Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitahidi kuelewa mahitaji ya kimwili, kihisia, na ya kiroho ya ndugu na dada zako

Je, Unaweza Kusaidia Katika Kutaniko Lenu?

Je, Unaweza Kusaidia Katika Kutaniko Lenu?

KABLA ya kwenda mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Wakristo wa mapema wangewezaje kukabili changamoto hiyo?

Martin Goodman, profesa wa Chuo Kikuu cha Oxford, anasema kwamba “katika milki ya mapema ya Roma, Wakristo walikuwa tofauti na vikundi vingine vya kidini, wakiwemo Wayahudi, kwa sababu ya utume ambao walikuwa wamepewa.” Yesu alisafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine ili atimize huduma yake. Kwa kuiga mfano wake, Wakristo wa kweli walielewa kwamba kutangaza “habari njema ya ufalme wa Mungu” kunahusisha kuwatafuta watu wanaotamani kujua kweli ya Biblia. (Luka 4:43) Hiyo ni sababu moja iliyofanya makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza yawe na “mitume,” neno linalomaanisha wale waliotumwa, yaani wajumbe. (Marko 3:14) Yesu aliwaamuru wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mt. 28:18-20.

Mitume hao 12 hawapo duniani pamoja nasi leo, lakini watumishi wengi wa Yehova wanaonyesha roho ya umishonari. Wanaitikia mwaliko wa kuongeza huduma yao kwa kusema hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Baadhi yao wamehamia nchi nyingine, kama wanavyofanya maelfu ya wahitimu wa Shule ya Gileadi. Wengine wamehamia eneo tofauti katika nchi yao. Wengi wamejifunza lugha nyingine ili wajiunge na makutaniko na vikundi vinavyosaidia watu wanaozungumza lugha hiyo. Huenda ndugu na dada hao waliohamia katika maeneo yenye uhitaji au waliojifunza lugha nyingine walikabili hali fulani ngumu, na labda haikuwa rahisi kwao kushughulika na hali hiyo. Walihitaji kujidhabihu ili waonyeshe kwamba wanampenda Yehova na jirani zao. Baada ya kuhesabu gharama, walijitoa ili wasaidie. (Luka 14:28-30) Kwa kweli, msaada wa ndugu na dada hao unatimiza uhitaji mkubwa.

Hata hivyo, hali hutofautiana. Si Mashahidi wote walio na uwezo wa kuhamia katika maeneo yenye uhitaji au kujifunza lugha nyingine. Hivyo, je, tunaweza kuonyesha roho ya umishonari, hata ndani ya kutaniko letu?

UWE MMISHONARI KATIKA KUTANIKO LENU

Tumia vizuri hali yako kutimiza mahitaji ya ndugu na dada zako

Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha waziwazi roho ya umishonari, lakini inaelekea kwamba wengi wao walibaki katika miji yao ya nyumbani. Hata hivyo, maneno ambayo Paulo alimwandikia Timotheo yaliwahusu wao pia, na yanawahusu watumishi wote wa Mungu. Aliandika hivi: “Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Tim. 4:5) Amri ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme na kuwafundisha watu Biblia inawahusu Wakristo wote, haidhuru wanaishi wapi. Zaidi ya hilo, tunaweza pia kufanya mambo mengi ambayo wamishonari hufanya katika kutaniko letu.

Kwa mfano, mmishonari anapotumikia katika nchi nyingine lazima abadili maisha yake ili yapatane na hali mpya. Kwa nini? Kwa sababu mambo mengi ni tofauti kabisa katika mgawo wake mpya. Namna gani ikiwa hatuwezi kuhamia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa? Je, tukate shauri kwamba tunafahamu kila kitu kuhusu eneo la kutaniko letu, au tutajitahidi kutafuta njia mpya za kuwahubiria watu? Kwa mfano, katika miaka ya 1940, akina ndugu walitiwa moyo wapange siku moja kila juma kwa ajili ya mahubiri ya barabarani. Je, unaweza kufanya hivyo pia? Au namna gani kuhubiri kwa kutumia vigari vya machapisho? Jambo kuu ni hili: Je, umefikiria njia hizo za kuhubiri habari njema, ambazo huenda ni mpya kwako?

Watie moyo wengine wafanye kazi ya kueneza injili

Kuwa na mtazamo unaofaa kutatusaidia tuwe wenye bidii na shauku katika huduma. Katika visa vingi, wengi wa wale wanaojitolea kuhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa au kutumikia katika eneo linalozungumza lugha nyingine ni wahubiri wenye uzoefu mwingi. Hivyo wanawasaidia wengi, hasa wanapoongoza katika huduma ya shambani. Zaidi ya hilo, wamishonari husimamia mipango ya kutaniko hadi ndugu wanaostahili wanapopatikana. Ikiwa wewe ni ndugu aliyebatizwa, je, “unajitahidi” kusitawisha sifa za kustahili ili uwe tayari kuwatumikia waabudu wenzako kutanikoni?—1 Tim. 3:1.

WAIMARISHE WENGINE

Wape msaada wanaohitaji

Zaidi ya kuwa wenye bidii katika huduma ya shambani na kuwa tayari kubeba majukumu kutanikoni, tunaweza kusaidia kutaniko letu katika njia nyingine pia. Sisi sote, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, tunaweza kuwa “msaada wenye kutia nguvu” kwa waabudu wenzetu wenye uhitaji.—Kol. 4:11.

Ili tuwasaidie waabudu wenzetu, tunahitaji kuwajua vizuri. Biblia inatuhimiza “tufikiriane” tunapokusanyika pamoja. (Ebr. 10:24) Ingawa tunaepuka kujiingiza katika mambo ya kibinafsi ya wengine, maneno hayo yanatuhimiza tujitahidi kuwajua na kuwaelewa ndugu zetu na mahitaji yao. Tunaweza kuwasaidia kimwili, kihisia, au kiroho. Kuwasaidia waabudu wenzetu si jukumu la wazee na watumishi wa huduma pekee. Ni kweli kwamba katika hali fulani lingekuwa jambo linalofaa kwa akina ndugu hao kutoa msaada unaohitajika. (Gal. 6:1) Hata hivyo, sote tunaweza kuwasaidia ndugu na dada waliozeeka, au familia zinazokabili matatizo.

Wasaidie kihisia wale walio na mahangaiko ya maisha

Kwa mfano, Salvatore alipokabili tatizo la kifedha lililomlazimu auze biashara yake, nyumba, na mali nyingi za familia, hakujua familia yake ingekabilianaje na hali hiyo. Familia fulani kutanikoni ilitambua tatizo lao. Familia hiyo ilitoa msaada wa kifedha, ilimsaidia Salvatore na mke wake wapate kazi, na iliendelea kuwasikiliza na kuwatia moyo. Hilo lilifanya wawe na urafiki imara ambao umedumu kwa miaka mingi. Licha ya changamoto walizokabili, washiriki wa familia zote mbili wanafurahi sana wanapokumbuka mambo mazuri waliyofanya wakiwa pamoja.

Kwa Wakristo wa kweli, dini si jambo la siri. Kama Yesu alivyoonyesha, tunahitaji kuwasaidia watu wote wajue ahadi nzuri za Biblia. Iwe tuna uwezo wa kuhamia eneo lingine au la, tunaweza kufanya yote tuwezayo ili kuwatendea wote mema. Na bila shaka tunaweza kufanya hivyo katika kutaniko letu. (Gal. 6:10) Tukifanya hivyo, tutapata shangwe inayotokana na kutoa na tutasaidiwa kuendelea “kuzaa matunda katika kila kazi njema.”—Kol. 1:10; Mdo. 20:35.