Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Kifo cha Mwenzi Wako wa Ndoa

Kukabiliana na Kifo cha Mwenzi Wako wa Ndoa

BIBLIA inasema hivi waziwazi: Mume anapaswa ‘kumpenda mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.’ Mke pia anapaswa “kumheshimu sana mume wake.” Wanapaswa kutimiza majukumu yao wakiwa “mwili mmoja.” (Efe. 5:33; Mwa. 2:23, 24) Baada ya muda, uhusiano wao na upendo wao unazidi kuimarika. Uhusiano huo unaweza kufananishwa na mizizi ya miti miwili inayokua pamoja. Hisia za wenzi hao wa ndoa wenye furaha hufungamana kama mizizi ya miti hiyo.

Hata hivyo, inakuwaje mume au mke akifa? Basi, kifungo chao cha maisha huvunjika. Mara nyingi mwenzi anayebaki akiwa mjane huachwa akiwa amevunjika moyo, mpweke, na huenda akawa mwenye hasira au kuhisi kuwa ana hatia. Daniella, aliyekuwa amefunga ndoa kwa miaka 58, alijua watu wengi waliofiwa na wenzi wao wa ndoa. * Hata hivyo, baada ya mume wake kufa, alisema hivi: “Sikuelewa jinsi mtu anavyohisi anapofiwa. Mtu hawezi kuelewa hali hiyo mpaka inapompata.”

MAUMIVU YA MUDA MREFU

Watafiti fulani husema kwamba hakuna mkazo unaozidi mkazo wa kufiwa na mwenzi unayempenda. Wengi waliofiwa na wenzi wao wanakubaliana na hilo. Mume wa Millie alikufa miaka mingi iliyopita. Akizungumzia maisha yake akiwa mjane, anasema hivi: “Ninajiona kuwa  mlemavu.” Alikuwa akirejelea hali yake ya kihisia baada ya kufiwa na mwenzi wake wa ndoa aliyeishi naye kwa miaka 25.

Susan alifikiri kwamba wajane walioomboleza kwa miaka mingi baada ya kufiwa na waume zao walionyesha huzuni kupita kiasi. Kisha, mume aliyeishi naye kwa miaka 38 akafa. Ingawa miaka zaidi ya 20 imepita, Susan anasema hivi: “Mimi humfikiria kila siku.” Susan hutokwa na machozi kwa kuwa anamkosa sana.

Biblia inakubali kwamba mtu hupata uchungu mkali sana na wa muda mrefu anapofiwa na mwenzi wake wa ndoa. Sara alipokufa, Abrahamu, mume wake, ‘aliingia ndani kumwombolezea Sara na kumlilia.’ (Mwa. 23:1, 2) Ingawa aliamini ufufuo, Abrahamu alihuzunika sana mpendwa wake alipokufa. (Ebr. 11:17-19) Yakobo hakumsahau haraka mke wake mpendwa Raheli alipokufa. Alimsifu alipozungumza na wanawe kumhusu.—Mwa. 44:27; 48:7.

Tunapaswa kujifunza nini kutokana na mifano hiyo ya Kimaandiko? Mara nyingi, wajane huhisi uchungu wanapofiwa na mwenzi wa ndoa waliyeishi naye kwa miaka mingi. Tunapaswa kuelewa kwamba kulia na kuhuzunika baada ya kufiwa na mwenzi wa ndoa ni hali ya kawaida, wala si udhaifu. Huenda tukahitaji kuwaonyesha hisia-mwenzi na kuwategemeza kwa muda mrefu.

