Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | USIKATE TAMAA!

Kwa Sababu Kuna Msaada

Kwa Sababu Kuna Msaada

“[Mtupieni Mungu] mahangaiko yenu yote . . . , kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 PETRO 5:7.

Kifo kinaweza kuonekana kuwa bora kuliko kuishi unapohisi huwezi kubadili hali yako. Hata hivyo, hebu fikiria mambo yafuatayo ambayo yanaweza kukusaidia.

Sala. Kusali si njia ya kukufanya uhisi vizuri tu wala si jambo tunalofanya tunapokata tamaa. Ni mawasiliano halisi kati yako na Yehova Mungu, ambaye anakujali. Yehova anataka umweleze mambo yanayokuhangaisha. Kwa hakika, Biblia inatuhimiza hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.”Zaburi 55:22.

Kwa nini usizungumze na Mungu katika sala leo? Tumia jina lake, Yehova, na umweleze yaliyo moyoni mwako. (Zaburi 62:8) Yehova anataka uwe rafiki yake. (Isaya 55:6; Yakobo 2:23) Sala ni njia ya mawasiliano unayoweza kutumia wakati wowote na mahali popote.

Kulingana na uchunguzi wa Shirika la Marekani la Kuzuia Kujiua, “utafiti umeonyesha kwamba idadi kubwa ya watu waliojiua, yaani, asilimia 90 au zaidi, walikuwa na ugonjwa wa kiakili walipojiua. Hata hivyo, mara nyingi ugonjwa huo haukutambuliwa, haukupimwa, au kutibiwa ifaavyo”

Watu wanaokujali. Uhai wako ni muhimu kwa wengine kutia ndani watu wa familia yako au marafiki ambao huenda tayari wameonyesha kwamba wanakujali. Watu wanaokujali wanatia ndani watu ambao hujawahi kuwaona. Kwa mfano, katika utumishi wao, mara nyingine Mashahidi wa Yehova hukutana na watu waliofadhaika, na baadhi ya watu hao wamekiri kwamba walihitaji sana msaada na walikuwa wamefikiria kujiua. Kuhubiri nyumba kwa nyumba kumewapa Mashahidi wa Yehova nafasi ya pekee ya kuwasaidia watu kama hao. Mashahidi wa Yehova wanamwiga Yesu kwa kuwajali wanadamu wenzao. Wanakujali wewe pia.

Yohana 13:35.

Msaada wa wataalamu. Mawazo ya kujiua mara nyingi huletwa na ugonjwa wa kubadilika kwa hisia kama vile kushuka moyo. Hupaswi kuaibika iwapo una ugonjwa wa kihisia kwani ni sawa tu na ugonjwa mwingine. Kwa kweli kushuka moyo kumeitwa “homa ya akili.” Mtu yeyote anaweza kupatwa na ugonjwa huo na unaweza kutibiwa. *

KUMBUKA: Kwa kawaida, huwezi kupambana peke yako na ugonjwa wa kushuka moyo. Hata hivyo, unaweza kufaulu ikiwa utasaidiwa.

UNACHOWEZA KUFANYA SASA: Tafuta daktari anayetegemeka ambaye hutibu magonjwa ya kihisia kama vile kushuka moyo.

^ fu. 9 Ikiwa unalemewa na mawazo ya kujiua au hayaishi, tafuta msaada labda kwa kupiga simu kwenye kituo cha kutoa msaada au kwenye idara ya hospitali inayoshughulikia hali za dharura. Utapata wataalamu wanaoweza kukusaidia.