Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alishinda Woga na Shaka

Alishinda Woga na Shaka

Igeni Imani Yao

Alishinda Woga na Shaka

PETRO aling’ang’ana kupiga kasia huku akitazama mbele. Je, mwanga huo hafifu alioona upande wa mashariki ulikuwa ishara kwamba alfajiri imefika? Misuli yake ya mgongo na ya mabega ilikuwa ikiuma kwa sababu ya kupiga kasia kwa saa nyingi. Upepo uliokuwa ukimpiga usoni ulikuwa umeichafua Bahari ya Galilaya. Mawimbi yalipiga mashua yao ya uvuvi na maji hayo yakammwagikia. Lakini bado aliendelea kupiga kasia.

Petro na wenzake walikuwa wamemwacha Yesu ufuoni. Siku hiyo walikuwa wamemwona Yesu akilisha umati wa maelfu ya watu waliokuwa na njaa kwa kutumia mikate na samaki wachache. Kwa sababu hiyo, watu walitaka kumfanya Yesu awe mfalme, lakini hakutaka kujihusisha katika siasa. Pia hakutaka wafuasi wake wajitakie makuu kwa njia hiyo. Akiepuka umati huo, aliwaagiza wanafunzi wake wapande mashua na kuelekea upande ule mwingine wa ziwa huku yeye akienda mlimani kusali akiwa peke yake.—Marko 6:35-45; Yohana 6:14, 15.

Wanafunzi walikuwa wameondoka usiku, lakini sasa mwezi ulikuwa ukikaribia kuzama upande wa magharibi. Hata hivyo, walikuwa wamesafiri kilomita chache. Kazi nyingi waliyokuwa wakifanya na kelele za upepo mkali uliokuwa ukivuma pamoja na mawimbi yalifanya iwe vigumu hata kuwa na mazungumzo. Huenda Petro alikuwa akiwaza na kuwazua.

Alikuwa na mambo mengi ya kuwazia! Amekuwa akimfuata Yesu wa Nazareti kwa zaidi ya miaka miwili. Amejifunza mambo mengi, lakini bado alikuwa na mengi ya kujifunza. Utayari wake wa kujifunza—kukabiliana na vipingamizi kama vile shaka na woga—kunamfanya awe mfano mzuri ambao tunaweza kuiga. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

“Tumempata Masihi”!

Petro hawezi kusahau siku ambayo alikutana na Yesu wa Nazareti. Ndugu yake, Andrea, alikuwa amemfikishia habari hizi zenye kustaajabisha: “Tumempata Masihi.” Maneno hayo yalianza kubadili maisha ya Petro.—Yohana 1:41.

Petro aliishi huko Kapernaumu, jiji lililokuwa kwenye fuo za ziwa la maji baridi linaloitwa Bahari ya Galilaya. Yeye na Andrea walishirikiana na Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, katika biashara ya uvuvi. Petro alikuwa akiishi na mke wake, mama mkwe, na ndugu yake Andrea. Kutegemeza familia kama hiyo kwa uvuvi kulihitaji jitihada, nguvu, na ubunifu. Tunaweza kuwazia wavuvi hao wakitupa nyavu zao usiku kucha na kuzikokota kati ya mashua zao mbili ili kuvua chochote kile ambacho kingepatikana. Tunaweza pia kuwazia kazi nyingi ya siku nzima ya kuchagua na kuuza samaki, kurekebisha nyavu zao na kuziosha.

Biblia inatueleza kwamba Andrea alikuwa mwanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Bila shaka, Petro alimsikiliza kaka yake akizungumza kuhusu ujumbe wa Yohana akiwa na hamu kubwa. Siku moja, Andrea alimwona Yohana akimwelekezea Yesu mkono na kusema: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu!” Na mara moja Andrea akawa mfuasi wa Yesu na kwa shauku akamwambia hivi Petro: Masihi amefika! (Yohana 1:35-40) Baada ya uasi kutokea huko Edeni miaka 4,000 hivi iliyopita, Yehova Mungu alikuwa ameahidi kwamba mtu wa pekee angekuja kutoa tumaini hakika kwa wanadamu. (Mwanzo 3:15) Andrea alikuwa amekutana na Mwokozi huyo, Masihi mwenyewe! Petro alitoka haraka kwenda kukutana na Yesu.

