Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuchangiaje Kuimarisha Umoja Wetu wa Kikristo?

Unaweza Kuchangiaje Kuimarisha Umoja Wetu wa Kikristo?

“Kutoka katika yeye mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane.”​—EFE. 4:16.

NYIMBO: 53, 107

1. Ni sifa gani ambayo imekuwa ikionekana wazi katika kazi za Mungu?

TANGU mwanzo wa uumbaji, umoja umeonekana wazi katika kazi za Yehova. Akirejelewa kama hekima, Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu alisema hivi: ‘Nilikuwa kando yake (Yehova) nikiwa stadi wa kazi, nami nikawa yule ambaye yeye alimpenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku.’ (Met. 8:30) Baba na Mwana walishirikiana, nao walibuni viumbe mbalimbali tunavyoona leo. Ushirikiano haukuishia hapo. Sifa hiyo ilionekana safina ilipokuwa ikijengwa katika siku za Noa; watu wa Mungu walipokuwa wakisimamisha, wakibomoa, na kusafirisha maskani nyikani; na hata wakati wa kupiga muziki na kuunganisha sauti kumsifu Yehova hekaluni. Mambo hayo yote yalihitaji ushirikiano.—Mwa. 6:14-16, 22; Hes. 4:4-32; 1 Nya. 25:1-8.

2. (a) Ni sifa gani iliyoonekana wazi katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza? (b) Tutachunguza maswali gani?

2 Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, likiongozwa na Yesu Kristo, lilijulikana pia kwa kufanya kazi kwa umoja. Mtume Paulo alieleza kwamba Wakristo watiwa mafuta walikuwa na “zawadi za namna mbalimbali” na walishiriki katika “huduma” na “utendaji wa namna mbalimbali,” lakini wote walikuwa sehemu ya “mwili mmoja.” (Soma 1 Wakorintho 12:4-6, 12.) Namna gani leo? Tunawezaje kuunganishwa pamoja kwa upatano tunapohubiri habari njema? Na tunawezaje kushirikiana kutanikoni na katika familia?

KUSHIRIKIANA KATIKA HUDUMA

3. Yohana alipokea maono gani?

3 Mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana aliwaona malaika saba katika maono, na kila mmoja wao alipiga tarumbeta. Malaika wa tano alipopiga tarumbeta yake, Yohana aliona “nyota” ikianguka kutoka mbinguni mpaka duniani. “Nyota” hiyo ilikuwa na ufunguo wa shimo la abiso mkononi. Baada ya kulifungua, moshi mzito ukapanda kutoka katika shimo hilo na nzige wengi wakatoka katika moshi huo. Badala ya kuharibu mimea, nzige hao wa mfano waliwavamia “wanadamu wasio na muhuri wa Mungu juu ya mapaji ya nyuso zao.” (Ufu. 9:1-4) Bila shaka, Yohana alijua jinsi nzige walivyo waharibifu; walifanya uharibifu mkubwa sana huko Misri katika siku za Musa. (Kut. 10:12-15) Nzige wa mfano ambao Yohana aliona wanafananisha Wakristo watiwa mafuta wanapotangaza ujumbe mzito wa hukumu ya Yehova. Sasa wanaungwa mkono na mamilioni ya waandamani wao wenye tumaini la kuishi duniani. Ni wazi kwamba tunapohubiri kwa umoja tunadhoofisha mamlaka ya Shetani juu ya milki yake ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo!

4. Watu wa Mungu wanapaswa kufanya kazi gani, na ni njia gani pekee ya kutimiza kazi hiyo?

4 Watu wa Yehova wana kazi kubwa sana ya kuhubiri “habari njema” duniani kote kabla ya mwisho wa mfumo huu. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kazi hiyo inahusisha kumwalika “yeyote anayeona kiu” aje anywe “maji ya uzima bure.” (Ufu. 22:17) Tukiwa washiriki wa kutaniko la Kikristo, tunawezaje kufanikiwa kufanya hivyo? Hakuna njia nyingine isipokuwa “kuunganishwa pamoja kwa upatano” na kushirikiana.—Efe. 4:16.