KUKABILIANA NA HALI SIKU BAADA YA SIKU

Kuwa mjane ni tofauti na kuwa mseja. Baada ya kukaa katika ndoa kwa miaka mingi, mara nyingi mume hujua jinsi ya kumfariji na kumtia moyo mke wake anaposhuka moyo au kuvunjika moyo. Mume anapokufa, mke hukosa upendo na faraja. Vivyo hivyo, mke humfurahisha mume wake na kumfanya ahisi akiwa salama. Mume huthamini sana anapoguswa kwa upendo na mke wake na kuambiwa maneno yenye kutuliza, naye huthamini mke wake anapomjali na kutosheleza mahitaji yake. Mke akifa, huenda mume akahisi upweke maishani. Hivyo, wale waliofiwa na wenzi wa ndoa wana hofu na shaka kuhusu wakati ujao. Ni kanuni gani ya Biblia inayoweza kuwasaidia kuwa na amani na utulivu?

Ukifiwa na mwenzi wako, Mungu atakusaidia kuvumilia hali hiyo siku baada ya siku

“Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.” (Mt. 6:34) Maneno hayo ya Yesu yanahusu hasa mahitaji ya kimwili, hata hivyo, yamewasaidia wengi kuvumilia baada ya kufiwa na mpendwa wao. Charles aliandika hivi miezi kadhaa baada ya mke wake kufa: “Bado ninamkosa sana Monique, na nyakati nyingine ninamkosa hata zaidi. Hata hivyo, nilitambua kwamba ni kawaida kuhisi hivyo, na hatimaye maumivu yangu yatapungua baada ya muda.”

Charles alivumilia ‘kwa muda.’ Aliwezaje? Alisema hivi: “Yehova alinisaidia kuvumilia hali hiyo siku baada ya siku.” Charles hakulemewa na huzuni. Maumivu yake hayakuisha mara moja wala hayakumlemea. Ikiwa umefiwa na mwenzi wako wa ndoa, jitahidi kukabiliana na hali hiyo siku baada ya siku. Utapata manufaa au kitia-moyo pole kwa pole.

 Kifo hakikuwa sehemu ya kusudi la awali la Yehova. Badala yake ni mojawapo ya “kazi za Ibilisi.” (1 Yoh. 3:8; Rom. 6:23) Shetani anatumia kifo na woga wa kifo kuwafanya watu kuwa watumwa na kukosa tumaini. (Ebr. 2:14, 15) Shetani anafurahi mtu anapokata tamaa na kuhisi kwamba hawezi kuwa na furaha ya kweli na uradhi, hata katika ulimwengu mpya wa Mungu. Hivyo, dhambi ya Adamu na hila za Shetani ndizo zinazomfanya mjane ateseke kihisia baada ya kufiwa na mwenzi wake. (Rom. 5:12) Yehova atarekebisha kabisa hali iliyosababishwa na Shetani kwa kuondoa kifo, silaha ya kikatili anayotumia. Wale watakaowekwa huru au kuokolewa kutokana na kifo wanatia ndani wengi waliofiwa na mwenzi wa ndoa kama wewe.

Ni wazi kwamba kutakuwa na mabadiliko mengi katika mahusiano ya wanadamu baada ya wafu kufufuliwa duniani. Wazia wazazi, babu na nyanya, na mababu wengine watakaofufuliwa na kuishi na watoto na wajukuu wao kufikia hali ya ukamilifu. Madhara ya kuzeeka yataondolewa. Je, huenda vijana watahitaji kujifunza kuwaona mababu zao kwa njia tofauti na leo? Na je, hatuamini kwamba mabadiliko hayo yataboresha pia familia ya wanadamu?

Kuna maswali mengi kuhusu watakaofufuliwa, hasa kuhusu wale waliofiwa na wenzi wawili au zaidi. Masadukayo waliuliza swali kuhusu mwanamke aliyefiwa na mume wake wa kwanza, kisha wa pili, hadi wa saba. (Luka 20:27-33) Wenzi hao watakuwa na uhusiano gani baada ya  ufufuo? Kwa kweli hatujui, na hakuna haja ya kukisia-kisia au kuhangaika kwa sababu ya mambo tusiyojua. Kwa sasa, ni lazima tumtegemee Mungu. Hata hivyo, jambo moja ni hakika, lolote atakalofanya Yehova wakati ujao litafaa, nalo litakuwa lenye kutamanika wala si kuogopesha.

