Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Uvumilivu

Uvumilivu

Kukubali, kusamehe, na kuvumilia huleta amani. Hata hivyo, je, uvumilivu unapaswa kuwa na mipaka?

Ni nini siri ya kuwa mvumilivu?

HALI ILIVYO LEO

Ulimwenguni pote watu wanazidi kukosa sifa ya uvumilivu kwa sababu ya ubaguzi wa rangi au jamii, taifa, kabila, na dini zenye imani kali.

BIBLIA INASEMA NINI?

Wakati wa huduma yake, Yesu Kristo aliishi miongoni mwa watu waliokosa sifa ya uvumilivu. Wayahudi na Wasamaria walichukiana. (Yohana 4:9) Wanawake walidharauliwa na wanaume. Na viongozi wa kidini Wayahudi waliwadharau watu wa kawaida. (Yohana 7:49) Hata hivyo, Yesu Kristo alikuwa na mtazamo tofauti sana. Wapinzani wake walisema hivi: “Mtu huyu hukaribisha watenda-dhambi na hula pamoja nao.” (Luka 15:2) Yesu alikuwa mwenye fadhili, subira, na mvumilivu kwa kuwa alikuja, si kuhukumu watu, bali kuwaponya kiroho. Upendo ndiyo sifa kuu iliyomchochea kufanya hayo yote.—Yohana 3:17; 13:34.

Yesu ni mfano mzuri wa mtu mwenye uvumilivu kwa kuwa alikuja, si kuhukumu watu, bali kuwaponya kiroho

Upendo, sifa muhimu ili kuwa na uvumilivu, hutufanya tuwapende wengine kutoka moyoni licha ya kutokamilika au kasoro zao. Andiko la Wakolosai 3:13 linasema hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”

“Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi, kwa sababu upendo hufunika  dhambi nyingi.” 1 Petro 4:8.

Kwa nini uvumilivu una mipaka?

HALI HALISI

Jamii nyingi zinajaribu kudumisha sheria na utaratibu. Hivyo, huwawekea watu viwango vyenye usawaziko vya jinsi ya kujiendesha.

BIBLIA INASEMA NINI?

“[Upendo] haujiendeshi bila adabu.” (1 Wakorintho 13:5) Ijapokuwa Yesu aliweka mfano mzuri katika kuvumilia, hakuunga mkono ukosefu wa adabu, unafiki, wala uovu wowote. Badala yake, alishutumu kwa ujasiri mambo hayo. (Mathayo 23:13) Alisema hivi: “Kwa maana yule ambaye huzoea kufanya mambo maovu huchukia nuru [ya kweli].”—Yohana 3:20.

Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.” (Waroma 12:9) Aliishi kulingana na maneno hayo. Kwa mfano, Wakristo fulani Wayahudi walipojitenga na waamini wasio Wayahudi, Paulo aliyekuwa Myahudi, kwa ujasiri na fadhili alizungumzia hali hiyo. (Wagalatia 2:11-14) Alijua kwamba Mungu ambaye “hana ubaguzi,” hangevumilia kuona ubaguzi wa kijamii miongoni mwa watu Wake.—Matendo 10:34.

Kwa kuwa ni Wakristo, Mashahidi wa Yehova hufuata mwongozo wa maadili unaopatikana katika Biblia. (Isaya 33:22) Hata hivyo, hawavumilii uovu miongoni mwao. Kutaniko safi la Kikristo linapaswa kutochafuliwa na watu wasiofuata viwango vya Mungu. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wanatii mwongozo huu ulio wazi wa Biblia: “Ondoeni yule mtu mwovu kati yenu.”—1 Wakorintho 5:11-13.

“Enyi mnaompenda Yehova, chukieni yaliyo mabaya.”Zaburi 97:10.

Je, Mungu ataendelea kuvumilia uovu milele?

MAONI YA WATU WENGI

Uovu utaendelea kuwapo kwa kuwa ni asili ya mwanadamu.

BIBLIA INASEMA NINI

Nabii Habakuki alisali hivi kwa Yehova Mungu: ‘Kwa nini unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana hutokea, kwa nini mzozo huendelezwa?’ (Habakuki 1:3) Mungu alimhakikishia nabii wake aliyekuwa na wasiwasi kwamba angewaadhibu waovu. Mungu alisema hivi kuhusiana na ahadi hiyo: ‘Bila shaka itatimia. Haitachelewa.’—Habakuki 2:3.

Hata hivyo, watenda maovu bado wana nafasi ya kuacha mwenendo wao mbaya. “‘Je, ninapendezwa hata kidogo na kifo cha mtu mwovu,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘bali kwamba ageuke na kuziacha njia zake, naye kwa kweli aendelee kuishi?’” (Ezekieli 18:23) Wale wanaomtafuta Yehova kwa kuacha njia zao mbaya wanaweza kuwa na tumaini zuri la wakati ujao. Methali 1:33 inasema hivi: “Mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”

“Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena. .  Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”Zaburi 37:10, 11.