Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Afrika Magharibi

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Afrika Magharibi

PASCAL, aliyelelewa katika kijiji cha watu maskini nchini Côte d’Ivoire, alitamani sana kuishi maisha bora. Akiwa mwanandondi asiye na uzoefu, alijiuliza hivi: ‘Nitafanya nini ili niwe mashuhuri na kuwa tajiri?’ Alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, aliamua kuhamia Ulaya ili atimize mradi wake. Lakini alitaka kuingia Ulaya kwa njia isiyo halali kwa sababu hakuwa na hati za kusafiri.

Katika mwaka wa 1998, akiwa na umri wa miaka 27, Pascal alianza safari yake. Alivuka mpaka na kuingia nchini Ghana, akasafiri hadi Togo na kuingia Benin, na hatimaye akafika kwenye mji wa Birni Nkonni huko Niger. Sehemu iliyobaki ya safari yake ilikuwa hatari zaidi. Ili kufika upande wa kaskazini, angehitaji kusafiri kwa lori na kuvuka Jangwa la Sahara. Kisha, angehitaji kusafiri kwa mashua hadi Ulaya kupitia bahari ya Mediterania. Huo ndio uliokuwa mpango wake, lakini mambo mawili yalimzuia kuondoka nchini Niger.

Kwanza, pesa zake ziliisha. Pili, alikutana na Noé, painia aliyeanza kumfundisha Biblia. Mambo aliyojifunza yalimgusa moyo sana na kumfanya abadili maoni yake kuhusu maisha. Alianza kufuatilia miradi ya kiroho badala ya miradi ya kimwili. Pascal alibatizwa mnamo Desemba 1999. Ili kumshukuru Yehova, alianza kutumikia akiwa painia mwaka wa 2001 nchini Niger, katika mji alikojifunzia kweli. Anahisije kuhusu utumishi wake? Anasema hivi kwa uchangamfu: “Sasa nina maisha bora kabisa!”

KUISHI MAISHA BORA BARANI AFRIKA

Anne-Rakel

Kama Pascal, wengi wametambua kwamba kufuatilia miradi ya kiroho huleta uradhi zaidi maishani. Ili kufikia miradi hiyo, wengine wamehamia Afrika kutoka Ulaya ili kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Kwa kweli, Mashahidi 65 hivi kutoka Ulaya walio na umri wa kati ya miaka 17 na 70 wamehamia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri huko Afrika Magharibi katika nchi ya Benin, Burkina Faso, Niger, na Togo. * Ni nini kilichowachochea kufanya uamuzi huo mzito, na matokeo yamekuwa nini?

Anne-Rakel kutoka Denmark anasimulia hivi: “Wazazi wangu walikuwa wamishonari nchini Senegal. Kila mara walisimulia kwa msisimuko kuhusu maisha ya umishonari hivi kwamba nikatamani kuwa na maisha kama hayo.” Miaka 15 hivi iliyopita, Anne-Rakel alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi alihamia Togo anakotumikia katika kutaniko la lugha ya ishara. Kufanya hivyo kumewachocheaje wengine? Anasema hivi: “Baadaye ndugu na dada yangu mdogo walijiunga nami nchini Togo.”

Albert-Fayette na Aurele

 Aurele, ndugu aliyeoa mwenye umri wa miaka 70 kutoka Ufaransa anasema hivi: “Nilipostaafu miaka mitano iliyopita, nilihitaji kuamua ama kuishi maisha matulivu nchini Ufaransa nikisubiri Paradiso au kupanua huduma yangu.” Aurele aliamua kupanua huduma yake. Miaka mitatu hivi iliyopita, yeye na mke wake, Albert-Fayette, walihamia Benin. Aurele anasema hivi: “Kujitolea kumtumikia Yehova katika eneo hili ndio uamuzi bora zaidi tuliowahi kufanya.” Anaongezea hivi huku akitabasamu: “Sehemu fulani za pwani tunazohubiri zinanikumbusha kuhusu Paradiso.”

