Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIRI YA FURAHA YA FAMILIA

Zungumza na Kijana Wako—Bila Kubishana

Zungumza na Kijana Wako—Bila Kubishana

“Binti yangu alipofikisha umri wa miaka 14, alianza kuzungumza nami bila heshima. Nilipomwambia ‘Njoo tule,’ alinijibu ‘Nitakula wakati ninaotaka.’ Nilipomuuliza kama amemaliza kazi zake, alinijibu ‘Acha kunisumbua!’ Mara nyingi tulifokeana kwa sauti ya juu.”—MAKI, JAPANI. *

Ikiwa wewe ni mzazi wa kijana anayebalehe, huenda ikawa vigumu kwako kukabiliana na mabishano. “Binti yangu anaponipinga, mimi hupandwa na hasira. Tunakasirika sana na kufokeana,” anasema Maria, ambaye ana binti mwenye umri wa miaka 14, nchini Brazili. Naye Carmela, anayeishi nchini Italia anakabili hali sawa na hiyo. Anasema, “Mimi na kijana wangu hubishana kila wakati na mwishowe yeye huondoka kwa hasira na kujifungia chumbani.”

Kwa nini baadhi ya vijana wanapenda kubishana? Je, ni kwa sababu ya rafiki zao? Huenda ikawa hivyo. Biblia inasema kwamba rafiki za mtu wanaweza kumfanya awe na tabia nzuri au mbaya. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Kwa kuongezea, burudani nyingi za vijana huchochea uasi.

Hata hivyo, kuna sababu nyingine ambazo si vigumu kushughulika nazo ikiwa utajua namna zinavyoweza kumwathiri kijana wako. Ona mifano kadhaa.

ANASITAWISHA “NGUVU ZA KUFIKIRI”

Mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho  13:11) Kama alivyosema mtume Paulo, watoto hufikiri tofauti na watu wazima. Jinsi gani?

Kwa kawaida, watoto hawachanganui mambo. Hata hivyo, watu wazima huchanganua mambo kwa uzito na kufikiri kwa kina wanapofanya maamuzi. Kwa mfano, watu wazima hufanya maamuzi kwa kutegemea kanuni na kufikiria jinsi matendo yao yatakavyowaathiri wengine. Huenda wamezoea kufikiri kwa njia hiyo. Lakini vijana hawajazoea kufikiria hivyo.

Biblia inawatia moyo vijana wasitawishe “uwezo wa kufikiri.” (Methali 1:4) Kwa kweli, Biblia inawatia moyo Wakristo wote watumie “nguvu [zao] za kufikiri.” (Waroma 12:1, 2; Waebrania 5:14) Hata hivyo, nyakati nyingine uwezo wa kijana wa kufikiri unaweza kufanya abishane na wewe, hata katika mambo madogo. Au wakati mwingine anaweza kutoa maoni ambayo si sahihi. (Methali 14:12) Katika hali kama hizo, unawezaje kuzungumza naye bila kubishana?

JARIBU KUFANYA HIVI: Huenda kijana wako anajaribu tu mbinu zake mpya za kufikiri, na labda hatashikilia maoni yake. Ili ujue maoni yake, kwanza mpongeze kwa uwezo wake wa kufikiri. (“Naelewa unavyofikiri, hata ingawa sikubaliani na yote uliyosema.”) Kisha, msaidie achunguze kufikiri kwake. (“Je, unafikiri maoni yako yanaweza kutumiwa kusuluhisha kila jambo?”) Huenda ukastaajabu kuona jinsi kijana wako atakavyorekebisha maoni yake.

Tahadhari: Unapozungumza na kijana wako, si lazima ujionyeshe uko sawa wakati wote. Hata kama inaonekana hakubaliani na unachosema, huenda akajifunza mambo mengi kutokana na majadiliano yenu. Usishangae ikiwa baada ya siku chache kijana wako atakubaliana na maoni yako au hata kudai kwamba hayo ni maoni yake.

“Nyakati nyingine mimi na mwanangu tulibishania mambo madogokama vile, kutupa chakula au kumchokoza dada yake. Lakini katika visa vingi huenda ingefaa kama ningejaribu kumwelewa kwa kusema, ‘Aah kumbe ndivyo ilivyo’ au ‘Kumbe ndivyo unavyofikiri.’ Ninapokumbuka wakati huo, naona kwamba kama ningesema maneno kama hayo huenda tungeepuka mabishano mengi.”—Kenji, Japani.

ANASITAWISHA MAONI YAKE

Wazazi wenye busara huwaruhusu vijana watoe maoni yao

Kwa sehemu kubwa kumlea mtoto anayebalehe kunahusisha kumtayarisha kuwa mtu mzima. (Mwanzo 2:24) Mojawapo ya mambo muhimu ni kumsaidia kujitambua—kusitawisha tabia, imani, na viwango vinavyofaa. Anapokabili mkazo wa kufanya mambo yasiyofaa kijana mwenye viwango hatafikiria tu matokeo ya matendo yake. Badala yake atajiuliza hivi: ‘Mimi ni mtu wa aina gani? Ninafuata viwango gani? Mtu mwenye viwango hivi angefanyaje katika hali hii?’2 Petro 3:11.

