Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Yesu Hakujihusisha Katika Siasa?

Kwa Nini Yesu Hakujihusisha Katika Siasa?

Kwa Nini Yesu Hakujihusisha Katika Siasa?

HEBU wazia ni jioni mwaka wa 32 W.K. Yesu, Masihi aliyetabiriwa, sasa anajulikana na watu wengi kwa sababu ya kuwaponya wagonjwa na hata kuwafufua wafu. Leo, amewashangaza maelfu ya watu kwa kufanya ishara nyingi zenye nguvu na kuwafundisha kuhusu Mungu. Sasa, anawaweka watu wenye njaa katika makundi madogo-madogo. Anatoa sala kwa Yehova na kuwalisha wote kimwujiza. Kisha anakusanya masalio ili kingine kisitupwe. Watu wanaitikia jinsi gani?—Yohana 6:1-13.

Umati unapoona jinsi Yesu alivyofanya miujiza, ustadi wake wa kuongoza watu wengi, na jinsi alivyowatimizia mahitaji yao, walikata kauli kwamba Yesu angekuwa mfalme mzuri. (Yohana 6:14) Hilo halitushangazi. Kumbuka walikuwa wanatafuta mtawala mzuri, anayefaa; nchi yao ilikuwa chini ya utawala wa kigeni uliokuwa unawakandamiza. Hivyo, walimshinikiza Yesu ajiunge na siasa. Ukiwa na mambo haya akilini, fikiria jinsi Yesu alivyotenda.

Andiko la Yohana 6:15 linasema hivi: “Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” Msimamo wa Yesu ulikuwa wazi. Alikataa moja kwa moja kujihusisha katika siasa za nchi yake. Hakubadili kamwe msimamo wake. Alisema wafuasi wake wanapaswa kuchukua msimamo huohuo. (Yohana 17:16) Kwa nini hakujihusisha na siasa?

Kwa Nini Yesu Aliamua Kutounga Mkono Upande Wowote?

Msimamo wa Yesu wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa ulitegemea kanuni za Maandiko. Acha tuchunguze kanuni mbili.

“Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Hivyo ndivyo Biblia inavyosema kuhusu historia ya utawala wa wanadamu. Kumbuka, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho kwa miaka mingi kabla ya kuja duniani akiwa mwanadamu. (Yohana 17:5) Hivyo, alijua kuwa mwanadamu hakuwa na uwezo wa kutimiza mahitaji ya mabilioni ya wanadamu kwa njia inayofaa; wala hakuumbwa na Mungu afanye kazi hiyo. (Yeremia 10:23) Yesu alijua kuwa suluhisho la matatizo ya wanadamu lilikuwa na chanzo kingine, na si serikali za wanadamu.

“Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Je, maneno hayo yanakushangaza? Wengi hushangazwa. Wao hufikiri kuhusu watu wenye nia nzuri wanaoingia serikalini kwa sababu wanataka kuifanya dunia iwe mahali salama. Lakini hata watawala wenye nia nzuri wajitahidi kadiri gani, hawawezi kushinda uvutano wa yule ambaye Yesu alimwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 14:30) Hiyo ndiyo sababu Yesu alimwambia mwanasiasa mmoja hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Yesu ndiye angekuwa Mfalme wa wakati ujao wa serikali ya Mungu ya kimbingu. Ikiwa Yesu angejihusisha katika siasa, angekuwa amevunja ushikamanifu wake kwa serikali ya Baba yake.

Kwa hiyo, je, Yesu alifundisha kuwa wafuasi wake hawapaswi kujitiisha kwa serikali za kidunia? La, badala yake, aliwafundisha jinsi wanavyopaswa kuwa na usawaziko wanapotimiza wajibu wao kumwelekea Mungu na kuelekea serikali za wanadamu.