Clodomir na mke wake, Lysiane, walihamia Benin kutoka Ufaransa miaka 16 iliyopita. Mwanzoni, walitamani sana kurudi Ufaransa ili kuona familia na marafiki wao, na walikuwa na wasiwasi kwamba hawangeweza kuishi Benin. Hata hivyo, hawakuwa na sababu ya kuwa na wasiwasi. Walipata shangwe nyingi. Clodomir anasema hivi: “Kwa miaka 16, tumekuwa na pendeleo la kumsaidia angalau mtu mmoja kila mwaka kukubali kweli.”

Lysiane na Clodomir wakiwa na baadhi ya watu waliowasaidia kujifunza kweli

Johanna na Sébastien

Sébastien na Johanna, wenzi wa ndoa kutoka Ufaransa walihamia Benin mwaka wa 2010. Sébastien anasema hivi: “Kuna mengi sana ya kufanya kutanikoni. Ni kama tunazoezwa mambo mengi sana ya kitheokrasi kwa muda mfupi!” Watu wanaitikiaje katika huduma? Johanna anasema hivi: “Watu wana kiu ya kujifunza kweli. Hata tunapokuwa katika shughuli zetu za kibinafsi, watu hutusimamisha njiani na kuuliza maswali ya Biblia na kuchukua machapisho yetu.” Kuhama kumeisaidiaje ndoa yao? Sébastien anasema hivi: “Kumeimarisha ndoa yetu. Ninafurahia sana kuhubiri siku nzima na mke wangu.”

Eric na mke wake, Katy, wanafanya upainia katika eneo lenye watu wachache kaskazini mwa Benin. Walipoishi Ufaransa miaka kumi hivi iliyopita, walianza kusoma makala kuhusu kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi na kuzungumza na watumishi wa wakati wote. Hilo liliwachochea kuhamia nchi nyingine katika mwaka wa 2005. Walitiwa moyo sana walipoona ongezeko. Eric anasema hivi: “Miaka miwili iliyopita, kikundi chetu katika mji wa Tanguiéta kilikuwa na wahubiri 9; sasa wamefika 30. Watu 50 hadi 80 huhudhuria mikutano siku ya Jumapili. Ni shangwe iliyoje kuona ongezeko hilo kubwa!”

Katya na Eric

 TAMBUA NA USHINDE CHANGAMOTO

Benjamin

Baadhi ya ndugu na dada waliohamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri walikabili changamoto gani? Benjamin, mwenye umri wa miaka 33, ni kaka ya Anne-Rakel. Alipokuwa nchini Denmark mwaka wa 2000, alikutana na mmishonari aliyetumika nchini Togo. Benjamin anakumbuka hivi: “Nilipomwambia mmishonari huyo kwamba nilitaka kuwa painia, alisema: ‘Unaweza kuwa painia nchini Togo.’” Benjamin alifikiria jambo hilo. Anasema: “Wakati huo, sikuwa nimefikisha umri wa miaka 20, lakini dada zangu wawili tayari walikuwa wakitumika nchini Togo. Basi, ilikuwa rahisi zaidi kwangu kuhamia huko.” Kwa hiyo, akahama. Hata hivyo, alikabili changamoto fulani. Benjamin anasema hivi: “Sikujua neno hata moja la Kifaransa. Hali ilikuwa ngumu miezi sita ya kwanza kwa sababu sikuweza kuwasiliana na watu.” Hata hivyo, baadaye alifanya maendeleo. Benjamin sasa anafanya kazi katika Betheli ya Benin, akisaidia katika idara ya kompyuta na kusafirisha machapisho.

Marie-Agnès na Michel

Eric na Katy, waliotajwa mwanzoni walitumika katika eneo la lugha ya kigeni nchini Ufaransa kabla ya kuhamia Benin. Afrika Magharibi ilitofautianaje na Ufaransa? Katy anasema: “Haikuwa rahisi kupata nyumba nzuri. Kwa miezi kadhaa, tuliishi katika nyumba isiyokuwa na umeme wala maji ya bomba.” Eric anaongezea hivi: “Majirani walipiga muziki kwa sauti ya juu hadi usiku wa manane. Unahitaji subira na kuwa tayari kuishi katika mazingira ya aina hiyo.” Wote wanakiri hivi: “Shangwe ya kutumikia katika eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida haiwezi kamwe kulinganishwa na matatizo yoyote yale.”