Biblia inatueleza kuhusu Yosefu, kijana mwenye viwango. Kwa mfano, mke wa Potifa alipomshawishi afanye naye ngono, Yosefu alijibu hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwanzo 39:9) Ingawa kufikia wakati huo Waisraeli hawakuwa wamepewa sheria inayokataza uzinzi, Yosefu alielewa maoni ya Mungu kuhusu ngono. Isitoshe, neno “ninawezaje” linaonyesha wazi kwamba alipenda maoni ya Mungu na yalikuwa sehemu ya utu au utambulisho wake.Waefeso 5:1.

Kijana wako pia anajaribu kujiwekea viwango. Jambo hilo ni zuri kwa sababu litamsaidia kukabiliana na vishawishi kutoka kwa vijana wenzake. (Methali 1:10-15) Kwa upande mwingine viwango hivyo vinaweza kumfanya apinge maamuzi yako. Utafanya nini?

JARIBU KUFANYA HIVI: Badala ya kubishana naye, rudia maneno aliyosema. (“Sijui kama nimekuelewa. Unasema kwamba . . . ”) Kisha muulize maswali. (“Ni nini kinachofanya ufikiri hivyo?” au “Kwa nini uliamua hivyo?”) Mpe muda wa kujieleza. Mwache aeleze maoni yake. Ikiwa mnatofautiana kwa sababu ya mapendezi wala si kwamba maoni yake yana makosa, onyesha kwamba unaheshimu maoni yake—hata kama hukubaliani na mapendezi yake.

 Kijana wako anapoendelea kujiwekea viwango na kusitawisha utu wake, hilo litamsaidia. Zaidi ya yote, Biblia inasema Wakristo hawapaswi kuwa kama watoto wanaorushwa “huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.” (Waefeso 4:14) Kwa hiyo, mruhusu kijana wako ajiwekee viwango na awe na msimamo imara.

“Ninapowaambia binti zangu kwamba niko tayari kuwasikiliza, wanakuwa na mwelekeo wa kukubali maoni yangu hata kama ni tofauti na maoni yao. Ninaepuka kuwalazimisha kufikiri kama ninavyofikiri, badala yake nataka wawe na msimamo wao.”—Ivana, Jamhuri ya Czech.

UWE IMARA LAKINI MWENYE USAWAZIKO

Vijana fulani huendelea kusisitiza maoni yao tena na tena ili kuwachosha wazazi wao. Ikiwa hali iko hivyo katika familia yako, uwe mwangalifu. Ingawa kukubali maoni yake katika hali hiyo kunaweza kusuluhisha mambo, kutamfanya kijana aamini kwamba kubishana ni njia bora ya kupata anachotaka. Dawa ni nini? Fuata ushauri huu wa Yesu: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” (Mathayo 5:37) Watoto wako wakijua kwamba una msimamo thabiti hawatabishana nawe mara kwa mara.

Hata hivyo, usisahau kuwa na usawaziko. Acha kijana wako ajieleze, kwa mfano, kwa nini anataka ubadili muda uliomwekea wa kurudi nyumbani. Katika hali hiyo, hutakuwa ukilegeza msimamo wako badala yake utatii ushauri huu wa Biblia: “Usawaziko wenu na ujulikane.”Wafilipi 4:5.

JARIBU KUFANYA HIVI: Panga kuwe na mkutano wa familia ili mzungumzie sheria za nyumbani. Onyesha kwamba uko tayari kusikiliza maoni yao kabla ya kufanya maamuzi. “Vijana wanapaswa kuona kwamba wazazi wako tayari kusikiliza na kufuata mapendekezo ya watoto wao ikiwa hayavunji kanuni za Biblia,” anasema Roberto, baba anayeishi Brazili.

Bila shaka, hakuna mzazi mkamilifu. Biblia inasema hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Ikiwa unahisi umesababisha kuwe na mabishano kati yako na kijana wako usisite kuomba msamaha. Ukikubali makosa yako unamwekea kijana mfano mzuri wa unyenyekevu na hilo litamsaidia aige mfano wako.

“Baada ya kubishana na kijana wangu, nilimwomba msamaha kwa sababu nilimfokea kwa hasira. Jambo hilo lilimtuliza na kufanya iwe rahisi kwake kunisikiliza.”—Kenji, Japani.

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

  • Ni kwa njia gani mimi huchangia mabishano kati yangu na kijana wangu?

  • Nitatumiaje habari hii ili nimfahamu kijana wangu vizuri zaidi?

  • Nitafanya nini ili nizungumze na kijana wangu bila kubishana?