Kufikia wakati huo, Petro alikuwa akijulikana kwa jina Simoni, au Simeoni. Lakini Yesu alimtazama na kumwambia: “‘Wewe ni Simoni mwana wa Yohana; utaitwa Kefa’ (ambalo linatafsiriwa Petro).” (Yohana 1:42) “Kefa” ni neno la kawaida linalomaanisha “jiwe,” au “mwamba.” Kwa wazi, maneno ya Yesu yalikuwa ya kinabii. Aliona mapema kwamba Petro angekuwa kama mwamba, mtu imara mwenye kutegemeka kati ya wafuasi wa Kristo. Je, Petro aliona kwamba ana sifa hizo? Haielekei. Watu fulani pia leo wanaposoma masimulizi ya Injili hawamwoni Petro akiwa na sifa hizo zilizo kama mwamba. Wengine wamesema kwamba alionekana kuwa hana msimamo na mwenye kuyumbayumba.

Petro alikuwa na udhaifu wake na Yesu aliujua. Lakini sikuzote Yesu, kama Baba yake, Yehova, alijaribu kuona sifa nzuri za watu wengine. Yesu aliona kuwa Petro ana sifa fulani nzuri, kwa hiyo alimsaidia kuboresha sifa hizo. Yehova na Mwana wake hutafuta sifa nzuri ndani yetu leo. Huenda ikawa vigumu sana kwetu kuamini kwamba wanaweza kupata sifa nzuri ndani yetu. Hata hivyo, tunahitaji kuamini maoni yao na kukubali kufinyangwa kama Petro alivyofanya.—1 Yohana 3:19, 20.

“Acha Kuogopa”

Labda Petro aliandamana na Yesu katika safari yake ya kuhubiri iliyofuata. Huenda akawa alimshuhudia Yesu akifanya muujiza wake wa kwanza, kubadili maji yawe divai katika karamu ya ndoa huko Kana. Jambo muhimu hata zaidi, alimsikia Yesu akizungumzia ujumbe wa Ufalme wa Mungu wenye kupendeza na uliojaa tumaini. Lakini bado alimwacha na kurudia biashara yake ya uvuvi. Hata hivyo, miezi kadhaa baadaye, Petro alikutana tena na Yesu uso kwa uso, na wakati huu Yesu akamwomba Petro awe mfuasi wake maisha yake yote.

Usiku mzima Petro na wenzake walikuwa wamefanya kazi bila mafanikio. Walikuwa wameshusha nyavu zao tena na tena, lakini hakupata chochote walipozitoa majini. Bila shaka, Petro alitumia uzoefu na ustadi wake wote ili kupata samaki, akijaribu maeneo mbalimbali katika ziwa hilo ili apate mahali samaki hao walipokuwa wakila. Kwa hakika, kuna pindi ambapo, kama wavuvi wengi, Petro alitamani kwamba angetazama ndani ya maji hayo na kuona mahali samaki hao walipokuwa au awaingize katika nyavu zake. Bila shaka, mawazo kama hayo yalimfanya akate tamaa hata zaidi. Huo haukuwa mchezo kwa Petro; watu walikuwa wakimtegemea avue samaki. Mwishowe, alirudi ufuoni akiwa mikono mitupu. Lakini bado nyavu zilihitaji kusafishwa. Kwa hiyo, alikuwa akisafisha nyavu Yesu alipomwendea.

Umati ulikuwa umemsonga Yesu sana ukisikiliza kwa makini kila neno alilosema. Akiwa amezingirwa na watu hao, Yesu aliingia katika mashua ya Petro na kumwomba aivute mbali kidogo na nchi kavu. Sauti yake ikisikika waziwazi juu ya maji, Yesu akaufundisha umati. Kama wale waliokuwa ufuoni, Petro alisikiliza kwa makini sana. Hakuchoka kumsikiliza Yesu akizungumzia kichwa kikuu cha mahubiri yake—Ufalme wa Mungu. Lingekuwa pendeleo kubwa kama nini kumsaidia Kristo kueneza ujumbe huo wenye tumaini katika nchi yote! Lakini je, ilipatana na akili kwake kufikiria hivyo? Wangejiruzuku jinsi gani? Huenda Petro alifikiria tena kuhusu usiku uliotangulia ambao alijaribu kuvua bila mafanikio.—Luka 5:1-3.