Michel na Marie-Agnès, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka karibu 60 kutoka Ufaransa walihamia Benin miaka mitano hivi iliyopita. Mwanzoni walikuwa na wasiwasi. Michel anasema hivi: “Baadhi ya watu walisema ni kana kwamba tuliketi kwenye toroli iliyosukumwa na mwanasarakasi juu ya kamba! Hatukuogopa kwa sababu tulijua kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akisukuma toroli hiyo. Kwa hiyo, tulihama kwa sababu ya Yehova na kwa ajili yake.”

JINSI YA KUJITAYARISHA

Wale walio na uzoefu wa kuhubiri maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wanasema kwamba ni muhimu sana kujitayarisha kwa njia zifuatazo: Panga mapema. Jifunze kuishi chini ya hali mbalimbali. Usinunue vitu ambavyo hujapanga kuvinunua. Mtegemee Yehova.—Luka 14:28-30.

Sébastien, aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Kabla ya kuhama, mimi na Johanna tuliweka pesa akibani kwa miaka miwili. Hatukutumia pesa nyingi kwa ajili ya burudani wala hatukununua vitu tusivyohitaji.” Wanafanya kazi barani Ulaya kwa miezi michache kila mwaka ili waweze kuendelea na upainia nchini Benin kwa miezi inayosalia.

Marie-Thérèse

 Marie-Thérèse ni kati ya dada waseja 20 hivi kutoka nchi nyingine wanaotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri huko Afrika Magharibi. Alikuwa dereva wa basi nchini Ufaransa; hata hivyo, katika mwaka wa 2006 alichukua likizo ya mwaka mmoja ili afanye upainia nchini Niger. Baada ya muda mfupi, aligundua kwamba hayo ndiyo maisha aliyotamani sana. Marie-Thérèse anasema: “Baada ya kurudi Ufaransa, nilimwomba mwajiri wangu abadili ratiba yangu ya kazi, akakubali kuibadili. Kwa sasa, kuanzia Mei hadi Agosti, ninafanya kazi ya kuendesha basi nchini Ufaransa, kisha kuanzia Septemba hadi Aprili ninafanya upainia nchini Niger.”

Saphira

Wale ‘wanaoutafuta kwanza Ufalme’ wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawaandalia “vitu vingine vyote” vya lazima. (Mt. 6:33) Kwa mfano: Fikiria kisa cha Saphira, dada mseja kutoka Ufaransa mwenye umri wa miaka karibu 30 anayefanya upainia nchini Benin. Alirudi Ufaransa mwaka wa 2011 kufanya kazi ili aweze kujitegemeza kwa mwaka mwingine (mwaka wake wa sita) barani Afrika. Saphira anasema hivi: “Siku yangu ya mwisho kazini ilikuwa Ijumaa, lakini bado nilihitaji kufanya kazi siku kumi zaidi ili nipate pesa za kutosha kunitegemeza kwa mwaka mzima. Nilipaswa kuondoka Ufaransa baada ya majuma mawili tu. Nikasali kwa Yehova kuhusu hali yangu. Baada ya muda mfupi, kampuni inayowaajiri watu ilinipigia simu na kuniuliza ikiwa ningependa kumshikia mtu fulani kazi kwa majuma mawili.” Siku ya Jumatatu, Saphira alienda kuzoezwa na mfanyakazi aliyepaswa kumshikia kazi kwa majuma hayo mawili. Anasema: “Nilishangaa nilipojua kwamba ni dada Mkristo aliyehitaji likizo ya siku kumi ili ahudhurie Shule ya Utumishi wa Painia. Mwajiri wake alimwambia kwamba hangempa likizo ikiwa hawangepata mtu wa kufanya kazi yake. Dada huyo alimsihi sana Yehova amsaidie, kama nilivyokuwa nimefanya.”

CHANZO CHA URADHI WA KWELI

Baadhi ya ndugu na dada wamehamia Afrika Magharibi na kuishi huko kwa miaka mingi. Wengine wametumika huko kwa miaka michache na kurudi katika nchi zao. Hata hivyo, bado wahubiri hao waliotumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wananufaika na mambo waliyojifunza walipotumika katika maeneo hayo. Walijifunza kwamba kumtumikia Yehova huleta uradhi wa kweli maishani.

^ fu. 6 Ofisi ya tawi ya Benin husimamia kazi katika nchi hizo nne zinazotumia lugha ya Kifaransa.