Yesu Aliheshimu Mamlaka ya Serikali

Yesu alipokuwa akifundisha hekaluni, wapinzani wake walijaribu kumtega kwa kumwuliza ikiwa watu walipaswa kulipa kodi. Ikiwa Yesu angesema la, angeonekana kuwa mchochezi na labda angechangia roho ya uasi kati ya watu waliokuwa wamekandamizwa na waliotaka kuuondoa utawala wa Waroma wenye uonevu. Lakini kama angesema ndio, wengi wangehisi kuwa aliunga mkono ukosefu wa haki waliokuwa wanakabili. Jibu la Yesu lilikuwa na usawaziko wa hali ya juu. Alisema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Luka 20:21-25) Hivyo, wafuasi wake wanawajibika kwa Mungu na pia kwa Kaisari, yaani, serikali za kidunia.

Serikali huhakikisha kwamba kuna utaratibu wa kadiri. Wanawataka raia wawe wanyoofu, walipe kodi, na watii sheria za nchi. Yesu aliweka mfano gani wa “Kaisari vitu vya Kaisari”? Yesu alilelewa na wazazi ambao walitii sheria hata wakati ambapo haikuwa rahisi kwao kufanya hivyo. Kwa mfano, Yosefu akiwa na Maria mke wake aliyekuwa mja-mzito, walisafiri kilomita 150 hivi hadi Bethlehemu Waroma walipoamuru kwamba watu wahesabiwe. (Luka 2:1-5) Kama wazazi wake, Yesu pia alitii sheria, hata akalipa kodi ambazo hakudaiwa. (Mathayo 17:24-27) Pia alikuwa mwangalifu asivuke mipaka ya mamlaka yake kuelekea mambo ya kisheria. (Luka 12:13, 14) Kwa hiyo, tunaweza kusema kuwa Yesu aliheshimu mfumo wa serikali, ingawa alikataa kuwa sehemu ya serikali hiyo. Hata hivyo, Yesu alimaanisha nini aliposema tumlipe “Mungu vitu vya Mungu”?

Jinsi Yesu Alivyompa “Mungu Vitu vya Mungu”

Wakati fulani Yesu aliulizwa ni sheria gani kuu kati ya zile ambazo Mungu aliwapa wanadamu. Kristo alijibu: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” (Mathayo 22:37-39) Yesu alifundisha kwamba kuhusiana na kumlipa “Mungu vitu vya Mungu,” jambo la kwanza analotudai ni upendo, ambao unahusisha ushikamanifu kamili na wa moyo wote.

Je, upendo huo unaweza kugawanywa? Je, tunaweza kugawanya ushikamanifu wetu, nusu tumpe Yehova Mungu na serikali yake ya kimbingu kisha tupatie serikali fulani ya kidunia nusu ile nyingine? Yesu mwenyewe alitaja kanuni hii: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine.” (Mathayo 6:24) Yesu alikuwa akizungumza kuhusu kugawanya ushikamanifu kwa Mungu na kwa mali, lakini alihisi kuwa kanuni hiyo inaweza kutumika katika kujihusisha na siasa. Wafuasi wake wa karne ya kwanza walikuwa na maoni hayohayo.

Rekodi za kale zinaonyesha kuwa wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza hawakujihusisha katika siasa. Kwa sababu walimwabudu kikamili Yule ambaye Kristo alimwabudu, walikataa kuapa kwamba watakuwa washikamanifu kwa Roma na maliki wake, wala kujihusisha na utumishi wa jeshi, au kukubali vyeo katika serikali. Waliteswa sana kwa sababu ya ushikamanifu wao. Maadui wao waliwashtaki kwamba waliwachukia wanadamu wenzao. Je, mashtaka hayo yalikuwa ya kweli?

Wakristo wa Kweli Wanawajali Watu

Kumbuka Yesu alitaja kwamba sheria kuu ya pili kati ya sheria za Mungu ni, “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Ni wazi kuwa hakuna mfuasi wa kweli wa Kristo anayeweza kuwachukia wanadamu wenzake. Yesu aliwapenda watu, akajitoa kwa ajili yao, na akawasaidia walipokuwa na matatizo ya kawaida tu.—Marko 5:25-34; Yohana 2:1-10.

