Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Alisema Mwisho Utakuja Lini?

Yesu Alisema Mwisho Utakuja Lini?

Kama tulivyojifunza kwenye makala iliyopita, Biblia inapozungumzia mwisho wa ulimwengu haimaanishi mwisho wa sayari yetu dunia au wa wanadamu. Badala yake, inamaanisha mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo na wale wote wanaouunga mkono. Hata hivyo, Biblia inasema mwisho utakuja lini?

FIKIRIA MAMBO MAWILI AMBAYO YESU ALISEMA KUHUSU MWISHO:

“Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ile siku wala saa.”​—MATHAYO 25:13.

“Endeleeni kutazama, endeleeni kukaa macho, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni lini.”​—MARKO 13:33.

Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote duniani anayejua kihususa mwisho utakuja lini. Lakini, Mungu ameweka wakati hususa, yaani, “siku na saa” ya mwisho wa ulimwengu. (Mathayo 24:36) Je, hilo linamaanisha hakuna kabisa njia yoyote ya kujua ikiwa mwisho uko karibu? La hasha. Yesu aliwaambia wanafunzi wake wawe macho kuona baadhi ya matukio ambayo yangeashiria kuwa mwisho uko karibu.

ISHARA

Yesu alitaja matukio ambayo yangekuwa ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema hivi: “Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.” (Mathayo 24:3, 7) Pia, alisema kutakuwa na “magonjwa,” yaani, magonjwa yanayosambaa kwa kasi. (Luka 21:11) Je, unajionea mambo hayo ambayo Yesu alitabiri?

Leo, watu wanateseka sana kwa sababu ya vita, njaa, matetemeko ya ardhi, na magonjwa mbalimbali. Kwa mfano, mwaka wa 2004, tetemeko kubwa la ardhi lililotokea kwenye bahari ya Hindi lilisababisha tsunami iliyoua watu 225,000 hivi. Katika kipindi cha miaka mitatu, ugonjwa wa corona (COVID-19) umesababisha vifo vya watu milioni 6.9 hivi duniani pote. Yesu alisema matukio kama hayo yangeonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu uko karibu.

“SIKU ZA MWISHO”

Biblia inakiita “siku za mwisho,” kipindi kifupi cha wakati kabla ya mwisho wa ulimwengu. (2 Petro 3:3, 4) Timotheo ya pili 3:1-5 inasema kwamba siku za mwisho zingetambuliwa kwa kuporomoka kwa maadili. (Ona sanduku lenye kichwa; “ Kabla ya Mwisho wa Ulimwengu.”) Je, unajionea watu wakiwa wabinafsi, wenye pupa, wakali, na wasio na upendo? Jambo hilo pia ni uthibitisho kwamba tunaishi karibu zaidi na mwisho wa ulimwengu.

Siku za mwisho zitadumu kwa muda gani? Kulingana na Biblia, kitakuwa “kipindi kifupi cha wakati.” Kisha, Mungu atawaharibu “wale wanaoiharibu dunia.”​—Ufunuo 11:15-18; 12:12.

DUNIA PARADISO IKO KARIBU!

Tayari Mungu ameweka siku na saa ya kuuangamiza mfumo huu mwovu wa mambo. (Mathayo 24:36) Hata hivyo, kuna habari nyingine njema—Mungu “hataki yeyote aangamizwe.” (2 Petro 3:9) Kwa sasa, anawapa wanadamu nafasi ya kuishi kulingana na viwango vyake. Kwa nini? Kwa sababu anataka tuokoke mwisho wa ulimwengu huu na kuishi katika dunia itakayokuwa paradiso.

Mungu amepanga programu ya elimu ya Biblia ulimwenguni pote inayowasaidia watu kujua mambo ya kufanya ili waishi katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wake. Yesu alisema habari njema ya Ufalme wa Mungu ingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walitumia mabilioni ya saa kuwahubiria na kuwafundisha watu ujumbe wa tumaini wa Biblia. Yesu alisema kwamba kazi hii ya kuhubiri ingefanywa duniani kote kabla ya mwisho kuja.

Muda wa utawala wa wanadamu unakaribia kwisha. Lakini habari njema ni kwamba, unaweza kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kuishi katika dunia Paradiso ambayo Mungu ameahidi. Makala inayofuata itazungumzia mambo unayoweza kufanya ili uishi katika ulimwengu huo mpya.

Unabii wa Yesu kuhusu “siku za mwisho” unatupatia sababu ya kuwa na tumaini