5, 6. Kuhubiri habari njema kunatuunganisha jinsi gani?

5 Ili kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa watu wengi iwezekanavyo, tunahitaji kufanya kazi hiyo kwa mpangilio mzuri. Hiyo ndiyo sababu tunapokea miongozo. Miongozo tunayopokea kupitia makutaniko ulimwenguni pote inatutayarisha kufanya kazi kwa umoja. Baada ya kukutana katika mkutano wa utumishi wa shambani, tunaenda kuwatangazia watu ujumbe wa Ufalme. Tunaeneza ujumbe huo kwa kuzungumza na wengine na kwa kutumia mamilioni ya nakala za machapisho yetu. Je, unajitahidi kufuata mwongozo wa kushiriki katika kampeni za pekee za kuhubiri? Unapofanya hivyo, unajiunga na mamilioni ya watu katika kutangaza ujumbe wa malaika ‘anayeruka katikati ya mbingu,’ anayetajwa kwenye Ufunuo 14:6.

6 Inasisimua sana kusoma Kitabu cha Mwaka na kuona matokeo ya utendaji wetu! Fikiria pia jinsi tunavyounganishwa tunaposambaza mialiko ya makusanyiko ya eneo, ya pekee, na ya kimataifa. Katika makusanyiko hayo, tunasikiliza hotuba za Biblia zenye kuchochea na kunufaika na drama na maonyesho. Kwa kawaida mambo hayo hukazia mwaliko wenye upendo wa Yehova wa kumtumikia kwa nafsi yote. Mwadhimisho wa kifo cha Yesu hutuunganisha pia. Kwa kuwa tunathamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu na tunatii agizo la Yesu, kila mwaka tunakusanyika kwa ajili ya tukio hilo, siku ya Nisani 14 baada ya jua kutua. (1 Kor. 11:23-26) Na watu wote wanaruhusiwa kuhudhuria, hata wale ambao si Mashahidi. Kwa majuma kadhaa kabla ya siku ya Ukumbusho, tunajitahidi kuwaalika watu wengi iwezekanavyo walio kwenye eneo letu ili wajiunge nasi katika tukio hilo muhimu.

7. Tukifanya kazi kwa umoja, tutafanikiwa kutimiza nini?

7 Nzige mmoja hana madhara makubwa. Vivyo hivyo, kwa njia fulani jitihada zetu tukiwa mtu mmojammoja zinaweza kuonekana si kitu. Lakini tukifanya kazi pamoja, tutafanikiwa kuwasaidia mamilioni ya watu wamjue yule anayestahili heshima na sifa zote, Yehova! Hata hivyo, kushirikiana katika huduma sio njia pekee ya kuchangia umoja wa watu wa Mungu.

KUSHIRIKIANA KUTANIKONI

8, 9. (a) Paulo alitumia mfano gani ili kuwafundisha Wakristo waendelee kuwa na umoja? (b) Tunaweza kushirikiana jinsi gani kutanikoni?

8 Katika barua yake kwa Waefeso, Paulo alizungumzia mpangilio wa kutaniko na uhitaji wa ‘kukua katika mambo yote.’ (Soma Waefeso 4:15, 16.) Ni nini kitakachomsaidia kila mmoja wetu kufikia lengo hilo? Akitumia mfano wa mwili wa mwanadamu, Paulo alikazia umoja wa kutaniko ambalo linaongozwa na Yesu Kristo, kichwa cha kutaniko. Alieleza kuhusu ushirikiano “kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa.” Kila mmoja wetu, iwe ni kijana au mzee, mwenye nguvu au dhaifu, anaweza kuchangiaje umoja na hali nzuri ya kiroho kutanikoni?

9 Jambo la msingi ni kujitiisha na kuwaheshimu wale ambao Yesu amewaweka watoe mwongozo kutanikoni, yaani wazee. (Ebr. 13:7, 17) Wakati mwingine si rahisi kufanya hivyo. Hata hivyo, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie. Roho yake inaweza kutusaidia tuunge mkono mipango ya kutaniko kwa moyo wote. Ikiwa wakati fulani tunahisi ni vigumu kutii mwongozo tunaopewa, tunapaswa kutafakari jinsi unyenyekevu na ushirikiano wetu unavyoweza kuchangia umoja kutanikoni. Zaidi ya hilo, kushirikiana katika mambo hayo kunaweza kutusaidia sote tukue katika upendo.