Yesu alipomaliza kuzungumza, alimwambia Petro hivi: “Vuta mpaka mahali penye kilindi, nanyi mshushe nyavu zenu, mvue.” Petro alikuwa na shaka sana. Alisema: “Mwalimu, tulitaabika usiku wote na hatukupata chochote, lakini nitazishusha nyavu kwa amri yako.” Kwa kweli, Petro hakutaka kushusha nyavu hizo tena, hasa wakati huo ambapo huenda hata samaki hawakuwa wakila! Lakini alikubali, na huenda aliwaita wenzake waliokuwa katika mashua ya pili wamfuate.—Luka 5:4, 5.

Petro alihisi kwamba nyavu zilikuwa nzito alipojaribu kuzivuta. Akiwa na shaka, alivuta kwa nguvu, na baada ya muda mfupi aliona samaki wengi sana wakirukaruka ndani ya wavu! Kwa msisimko aliwaita wanaume waliokuwa katika mashua ya pili waje kumsaidia. Walipofanya hivyo, ilikuwa wazi kwamba samaki hao wote hawangetosha katika mashua moja. Walijaza mashua zote mbili, na bado samaki walikuwa wengi sana hivi kwamba zikaanza kuzama. Petro alijawa na mshangao. Kabla ya hapo alikuwa ameona nguvu za Kristo, lakini katika pindi hii Yesu alionyesha nguvu kwa niaba ya Petro na familia yake! Mwanamume huyo angeweza kufanya samaki waingie ndani ya nyavu! Petro alijawa na woga. Alipiga magoti na kusema: “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana.” Alijiona kuwa hastahili kushirikiana na Mtu aliyekuwa na mamlaka ya kutumia nguvu za Mungu katika njia kama hizo.—Luka 5:6-9.

Yesu alisema hivi kwa fadhili: “Acha kuogopa. Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:10, 11) Huo haukuwa wakati wa kuwa na shaka au woga. Shaka za Petro kuhusu mambo ya kila siku kama vile uvuvi hazikuwa na msingi; woga wake kuhusu kasoro na upungufu wake hakuwa na msingi vilevile. Yesu alikuwa na kazi kubwa sana ya kufanya, huduma ambayo ingebadili wakati ujao wa wanadamu. Alimtumikia Mungu ambaye “atasamehe kwa njia kubwa.” (Isaya 55:7) Yehova angewaandalia mahitaji yao ya kimwili na ya kiroho.—Mathayo 6:33.

Petro, Yakobo na Yohana walitenda upesi. “Wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu, wakamfuata.” (Luka 5:11) Petro alimwamini Yesu na Yule aliyekuwa amemtuma Yesu. Huo ndio uamuzi bora zaidi ambao angeweza kufanya. Leo, Wakristo wanaoshinda hisia za shaka na woga ili wamtumikie Mungu wanaonyesha kwamba wana imani kama hiyo. Kumtegemea Yehova kwa njia si bure.—Zaburi 22:4, 5.

“Kwa Nini Umekuwa na Shaka?”

Miaka miwili baada ya kukutana na Yesu, Petro alipiga kasia juu ya Bahari ya Galilaya usiku huo wenye upepo mkali uliotajwa mwanzoni mwa habari hii. Bila shaka, hatuwezi kujua ni mambo gani yaliyokuwa akilini mwake. Alikuwa amejionea mambo mengi sana. Yesu alikuwa amemponya mama mkwe wa Petro. Alikuwa ametoa Mahubiri ya Mlimani. Tena na tena, kupitia mafundisho na kazi zake za nguvu, alikuwa amethibitisha kwamba alikuwa Masihi, yule Mchaguliwa wa Yehova. Miezi ilipopita, kasoro za Petro, kama vile kushindwa na woga na shaka, zilipungua kwa kiasi fulani. Hata Yesu alikuwa amemchagua Petro kuwa mmoja wa wale mitume 12! Hata hivyo, punde si punde, Petro angegundua kwamba hakuwa amejiondolea kabisa hisia za woga na shaka.

