Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Mimi Hutazamia Ukamilifu?

Je, Mimi Hutazamia Ukamilifu?

 Ikiwa

  •   unatarajia tu kupata A+ kwenye mtihani

  •   unaepuka kufanya kitu kipya ukiogopa kwamba hutafaulu

  •   unaona kila rekebisho kuwa linaharibu sifa yako

 . . . , basi huenda jibu la swali lililoulizwa juu ni ndiyo. Lakini, je, hilo ni jambo zito sana?

 Kutazamia ukamilifu kuna ubaya gani?

 Hakuna ubaya wa kujaribu kufanya mambo kwa njia bora kabisa. Hata hivyo, “kuna tofauti kubwa kati ya kufanya mambo kwa njia bora na kujitahidi kufanya mambo yasiyowezekana,” kinasema kitabu Perfectionism​—What’s Bad About Being Too Good? Kitabu hicho kinaongezea hivi: “Kutazamia ukamilifu kunaweza kuwa mzigo mzito kwa sababu hakuna mwanadamu mkamilifu.”

 Biblia inakubaliana na maoni hayo. Inasema hivi: “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema.” (Mhubiri 7:​20) Kwa kuwa wewe si mkamilifu, wakati mwingine utafanya mambo kwa kiwango cha chini.

 Je, ni vigumu kwako kukubali hilo? Ikiwa ndivyo, fikiria njia nne ambazo kutazamia ukamilifu kunaweza kukuathiri kwa njia isiyofaa.

  1.   Jinsi unavyojiona. Watu wanaotazamia ukamilifu hujiwekea viwango vya juu kupita kiasi na bila shaka watavunjika moyo. “Kihalisi, hatuwezi kufanya vizuri katika kila jambo, na ikiwa kila wakati tutajilaumu kwa kutotimiza malengo yetu ya juu kupita kiasi, hatimaye tutaacha kujiamini. Hilo litafanya tushuke moyo.”​—Alicia.

  2.   Jinsi unavyohisi unaporekebishwa. Watu wanaotazamia ukamilifu huwa na tabia ya kuona ushauri wa kuwarekebisha kama kuharibiwa sifa. Kijana mmoja anayeitwa Jeremy anasema hivi: “Ninaporekebishwa, ninahisi vibaya sana. Kutazamia ukamilifu kunafanya mtu ashindwe kutambua mipaka yake na kukubali msaada anaohitaji.”

  3.   Jinsi unavyowaona wengine. Watu wanaotazamia ukamilifu mara nyingi huwakosoa wengine. Anna mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Ikiwa unatarajia ukamilifu, utataka watu wote wawe na viwango kama vyako. Watu wanaposhindwa kufikia viwango vyako, unawaona kuwa hawafai.”

  4.   Jinsi wengine wanavyokuona. Ikiwa unatarajia wengine wafanye mambo ya juu kupita ilivyo kawaida, usishangae watu wanapoanza kukukwepa! Msichana anayeitwa Beth anasema hivi: “Kujitahidi kufikia viwango vya juu kupita kiasi vya mtu anayetazamia ukamilifu kunachosha. Hakuna anayependa kuwa karibu na mtu wa namna hiyo!”

 Je, kuna njia nyingine bora ya kufanya mambo?

 Biblia inasema hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Watu wenye usawaziko ni wale wasiotazamia kufanya mambo kupita uwezo wao na hawatazamii wengine wafanye hivyo.

 “Kuna mambo mengi yanayotusonga maishani. Kwa nini ujiongezee mkazo wa kuwa mtu anayetazamia ukamilifu? Ni vigumu kukabiliana na mkazo huo!”​—Nyla.

 Biblia inasema ‘tuwe na kiasi katika kutembea na Mungu wetu.’ (Mika 6:8) Watu wenye kiasi hutambua mipaka yao. Hawajirundikii majukumu mengi kuliko wanayoweza kutimiza; wala hawapotezi muda mwingi kufanya mambo wasiyoweza kufanya.

 “Ili nihisi kwamba ninatimiza wajibu wangu vizuri, mimi hukubali majukumu kwa usawaziko. Ninatambua kwamba siwezi kufanya mambo mengi kupita kiasi.”​—Hailey.

 Biblia inasema hivi: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Mhubiri 9:​10) Kwa hiyo, dawa ya kukabiliana na kutazamia ukamilifu si uvivu, bali ni kufanya kazi kwa bidii, lakini tukiwa na sifa zilizotajwa hapo juu​—usawaziko na kiasi.

 “Ninajaribu kufanya kazi yangu vizuri kadiri niwezavyo, na ninaifanya kwa bidii. Ninatambua kwamba haitakuwa kamilifu, lakini ninafurahi kujua kwamba nilifanya yote niwezayo.”​—Joshua.