10. Watumishi wa huduma wanachangiaje umoja kutanikoni? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

10 Watumishi wa huduma wanatoa mchango mkubwa sana katika kudumisha umoja kutanikoni. Haidhuru wana umri gani, ndugu hao wanatumikia bila ubinafsi kwa manufaa ya wote. Kwa mfano, wanawasaidia wazee kwa kuhakikisha kwamba kuna machapisho ya kutosha kwa ajili ya huduma. Kwa kuongezea, mara nyingi ndugu hao wanashughulikia usafi na udumishaji wa Jumba la Ufalme, na wanawakaribisha wageni wanaohudhuria mikutano yetu. Tunaposhirikiana na ndugu hao, tunachangia hali nzuri ya kutaniko.—Linganisha na Matendo 6:3-6.

11. Vijana wanaweza kufanya nini ili kuchangia umoja katika makutaniko yao?

11 Ndugu wengi wakomavu wamelitumikia kutaniko kwa miaka mingi. Lakini huenda sasa hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya umri, hilo limefanya kuwe na marekebisho fulani ya lazima. Vijana wanaweza kusaidia sana. Ingawa hawana uzoefu, wanaweza kutimiza majukumu mengi zaidi ikiwa watazoezwa. Inapendeza sana kuona watumishi wa huduma wakitia bidii ili wastahili kuwa wazee! (1 Tim. 3:1, 10) Wazee fulani vijana wamefanya maendeleo hivi kwamba wamestahili kuwa waangalizi wa mzunguko, wakiwatumikia ndugu na dada katika makutaniko mengi. Je, unathamini kazi ambayo vijana wanafanya kwa hiari?—Soma Zaburi 110:3; Mhubiri 12:1.

KUSHIRIKIANA KATIKA FAMILIA

12, 13. Ni nini kinachoweza kuwasaidia washiriki wa familia washirikiane?

12 Acheni sasa tuzungumzie jinsi tunavyoweza kushirikiana katika familia. Wengi wamegundua kwamba kufanya Ibada ya Familia kila juma kunawasaidia kuimarisha uhusiano wao, iwe ni vijana au wazee. Ibada ya Familia huunganisha familia kwa sababu inakazia mambo ya kiroho. Kutumia wakati huo wenye kuburudisha kufanya mazoezi ya kuhubiri kunaweza kuwatayarisha washiriki wa familia kuhubiri kwa njia bora zaidi. Ni wazi kwamba washiriki wa familia wanapozungumzia Neno la Mungu pamoja, wanaimarisha uhusiano wao kwa kuwa wote wanampenda Mungu yuleyule na wanafurahia kufanya mapenzi yake.

Ibada ya Familia inaimarisha uhusiano kati ya vijana na wazee (Tazama fungu la 12 na 15)

13 Wenzi wa ndoa wanaweza kushirikiana jinsi gani ili ndoa yao imletee Yehova sifa? Wenzi wa ndoa wanaweza kufurahia umoja ikiwa wote ni watumishi waaminifu wa Yehova. Kwa mfano, Abrahamu na Sara, Isaka na Rebeka, Elkana na Hana walionyeshana upendo katika ndoa. Tunapaswa kujitahidi kufanya vivyo hivyo. (Mwa. 26:8; 1 Sam. 1:5, 8; 1 Pet. 3:5, 6) Jambo hilo litafanya wenzi wa ndoa wawe na umoja na wamkaribie zaidi Baba yao wa mbinguni.—Soma Mhubiri 4:12.

