Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Kuwafundisha Watoto Sifa ya Kujizuia

Kuwafundisha Watoto Sifa ya Kujizuia

KIKWAZO

Inaonekana kwamba mwana wako mwenye umri wa miaka sita hana sifa ya kujizuia. Anapoona kitu anachopenda, anataka apewe wakati huohuo! Anapokasirika mara nyingi yeye hukupiga-piga. Unajiuliza: ‘Je, ni kawaida kwa mtoto kutenda hivi?’ ‘Je, ni hali tu ya muda, au ninapaswa kumfundisha sifa ya kujizuia?’ *

MAMBO UNAYOHITAJI KUJUA

Mtazamo wa watu leo huathiri sifa ya kujizuia. Dakt. David Walsh anasema hivi: “Katika tamaduni nyingi zilizokubaliwa, watu wazima na watoto husikia kwa ukawaida ujumbe unaosema kwamba tunapaswa kufanya jambo lolote tunalotaka. Ujumbe huo unaochochea watu kufanya lolote wanalotaka, hutolewa na watu wenye nia njema ya kusaidia kuboresha maisha ya watu na pia watu wenye nia ya kupata pesa tu.” *

Ni muhimu kumfundisha mtoto mapema sifa ya kujizuia. Katika uchunguzi uliofanywa kwa muda mrefu, watafiti waliwapa watoto wenye umri wa miaka minne pipi moja-moja na kuwaambia kwamba wanaweza kuamua ama kula pipi hizo mara moja au kusubiri kwa kipindi fulani kifupi ili wapewe pipi nyingine ikiwa zawadi kwa sababu ya kuonyesha sifa ya subira. Baadaye maishani, walipohitimu shule za sekondari, watoto walioonyesha sifa ya kujizuia, walikuwa na hali nzuri kihisia, walikuwa na mahusiano mazuri na watu, na walifanya vizuri katika masomo kuliko wale waliokosa sifa hiyo.

Kuna madhara makubwa ya kutowafundisha watoto sifa ya kujizuia. Watafiti wanaamini kwamba ubongo wa mtoto unaweza kuathiriwa na hali anazopitia. Dakt. Dan Kindlon, anafafanua jambo hilo hivi: “Tukiendekeza watoto wetu, tusipoacha wajifunze kuwa na subira, tusipochelewa kuwapa wanachohitaji na kuwafundisha jinsi ya kupinga vishawishi, mabadiliko ya mfumo wa neva unaohusianishwa kwa ukaribu na ukuzi wa utu hayawezi kutokea.” *

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Weka mfano. Je, wewe hujitahidi kuwa na sifa ya kujizuia? Je, watoto wako hukuona ukiwa umekasirika kunapokuwa na foleni ya magari, ukishindwa kufuata utaratibu wa kusimama katika foleni unapokuwa dukani, au ukiwakatiza wengine wanapozungumza? “Njia nzuri zaidi ya kuwasaidia watoto wetu kuwa na sifa ya kujizuia ni kwa sisi wenyewe kwanza kujitahidi kuionyesha,” anaandika Kindlon.—Kanuni ya Biblia: Waroma 12:9.

Wafundishe watoto kuhusu matokeo ya kutojizuia. Ikitegemea umri wa mtoto, msaidie kuona kwamba kuna faida anapojizuia na hasara ya kutofanya hivyo. Kwa mfano, ikiwa mtoto wako amekasirika kwa sababu ya kutendewa isivyo haki na mtu, msaidie atulie na ajiulize hivi: ‘Je, kulipiza kisasi kutanisaidia au kutaongeza tatizo? Je, kuna njia yoyote nzuri ya kushughulikia hali hii—labda kwa kuhesabu moja mpaka kumi na hivyo kuruhusu hasira ipungue? Je, huenda ikafaa zaidi nikiondoka?’—Kanuni ya Biblia: Wagalatia 6:7.

Mpongeze mtoto wako. Mpongeze mtoto wako anapoonyesha sifa ya kujizuia. Mweleze kwamba huenda isiwe rahisi sikuzote kuonyesha sifa hiyo, hata hivyo anafanya vema kila mara anapoionyesha. Biblia inasema hivi: “Mtu asiyezuia roho yake ni kama jiji lililobomolewa, lisilo na ukuta.” (Methali 25:28) Kinyume na hilo, “asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu.”—Methali 16:32.

Tenda. Unaweza kumfundisha mtoto wako kwa kuwa na kipindi cha maigizo chenye maswali kama vile: “Ungefanya Nini?” au “Maamuzi Mazuri, Maamuzi Mabaya” au jambo lingine kama hilo. Zungumzieni hali mbalimbali zinazohusiana na mambo hayo na jinsi ya kukabiliana nazo, kisha kuonyesha ikiwa ni “nzuri” au “mbaya.” Uwe mbunifu: Ukipenda, unaweza kutumia vikaragosi, michoro, au mbinu yoyote ili kufanya zoezi hilo liwe lenye kufurahisha na pia kufundisha. Lengo lako liwe kumsaidia mtoto kutambua kwamba kujizuia ni bora kuliko kufanya mambo haraka-haraka.—Kanuni ya Biblia: Methali 29:11.

Uwe na subira. Biblia inasema hivi: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” (Methali 22:15) Hivyo, usitarajie kwamba mtoto wako atasitawisha sifa ya kujizuia mara moja. “Hilo huchukua muda mrefu na maendeleo hufanyika polepole, makosa hujitokeza, na hatimaye mafanikio,” kinasema kitabu Teach Your Children Well. Hata hivyo, jitihada hizo si za bure. Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Mtoto anayeweza kujizuia, atakuwa na uwezo mkubwa wa kujiepusha na dawa za kulevya atakapokuwa na umri wa miaka kumi na mbili au kujiepusha na ngono atakapokuwa na umri wa miaka kumi na nne.”

^ fu. 4 Ingawa tunamzungumzia mtoto wa kiume, kanuni zinazotajwa katika makala hii zinawafaa pia watoto wa kike.

^ fu. 6 Kutoka kwenye kitabu No: Why Kids—of All Ages—Need to Hear It and Ways Parents Can Say It.

^ fu. 8 Kutoka kwenye kitabu Much of a Good Thing—Raising Children of Character in an Indulgent Age.