Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | FRÉDÉRIC DUMOULIN

Mtaalamu Anayefanya Utafiti Anaelezea Kuhusu Imani Yake

Mtaalamu Anayefanya Utafiti Anaelezea Kuhusu Imani Yake

Kwa zaidi ya miaka kumi, Frédéric Dumoulin amefanya kazi ya utafiti wa madawa kwenye Chuo Kikuu cha Ghent, Ubelgiji. Zamani hakuamini kuna Mungu. Lakini baadaye alianza kuamini kwamba Mungu ndiye aliyeumba kila kitu. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji Frédéric—ambaye sasa ni Shahidi wa Yehova—kuhusu kazi yake na pia imani yake.

Je, ulikuwa mfuasi wa dini ulipokuwa mtoto?

Ndiyo. Mama yangu alikuwa Mkatoliki. Lakini niliposoma kuhusu Vita vya Kidini na Baraza la Kuhukumu Waasi wa Kidini, nilichukia dini na sikutaka kujihusisha nayo. Pia, nilisoma kuhusu dini zisizo za Kikristo lakini hazikuwa tofauti. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilihisi kwamba kuenea kwa ufisadi ndani ya dini ni uthibitisho kwamba hakuna Mungu. Kwa hiyo, nilipojifunza shuleni kuhusu nadharia ya mageuzi, niliamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe.

Kwa nini ulivutiwa na sayansi?

Nilipokuwa na umri wa miaka saba, nilipewa darubini na niliipenda sana. Kati ya mambo mengine, niliitumia kuchunguza wadudu mbalimbali, kama vile vipepeo.

Kwa nini ulitaka kujua chanzo cha uhai?

Nilipokuwa na umri wa miaka 22, nilikutana na mwanasayansi ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova. Aliamini kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai. Nilishangaa sana. Nilidhani kwamba ningeweza kukosoa imani yake. Hata hivyo, alijibu maswali yangu kwa njia nzuri. Nilianza kuwachunguza watu wanaoamini kuna Mungu.

Miezi michache baadaye nilikutana na Shahidi mwingine ambaye alikuwa mtaalamu wa matibabu. Alipoeleza kuhusu imani yake nilimsikiliza kwa sababu nilitaka kujua kwa nini watu wanamwamini Mungu. Nilitaka kumsaidia ili aache kupotoshwa.

Je, ulifaulu kumsadikisha kwamba amekosea?

Hapana, nilishindwa. Nilianza kuchunguza nadharia mbalimbali  kuhusu chanzo cha uhai. Hata hivyo, nilishangaa kugundua kwamba baadhi ya wanasayansi maarufu wanasema kwamba hata chembe ndogo kabisa ya uhai ni tata sana hivi kwamba haikujitokeza yenyewe. Wengine wao wanaamini chembe hizo zilitoka kwenye anga ya mbali. Hawakubaliani kuhusu chanzo cha uhai.

Je, kuna jambo wanalokubaliana?

Kwa kushangaza, wanasayansi wengi wanakubaliana kwamba kwa njia fulani uhai ulitokana na vitu visivyo hai. Nilianza kujiuliza, ‘Ikiwa hawajui jinsi uhai ulivyojitokeza bila kuumbwa, wanawezaje kuwa na uhakika na wanayosema?’ Nikaanza kuchunguza mafundisho ya Biblia kuhusu chanzo cha uhai.

Ulionaje yale ambayo Biblia inasema?

Kadiri nilivyoendelea kusoma Biblia ndivyo nilivyozidi kuona kwamba inasema ukweli. Kwa mfano, hivi karibuni wanasayansi wamegundua kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Lakini mstari wa kwanza kwenye Biblia, ulioandikwa karibu miaka 3,500 iliyopita unasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” * Niliona kwamba kila jambo ambalo Biblia inataja kuhusu sayansi, ni sahihi kabisa.

Niliona kwamba kila jambo ambalo Biblia inataja kuhusu sayansi, ni sahihi kabisa

Je, ujuzi wako wa sayansi ulikuzuia kumwamini Mungu?

La hasha! Nilipoanza kuamini kuna Mungu, bado nilikuwa mwanafunzi wa chuo kikuu. Kufikia sasa, kadiri ninavyoendelea kusoma kuhusu viumbe hai, ndivyo ninavyozidi kuamini kuna Muumba.

Je, unaweza kutoa mfano?

Ndiyo. Nimechunguza jinsi dawa na sumu zinavyoathiri viumbe hai. Jambo linaloshangaza ni jinsi ubongo wetu unavyolindwa dhidi ya bakteria na vitu vingine hatari. Kuna kizuizi kati ya damu na chembe za ubongo.

Kwa nini hilo ni jambo la kushangaza?

Zaidi ya miaka 100 iliyopita, watafiti waligundua kwamba vitu vinavyoingia kwenye mzunguko wa damu huingia kwenye kila sehemu ya mwili—isipokuwa kwenye ubongo na uti wa mgongo. Jambo hilo linanishangaza, kwa sababu mishipa midogo hupeleka damu kwenye chembe zote za ubongo. Chembe zote za ubongo husafishwa, hulishwa, na hupata oksijeni kutoka kwenye damu. Sasa, inawezekanaje kwamba damu yetu itenganishwe na chembe za ubongo? Kwa miaka mingi hilo halikueleweka.

Kizuizi hicho hufanyaje kazi?

Mishipa midogo ya damu ni tofauti sana na mirija ya plastiki ambayo hutenganisha kitu kilicho ndani na kilicho nje. Kuta za mishipa ya damu zimeundwa kwa chembe. Chembe hizo huruhusu vitu mbalimbali kutia ndani bakteria kuingia na kutoka. Hata hivyo, chembe zinazounda mishipa ya damu katika ubongo ni tofauti. Mishipa hiyo imeunganishwa kwa ukaribu sana. Chembe hizo pamoja na miungano hiyo inastaajabisha. Mpangilio huo mkubwa na tata huhakikisha kwamba vitu fulani—kama vile oksijeni, kaboni dioksidi, na glukosi—vinapita kwenye mzunguko wa damu na kwenye ubongo kwa njia nzuri. Lakini vitu vingine kama vile, protini, na chembechembe huzuiwa. Kwa hiyo, kizuizi kati ya damu na ubongo kina molekuli zenye uwezo wa kuzuia chembechembe, kemikali, na nguvu za umeme. Mimi naona kwamba haiwezekani ubunifu huo ulitokana na mageuzi.