14. Ikiwa mume au mke wako hamtumikii Yehova, unaweza kufanya nini ili uimarishe ndoa yako?

14 Wakristo wanapaswa kuepuka kufungwa nira isivyo sawa na wasio waamini. (2 Kor. 6:14) Namna gani kuhusu ndugu na dada zetu wanaoishi katika familia zilizogawanyika kidini? Baadhi ya watumishi wa Mungu leo walijifunza kweli baada ya kufunga ndoa, na wanaishi na mwenzi ambaye si Shahidi. Hata katika hali hiyo, kutumia kanuni za Biblia kunaweza kuchangia umoja katika familia. Hilo linahusisha kushirikiana na mwenzi wako kadiri iwezekanavyo bila kulegeza msimamo wa Kikristo. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, lakini mara zote fikiria faida unazoweza kupata. Huenda pia ikawa vigumu kutumia kanuni za Biblia mwenzi wa ndoa anapoacha kushirikiana na kutaniko. Dada Mkristo anayeitwa Mary alikabili hali kama hiyo. Yeye na mume wake, David, walimtumikia Yehova pamoja, lakini miaka 25 hivi iliyopita mume wake aliacha kuhudhuria mikutano. Mary alijitahidi kuwa mwaminifu kwa kuhudhuria mikutano, makusanyiko, na kutumia kanuni za Biblia nyumbani na pia kuwafundisha watoto wao sita. Watoto hao walipokuwa watu wazima na kuondoka nyumbani, Mary alijihisi mpweke sana. Kisha David alianza kusoma magazeti ambayo Mary alikuwa akimletea. Baada ya muda akaanza kuhudhuria mikutano. Mjukuu wake aliyekuwa na umri wa miaka sita, alikuwa akimhifadhia kiti katika Jumba la Ufalme. Ikiwa David hangehudhuria mkutano, mjukuu wake angemwambia, “Babu, nilikukosa mkutanoni leo.” Sasa David anafurahia kumtumikia Yehova, na Mary ana shangwe kwa kuwa wanafanya hivyo pamoja.

15. Wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa wanaweza kuwasaidiaje vijana?

15 Kwa kuwa Shetani anashambulia sana familia leo, ni muhimu sana watumishi wote wa Mungu wadumishe ushirikiano mzuri katika ndoa. Hata iwe umekuwa katika ndoa kwa muda gani, fikiria kile unachoweza kusema au kufanya ili kuimarisha ndoa yako. Wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa wanaweza kuwasaidia vijana kutanikoni. Wakati mwingine wanaweza kuwaalika wenzi wa ndoa vijana katika ibada yao ya familia. Wanapokuwa na wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa, vijana wanaweza kujionea kwamba upendo na umoja ni muhimu haidhuru mtu amekaa katika ndoa kwa muda mrefu kadiri gani.—Tito 2:3-7.

“TWENDENI JUU KWENYE MLIMA WA YEHOVA”

16, 17. Watumishi wa Mungu wenye umoja wanatazamia nini?

16 Hebu wazia Waisraeli katika nyakati za Biblia wakimsifu Yehova hekaluni wakati wa sherehe huko Yerusalemu. Walihitaji kwanza kujitayarisha kwa ajili ya safari, kusaidiana walipokuwa safarini, na kisha kuabudu pamoja hekaluni. Mambo hayo yote yalihitaji ushirikiano. (Luka 2:41-44) Tunapoendelea na safari yetu ya kuelekea ulimwengu mpya, sisi pia tunahitaji kuunganishwa pamoja kwa upatano na kushirikiana. Kufanya hivyo kunahitaji jitihada za dhati. Je, kuna jambo lolote unaloweza kufanya ili uonyeshe sifa hiyo vizuri zaidi?

17 Fikiria baraka zilizo mbele yetu! Tayari tuko tofauti kabisa na mfumo huu wenye machafuko na usio na umoja. Sasa tunajionea utimizo wa mambo ambayo Isaya na Mika walitabiri, yaani watu wa Mungu wakiungana kwenda juu kwenye “mlima wa Yehova.” (Isa. 2:2-4; soma Mika 4:2-4.) Kwa kweli, ibada yetu imeinuliwa sana “katika siku za mwisho.” Na bila shaka tutafurahi na kushangilia sana tutakapoishi wakati ambapo wanadamu wote wataunganishwa pamoja kwa upatano na kushirikiana!