Ghafula, katika kipindi cha kesha la nne la usiku, au wakati fulani kati ya saa 9:00 usiku na alfajiri, Petro aliacha kupiga kasia na akaketi wima. Kule mbele—juu ya mawimbi—aliona kitu fulani kikisonga! Je, ni mawimbi yaliyokuwa yakimulikwa na mwezi? Hapana, kitu hicho kilikuwa kirefu na kimenyooka. Kumbe alikuwa mtu! Ndiyo, kulikuwa na mtu anayetembea juu ya bahari! Kadiri alivyokaribia, ilionekana kana kwamba angewapita. Wakiwa na woga, wanafunzi walifikiri ulikuwa mzuka wa aina fulani. Mtu huyo alianza kuzungumza: “Jipeni moyo, ni mimi; msiogope.” Alikuwa ni Yesu!—Mathayo 14:25-28.

Petro alijibu hivi: “Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji.” Alikuwa na ujasiri mwingi. Akiwa na msisimuko kuhusu muujiza huo wa pekee, Petro alitaka imani yake iimarishwe. Alitaka kuhusishwa katika jambo lililokuwa likitendeka. Kwa fadhili, Yesu alimwambia aje. Petro alishuka kutoka kwenye mashua na kukanyaga juu ya maji. Hebu wazia jinsi Petro alivyohisi alipoweza kukanyaga na kusimama juu ya maji. Lazima awe alijawa na mshangao alipotembea kumwelekea Yesu. Hata hivyo, hisia nyingine ilianza kumkengeusha.—Mathayo 14:29.

Petro alihitaji kumkazia Yesu uangalifu. Akitumia nguvu za Yehova, Yesu ndiye aliyekuwa akimzuia Petro asizame. Na Yesu alikuwa akifanya hivyo kwa sababu ya imani ya Petro. Lakini Petro alikengeushwa fikira. Tunasoma hivi: “Akiitazama ile dhoruba ya upepo, akaogopa.” Petro alipoona mawimbi hayo yakiipiga mashua na kuruka, alijawa na wasiwasi. Huenda alijiwazia akizama katika ziwa hilo na kufa maji. Woga ulipojaa moyoni mwake, imani yake ilififia. Yule mtu ambaye alikuwa ameitwa Mwamba kwa sababu alikuwa imara akaanza kuzama kama jiwe kwa sababu ya imani yake kuyumbayumba. Ingawa Petro alikuwa mwogeleaji stadi, pindi hii hakutegemea uwezo huo. Alipaaza sauti: “Bwana, niokoe!” Yesu alimshika mkono na kumvuta. Kisha, wakiwa bado juu ya maji, Yesu alimfundisha somo hili muhimu: “Wewe mwenye imani kidogo, kwa nini umekuwa na shaka?”—Mathayo 14:30, 31.

“Umekuwa na shaka”—hayo yalikuwa maneno yanayoelezea vizuri hali ya Petro! Shaka inaweza kuwa na nguvu za kumwangamiza mtu. Tukijiruhusu tupatwe na shaka, inaweza kuharibu imani yetu na kutufanya tuzame kiroho. Tunahitaji kupigana nayo kwa bidii! Jinsi gani? Kwa kukazia fikira mambo yanayofaa. Tukikazia fikira mambo yanayotuogopesha, yanayotuvunja moyo, yanayotukengeusha fikira kutoka kwa Yehova na Mwana wake, shaka yetu itaongezeka. Tukikazia fikira Yehova na Mwana wake, mambo ambayo wamefanya, wanayofanya, na yale watakayofanya wakati ujao kwa ajili ya watu wanaowapenda, tutaepuka kuwa na shaka zinazoweza kuharibu imani yetu.

Petro alipoandamana na Yesu kurudi kwenye mashua, aliona dhoruba ikitulia. Bahari ya Galilaya ilitulia tuli. Petro na wanafunzi wenzake walisema hivi wakiwa na hakika, “Wewe kwa kweli ni Mwana wa Mungu.” (Mathayo 14:33) Jua lilipoanza kuchomoza juu ya ziwa hilo, moyo wa Petro ulijaa shukrani. Alijifunza kutoruhusu woga wake umfanye awe na shaka. Ni kweli kwamba bado alihitaji kufanya mabadiliko mengi ili awe Mkristo imara kama mwamba ambao Yesu alikuwa ametabiri. Lakini alikuwa amezimia kuendelea kujitahidi, kuendelea kukua. Je, wewe una mtazamo kama huo? Utaona kwamba imani ya Petro ni kielelezo kizuri cha kuiga.

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Yesu aliona mvuvi huyu anaweza kutokeza sifa nzuri

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana”

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

“Akiitazama ile dhoruba ya upepo, akaogopa”