Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Matatizo Tunayopata Ni Adhabu Kutoka kwa Mungu?

Je, Matatizo Tunayopata Ni Adhabu Kutoka kwa Mungu?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Matatizo Tunayopata Ni Adhabu Kutoka kwa Mungu?

Je, umewahi kupatwa na tatizo maishani ambalo lilikufanya ujiulize ikiwa Mungu anataka uteseke? Ugonjwa wa ghafula, aksidenti mbaya, au kifo cha mtu wa familia ni mambo yanayoweza kutufanya tuhisi ni kama Mungu anatuadhibu.

Badala ya kufikiri hivyo, unapaswa kufarijika kujua kwamba Mungu anataka watu wawe na furaha na bila matatizo. Tunaona hilo tunapofikiria kwamba Mungu alipowaumba wanadamu wawili wa kwanza, aliwaweka katika “bustani ya Edeni,” shamba la kiparadiso, ambamo wangeishi bila matatizo yoyote.—Mwanzo 2:15.

Kwa kusikitisha, wenzi hao wawili wa kwanza walikataa taraja hilo zuri nao wakakataa kumtii Mungu kimakusudi. Matokeo yalikuwa mabaya si kwao tu bali pia kwa wazao wao wote, kutia ndani sisi. Kwa nini? Hali hiyo inaweza kulinganishwa na kinachotokea wakati kichwa cha familia anapokataa kulipa kodi ya nyumba—familia yote hufukuzwa kutoka katika nyumba yao na kupatwa na matatizo na kuanza kupungukiwa. Kwa njia hiyohiyo, wanadamu wamepatwa na matatizo tangu uasi huo wa kwanza. (Waroma 5:12) Miaka mingi baadaye, mwanamume mwadilifu Ayubu alisema kwamba ikiwa kuteseka na maumivu yake yangewekwa “katika mizani,” yangekuwa ‘mazito hata kuliko mchanga wa bahari.’—Ayubu 6:2, 3.

Sababu nyingine inayofanya tupate matatizo ni kwamba hatuwezi kuona matukio ya mbele. Kwa mfano, wazia ikiwa mwenye nyumba angejenga na kuuza nyumba katika eneo ambalo hushika moto kwa urahisi. Bila kujua jambo hilo ununue moja ya nyumba hizo na kuishi ndani. Je, wewe na familia yako hamtakuwa mkijihatarisha sana? Matatizo ambayo ungepata hayawezi kusemwa kuwa ni adhabu kutoka kwa Mungu. Ukweli umesemwa wazi katika Biblia: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Hata hivyo, inafariji kujua kwamba ingawa tunapatwa na matatizo, Mungu amekusudia kwamba hivi karibu sana wanadamu watakombolewa kutokana nayo. Wakati huo utakapofika, hutapatwa tena, wala kuona, au kusikia kuhusu matatizo. Machozi ya huzuni, maumivu, kifo, na maombolezo yatakuwa “yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Pia, ahadi ya kwamba watu hawatajenga nyumba na kupanda mimea tena ili tu ije kuharibiwa na vita au misiba inapendeza sana. Badala yake, watu “wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21-25.

Unaposubiri Mungu aondoe matatizo yote kabisa, unaweza kufanya nini sasa ili upunguze madhara yake? Kwanza kabisa, “usitegemee uelewaji wako mwenyewe,” Biblia inatuhimiza, lakini “mtegemee Yehova kwa moyo wako wote.” (Methali 3:5) Tafuta mwongozo na faraja kutoka kwake. Sikiliza hekima ya kimungu inayopatikana katika Biblia. Itakusaidia kufanya maamuzi ya hekima na kukulinda dhidi ya matatizo hayo yanayoweza kuepukika.—Methali 22:3.