Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

“Nilitamani Kuwa Kasisi”

“Nilitamani Kuwa Kasisi”
  • MWAKA WA KUZALIWA: 1957

  • NCHI: MEXICO

  • HISTORIA: MWANAFUNZI WA SEMINARI; MWENYE HASIRA KALI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa katika mji mdogo wa Texcoco. Wakati huo, barabara nyingi zilikuwa za vumbi. Lilikuwa jambo la kawaida kuwaona watu kutoka vijiji jirani wakitumia punda kuleta bidhaa mjini ili kuuza. Familia yetu ya watoto tisa ilikuwa maskini sana, nami nilikuwa mtoto wa saba. Ili kutunza familia, baba yangu alifanya kazi ya kurekebisha viatu. Lakini alikufa nilipokuwa na umri wa miaka saba. Kuanzia wakati huo mama yangu alijitahidi sana kuitunza familia.

Babu yangu alicheza ala ya fidla na alikuwa kiongozi wa kikundi cha kuimba nyimbo za dini. Karibu watu wote wa familia yetu walijua kucheza ala fulani ya muziki. Mama yangu aliimba katika kwaya ya kanisa, na mjomba wangu alikuwa mwimbaji aliyeigiza na pia mpiga piano. Tulikuwa Wakatoliki—Nami nilikuwa mvulana anayetumika kwenye madhabahu, na nilitamani kuwa mmishonari Mkatoliki. Wakati huo huo nilipenda sana kutazama sinema za karate. Kadiri nilivyozitazama ndivyo nilivyozidi kupenda jeuri.

Nilijiunga na shule ya kidini iliyokuwa kama seminari huko Puebla. Nilitaka kuwa kasisi Mkatoliki. Hata hivyo, katika mwaka wa mwisho wa masomo yangu nilichukizwa na Kanisa Katoliki. Mtawa fulani wa kike alinitongoza ili nifanye naye ngono. Nilikataa, lakini hilo lilinichochea nitamani kuoa. Zaidi ya hayo, niligundua kwamba makasisi kadhaa walikuwa wakiishi maisha ya unafiki. Hatimaye, niliacha mradi wangu wa kuwa kasisi.

Nikiwa mvulana anayetumika kwenye madhabahu, nilitamani kuwa mmishonari, lakini pia nilipenda sana kutazama sinema za karate na nikawa mjeuri

 Niliamua kusomea muziki katika chuo cha National Conservatory of Music, huko Mexico City. Baada ya kuhitimu, nilifunga ndoa, na punde si punde tukapata watoto wanne. Nilipata riziki kwa kuimba wakati wa Misa katika Kanisa Katoliki.

Tangu mwanzo ndoa yetu ilikuwa na matatizo. Mimi na mke wangu tuligombana mara nyingi kwa sababu tulioneana wivu. Mwanzoni tuligombana lakini baadaye tukaanza kupigana. Kisha, baada ya miaka 13, tukaamua kutengana na hatimaye tukatalikiana.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza kabla sijatengana na mke wangu. Mashahidi wawili walibisha mlango wetu na wakaanzisha mazungumzo ya Biblia. Nilifikiri nilijua mengi kuhusu dini, hivyo nikataka kuwakosoa. Niliwauliza maswali magumu ambayo nilifikiri hayana majibu. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba kila mara walinipa majibu sahihi yanayotegemea Biblia. Niligundua kwamba sikujua mengi. Hata hivyo, mke wangu aliwachukia Mashahidi, na mimi nilikuwa na shughuli nyingi hivi kwamba wakaacha kuja.

Miaka mitano baadaye, nilikuwa nikiishi na mwanamke mwingine, anayeitwa Elvira, nilipokutana tena na Mashahidi wa Yehova. Elvira hakupinga Mashahidi, hivyo, ilikuwa rahisi kujifunza Biblia kwa ukawaida. Hata hivyo, ilinichukua miaka kadhaa kufanya mabadiliko.

Nilitambua kwamba ili kumwabudu Yehova kwa moyo wote, nilihitaji kufanya mabadiliko fulani makubwa. Kwanza nilihitaji kuacha kazi ya kuimba katika Misa za Kanisa Katoliki, na hilo lilimaanisha kwamba nilihitaji kutafuta kazi tofauti. (Ufunuo 18:4) Pia, nilihitaji kuandikisha ndoa yangu na Elvira.

Hata hivyo, jambo gumu zaidi lilikuwa, kujifunza kudhibiti hasira yangu kali. Maandiko mawili ya Biblia yalinisaidia sana: Zaburi 11:5, linaloonyesha kwamba Yehova anachukia jeuri, na 1 Petro 3:7, ambalo lilinifundisha ili Yehova asikilize sala zangu, nilipaswa kumtendea mke wangu kwa heshima. Nilipoendelea kutafakari maandiko hayo na kumwomba Yehova anisaidie, hatua kwa hatua nilianza kudhibiti hasira yangu.

Biblia ilinifundisha kwamba ili Yehova asikilize sala zangu, nilipaswa kumtendea mke wangu kwa heshima

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sasa ninafurahia maisha ya familia. Ninajitahidi kuwa na uhusiano mzuri na watoto niliopata katika ndoa yangu ya kwanza na vilevile kusaidia familia yangu ya sasa kuwa na imani thabiti.

Nilipokuwa mtoto, nilitamani kuwa kasisi na kusaidia watu. Sasa ninahisi maisha yangu yana kusudi la kweli. Ninapata riziki kwa kufundisha watu muziki. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunivumilia, na kwa kunipa nafasi ya kubadili maisha yangu, na kuwa mtu mzuri!