Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Unayoweza Kufanya Ili Uishi Katika Ulimwengu Mpya

Mambo Unayoweza Kufanya Ili Uishi Katika Ulimwengu Mpya

Katika makala zilizotangulia tulijifunza kwamba hivi karibuni Mungu atawaangamiza wanadamu wote waovu na kuondoa matatizo yote. Tuna uhakika kwamba jambo hilo litatokea. Kwa nini? Kwa sababu Neno la Mungu, Biblia, limeahidi hivi:

“Ulimwengu unapitilia mbali.”​—1 YOHANA 2:17.

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba baadhi ya watu wataokolewa kwa sababu mstari huohuo unaahidi hivi:

“Yule anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”

Hivyo, ili tuweze kuokolewa tunapaswa kufanya mapenzi ya Mungu. Na ili tujue mapenzi ya Mungu, kwanza, tunahitaji kumjua vizuri.

UKIMJUA MUNGU UTAOKOLEWA MWISHO WA ULIMWENGU HUU UTAKAPOKUJA

Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Ili tuokolewe na kuishi milele, tunahitaji kumjua Mungu. Hilo linatia ndani mambo mengi zaidi ya kujua tu Mungu yupo au kujua mambo machache kumhusu. Tunahitaji kuwa marafiki wa Mungu. Ili urafiki wowote uimarike na kusitawi, tunahitaji kutumia muda pamoja na marafiki wetu. Hivyo ndivyo tunavyopaswa kufanya inapohusu urafiki wetu na Mungu. Fikiria kweli muhimu tunazojifunza kutoka katika Biblia zinazotusaidia kusitawisha na kudumisha urafiki wetu na Mungu.

SOMA NENO LA MUNGU, BIBLIA, KILA SIKU

Unaweza kuokoka mwisho wa ulimwengu huu kwa kumwomba Mungu msaada na kufanya mapenzi yake

Tunakula chakula kila siku ili tuendelee kuishi. Lakini Yesu alisema hivi: “Mwanadamu hataishi kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.”​—Mathayo 4:4.

Leo, tunapata maneno ya Yehova kwenye Biblia. Unapojifunza kitabu hiki kitakatifu, utaelewa mambo ambayo Mungu alifanya zamani, anayofanya sasa, na atakayofanya wakati ujao.

MWOMBE MUNGU MSAADA

Tunaweza kufanya nini ikiwa tunataka kufuata mwongozo wa Mungu lakini ni vigumu kwetu kuacha mambo ambayo Mungu anasema ni mabaya? Katika hali kama hiyo, kumjua Mungu vizuri kunaweza kutusaidia.

Mfikirie mwanamke tutakayemwita Sakura ambaye zamani aliishi maisha mapotovu. Alipoanza kujifunza Biblia, alijifunza kuhusu amri ya Mungu ya ‘kuukimbia uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Sakura alisali ili Mungu amsaidie na aliweza kuacha zoea hilo baya. Hata hivyo, bado anahitaji kupambana na vishawishi. Anasema hivi: “Ikiwa ninaanza kuwaza mambo mapotovu, ninasali kwa Yehova kutoka moyoni, nikijua kwamba siwezi kupambana na hali hiyo peke yangu. Kusali kumenifanya niwe karibu zaidi na Yehova.” Kama Sakura, mamilioni ya watu wanaendelea kupata ujuzi kumhusu Mungu. Anawapa nguvu wanazohitaji ili wafanye mabadiliko katika maisha yao na kuishi kwa njia inayompendeza Yeye.​—Wafilipi 4:13.

Kadiri unavyoendelea kumjua Mungu vizuri, ndivyo atakavyokujua wewe kama rafiki yake mpendwa. (Wagalatia 4:9; Zaburi 25:14) Kisha, utaweza kuokolewa na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Lakini, ulimwengu mpya utakuwaje? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa kwenye Biblia.