Hata hivyo, Yesu alikuwa maarufu kwa kazi gani? Hakujulikana kama Mponyaji, wala kama Mlishaji wa Maelfu, wala kama Mfufuaji wa Wafu, ingawa alifanya mambo hayo yote yenye kustaajabisha. Lakini kwa kufaa watu walimwita Mwalimu. (Yohana 1:38; 13:13) Yesu alieleza kuwa sababu yake kuu ya kuja duniani ilikuwa kufundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu.—Luka 4:43.

Hilo ndilo linalowafanya wafuasi wa kweli wa Kristo wajitoe kufanya kazi hiyohiyo ambayo Bwana wao alifanya alipokuwa duniani—kuwafundisha watu habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Yesu Kristo aliwaagiza Wakristo wote wa kweli wawafundishe watu ulimwenguni pote kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Serikali hiyo ya kimbingu yenye uadilifu itatawala uumbaji wote wa Mungu kulingana na sheria ya upendo. Itatimiza mapenzi ya Mungu, na hata itaondoa kuteseka na kifo. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4) Si ajabu kwamba Biblia husema kwamba ujumbe wa Yesu ni “habari njema”!—Luka 8:1.

Hivyo, ikiwa unawatafuta wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo leo, utawatambua jinsi gani? Je, wanajihusisha katika siasa za ulimwengu huu? Au kazi yao kuu ni kama ile ya Yesu—kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu?

Je, ungependa kujifunza mengi kuhusu Ufalme wa Mungu na jinsi unavyoweza kuboresha maisha yako leo? Tunakualika uwasiliane na Mashahidi wa Yehova katika eneo lako au utembelee Tovuti yao, www.watchtower.org.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Je, Mashahidi wa Yehova Husaidia Jamii?

Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika siasa. Hata hivyo, wao huwasaidia sana watu wa rangi, kabila, na malezi mbalimbali katika jamii wanamoishi. Fikiria mifano ifuatayo:

▪ Mashahidi wa Yehova ni kikundi cha wajitoleaji zaidi ya milioni saba ambao hutumia zaidi ya saa bilioni 1.5 kila mwaka kuwafundisha watu Biblia na jinsi inavyoweza kuwasaidia kuacha tabia na mazoea mabaya, kujenga familia zenye furaha, na kuboresha maisha yao.

▪ Wao huchapisha na kugawanya vichapo bila malipo katika zaidi ya lugha 500, kutia ndani lugha ambazo hazina vichapo vingine vyovyote vilivyochapishwa.

▪ Wana masomo ya kuwazoeza watu kusema hadharani. Masomo hayo yamewasaidia mamilioni ya watu kuzungumza kwa ufasaha na busara.

▪ Wana programu za kuwafundisha watu kusoma na kuandika. Programu hizo zimewasaidia makumi ya maelfu ya watu ulimwenguni pote kujua kusoma na kuandika.

▪ Wana Halmashauri za Ujenzi za Mkoa zaidi ya 400 ulimwenguni pote ambazo huwazoeza wajitoleaji mbinu za ujenzi ili waweze kujenga vituo vya kujifunzia Biblia. Katika miaka kumi iliyopita, zaidi ya majengo ya ibada au Majumba ya Ufalme 20,000 yamejengwa.

▪ Wao hushiriki kutoa msaada wakati wa msiba, wakiwasaidia Mashahidi na watu ambao si Mashahidi. Katika miaka miwili ya hivi karibuni ambapo vimbunga vilipiga Marekani, Mashahidi waliojitolea walijenga upya zaidi ya Majumba ya Ufalme 90 na nyumba 5,500.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Watu walipojaribu kumchochea ajihusishe na siasa, Yesu aliondoka na kwenda “mlimani akiwa peke yake”