TUMAINI LA UFUFUO HUFARIJI

Fundisho la kwamba wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa ni mojawapo ya mafundisho yaliyo wazi zaidi katika Neno la Mungu. Masimulizi ya Biblia kuhusu watu waliofufuliwa yanatuhakikishia kwamba ‘wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti ya Yesu na kutoka.’ (Yoh. 5:28, 29) Wale watakaokuwa hai wakati huo watafurahi kukutana na watu waliowekwa huru kutokana na kifo. Kwa upande mwingine, hatuwezi kuwazia kamwe shangwe watakayokuwa nayo wale watakaofufuliwa.

Wafu wanapofufuliwa, dunia itajawa na shangwe ambayo haijawahi kuonekana. Mabilioni ya wanadamu waliokufa wataishi tena. (Marko 5:39-42; Ufu. 20:13) Kutafakari kuhusu muujiza huo wa wakati ujao kunapaswa kuwafariji wote waliofiwa na wapendwa wao.

Je, kuna yeyote atakayekuwa na sababu ya kuhuzunika wakati wa ufufuo? Biblia inaonyesha kwamba hakuna yeyote atakayehuzunika. Andiko la Isaya 25:8 linasema kwamba Yehova “kwa kweli atameza kifo milele.” Hilo linatia ndani maumivu yanayosababishwa na kifo, kwa kuwa unabii huo unaendelea kusema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” Ikiwa unahuzunika kwa sababu umefiwa na mwenzi wako wa maisha, bila shaka, ufufuo utakupa sababu ya kufurahi.

Hakuna mwanadamu anayeelewa kikamili yote atakayotimiza Mungu katika ulimwengu mpya. Yehova anasema hivi: “Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isa. 55:9) Ahadi ya Yesu kuhusu ufufuo inatupatia nafasi ya kumtegemea  Yehova kama alivyofanya Abrahamu. Ni jambo muhimu kwa kila Mkristo kumtii Mungu sasa ili ‘ahesabiwe kuwa anastahili kuupata mfumo ule wa mambo’ pamoja na watakaofufuliwa.—Luka 20:35.

SABABU YA KUWA NA TUMAINI

Uwe na tumaini badala ya kuwa na wasiwasi. Kwa maoni ya wanadamu, hakuna tumaini la wakati ujao. Hata hivyo, Yehova anatupatia tumaini bora. Hatujui kikamili jinsi Yehova atakavyotosheleza tamaa na mahitaji yetu yote, hata hivyo, tuna hakika kwamba atatimiza ahadi yake. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tumaini linaloonekana si tumaini, kwa maana mtu anapoona kitu, je, yeye hukitumainia? Lakini tukitumainia kile ambacho hatuoni, sisi huendelea kukingojea kwa uvumilivu.” (Rom. 8:24, 25) Kuwa na tumaini thabiti kuelekea ahadi za Mungu kutakusaidia kuvumilia. Ukivumilia, utaishi wakati ambapo Yehova “atakupa maombi ya moyo wako.” Atatosheleza “tamaa ya kila kitu kilicho hai.”—Zab. 37:4; 145:16; Luka 21:19.

Tegemea ahadi ya Yehova ya wakati ujao wenye shangwe nyingi

Mitume walifadhaika sana Yesu alipokuwa karibu kuuawa. Yesu aliwafariji kwa kuwaambia hivi: “Mioyo yenu isitaabike. Iweni na imani katika Mungu, iweni na imani pia katika mimi.” Akaendelea kuwaambia: “Sitawaacha ninyi mayatima. Ninakuja kwenu.” (Yoh. 14:1-4, 18, 27) Maneno hayo yangewapa wafuasi wake watiwa-mafuta msingi wa kuwa na tumaini na uvumilivu kwa karne nyingi. Pia, wale wanaotamani kuwaona wapendwa wao wakati wa ufufuo hawana sababu ya kukata tamaa. Yehova na Mwana wake hawatawaacha wakiwa wajane. Unaweza kuwa na hakika kuhusu hilo!

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.