Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Iweni Waigaji wa Mungu”

“Iweni Waigaji wa Mungu”

Mkaribie Mungu

“Iweni Waigaji wa Mungu”

Waefeso 4:32–5:2

FADHILI. Huruma. Msamaha. Upendo. Inasikitisha kwamba watu wengi hawaonyeshi sifa hizo leo. Namna gani wewe? Je, umewahi kuhisi kwamba jitihada zako za kukuza sifa hizo nzuri hazitafanikiwa? Huenda tamaa yako ya kufanya mambo kwa ukamilifu ikafanya iwe vigumu kukuza tabia nzuri kwa sababu ya tabia mbaya zilizokita mizizi au mambo yanayoumiza yaliyowahi kukupata wakati uliopita. Hata hivyo, Biblia inatufundisha ukweli huu wenye kufariji, kwamba Muumba wetu anajua tuna uwezo wa kukuza sifa nzuri.

Neno la Mungu linawahimiza hivi Wakristo wa kweli: “Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba Mungu ana imani na waabudu wake. Jinsi gani? Yehova Mungu alimuumba mwanadamu kwa mfano Wake, kulingana na sura Yake. (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo, Mungu amewapa wanadamu sifa zinazofanana na zake. * Kwa hiyo, Biblia inapowahimiza Wakristo ‘wawe waigaji wa Mungu,’ ni kana kwamba Yehova mwenyewe anawaambia: ‘Nina imani na nyinyi. Ninajua kwamba licha ya kutokamilika kwenu mnaweza kuwa kama mimi kwa kadiri fulani.’

Ni sifa gani za Mungu tunazoweza kuiga? Mistari inayozunguka andiko hilo inajibu. Ona kwamba Paulo alianza himizo la kumwiga Mungu kwa maneno “kwa hiyo.” Maneno hayo yanaunganisha mstari huo na ule unaotangulia, unaotaja fadhili, huruma nyororo, na msamaha. (Waefeso 4:32; 5:1) Kisha katika mstari unaofuata shauri hilo la kumwiga Mungu, Paulo anawaambia Wakristo waishi maisha yanayoonyesha kwamba wanawapenda watu bila ubinafsi. (Waefeso 5:2) Kwa kweli, Yehova Mungu ndiye mfano bora wa kuonyesha fadhili, huruma nyororo, kusamehe wengine kwa hiari, na kuonyesha upendo.

Kwa nini tutake kuwa kama Mungu? Ona jinsi Paulo anavyotuchochea: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” Je, hilo halitugusi moyo? Yehova anawaona waabudu wake kuwa watoto anaowapenda sana. Kama vile mvulana mdogo anavyojaribu kuwa kama baba yake, ndivyo Wakristo wa kweli wanavyojitahidi kuwa kama Baba yao wa mbinguni.

Yehova hawalazimishi wanadamu wamwige. Tofauti na hilo, ametupa uhuru wa kuchagua. Kwa hiyo, wewe mwenyewe utaamua ikiwa utamwiga au la. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Usisahau kamwe kwamba una uwezo wa kuonyesha sifa kama za Mungu. Bila shaka, ili umwige Mungu ni lazima kwanza ujifunze sifa na njia zake. Biblia inaweza kukusaidia kujifunza mambo yote kuhusu sifa na njia za Mungu, ambaye utu wake usio na kifani umewavuta mamilioni ya watu kumwiga.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Andiko la Wakolosai 3:9, 10 linaonyesha kwamba kuumbwa katika mfano wa Mungu kunahusiana na kuwa na utu wake. Wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanahimizwa wajivike “utu mpya” ambao “unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule [Mungu] aliyeuumba.”