Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | WAPANDA FARASI WANNE​—JINSI WANAVYOKUHUSU

Wapanda Farasi Wanne​Jinsi Wanavyokuhusu

Wapanda Farasi Wanne​Jinsi Wanavyokuhusu

Wanakimbia kwa kishindo kikubwa! Wapanda farasi wanne na farasi zao hufanyiza picha iliyo wazi sana akilini ambayo huvuta uangalifu katika Biblia! Farasi wa kwanza ni mweupe, mpanda farasi wake ni mfalme mwenye utukufu aliyewekwa rasmi hivi karibuni. Anafuatwa na farasi wa rangi ya moto, na mpandaji wake anaondoa amani duniani kote. Farasi wa tatu ni mweusi kama giza, na aliyeketi juu yake amebeba mizani, ishara ya upungufu wa chakula. Farasi wa nne ni wa rangi ya kijivu, akiashiria magonjwa na mambo mengine yanayosababisha vifo, mpandaji wake ni Kifo chenyewe. Nalo Kaburi, linafuata kwa ukaribu, likivuna idadi kubwa ya watu!—Ufunuo 6:1-8.

“Mwanzoni niliogopa sana niliposoma simulizi la wapanda farasi wanne. Nilihisi kwamba Siku ya Hukumu iko karibu sana na singeokoka kwa sababu sikuwa nimejitayarisha.”—Crystal.

“Nilivutiwa sana na wapanda farasi hao wanne walioketi juu ya farasi wenye rangi tofauti-tofauti. Nilipojua maana ya maono hayo, nilielewa kwa nini wapanda farasi hao wanaelezwa kwa njia hiyo.”—Ed

Je, unahisi kama Crystal kuhusu wapanda farasi wanne wa Apokalipsi? Au una maoni kama ya Ed? Vyovyote vile, mbio za wapanda farasi wanne ndilo simulizi linalojulikana sana katika kitabu cha mwisho cha Biblia cha Ufunuo. Je, unajua kwamba utafaidika kwa kuelewa maono hayo? Jinsi gani? Mungu anaahidi kwamba unaweza kuwa na furaha ya kweli kwa kusoma, kujifunza na kuishi kupatana na mambo yaliyoandikwa katika kitabu hicho cha kinabii.—Ufunuo 1:1-3.

Ingawa baadhi ya watu huogopa maono hayo ya wapanda farasi wanne, hayakukusudiwa kukuogopesha. Kwa kupendeza, mamilioni ya watu wametambua kwamba maono hayo yanaimarisha imani na kuwapa tumaini zuri la wakati ujao. Inaweza kuwa hivyo kwako pia. Tafadhali chunguza makala inayofuata.