. Inawezekana kwamba wewe hukasirika unaposhauriwa. Lakini jaribu kuzuia hisia zako. Ili ufanye hivyo, jiwazie kwamba unampa ushauri huohuo mtu mwingine, labda ndugu au dada yako. Je, sasa unaona faida za ushauri huo? Sasa fikiria ushauri unaopewa na uone mambo kwa njia hiyohiyo.——Kanuni ya Biblia:— Mhubiri 7:9.

“Wakati mwingine unaweza kukasirika sana unaposhauriwa hivi kwamba unasahau mtu anayekushauri anajaribu kukusaidia uwe mtu mzuri, bali si kwamba anataka kukuumiza hisia.”—Theresa.

Uwe mnyenyekevu. Usiruhusu kiburi kikuzuie kukubali ushauri. Kwa upande mwingine, usivunjike moyo eti kwa sababu unahitaji kufanya marekebisho fulani. Unyenyekevu utakusaidia katika hali hizo mbili. Kumbuka: Ushauri unaokuumiza zaidi huenda ndio ushauri unaohitaji zaidi. Ukiukataa, basi utakosa nafasi muhimu ya kukomaa.—Kanuni ya Biblia: Methali 16:18.

Ushauri unaokuumiza zaidi huenda ndio ushauri unaohitaji zaidi

“Kukubali ushauri ni sehemu muhimu ya kuwa mtu mkomavu. Tusipojifunza kukubali ushauri na kuruhusu utusaidie kukomaa, mwishowe sisi ndio tutakaoumia.”—Lena.

Onyesha shukrani. Hata unapohisi kwamba ni vigumu kukubali ushauri fulani, kwa nini usimshukuru mtu anayekushauri? Bila shaka, mtu huyo hana nia mbaya na kwa kweli anataka ufanikiwe.—Kanuni ya Biblia: Zaburi 141:5.

Si vibaya kusema ‘Asante,’ hasa ikiwa ulihitaji kushauriwa. Hata kama haukuhitaji, unaweza kuonyesha kwamba unathamini jitihada za mtu aliyekushauri.”—Carla.

^ fu. 4 Baadhi ya majina yamebadilishwa katika makala hii.

^ fu. 11 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

Mtu anayekataa kushauriwa ni kama rubani anayekataa mwongozo kutoka kwenye uwanja wa ndege. Anaweza kusababisha aksidenti.