Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuokoa Hazina ya Kale Kutoka Kwenye Takataka

Kuokoa Hazina ya Kale Kutoka Kwenye Takataka

NINI huja akilini mwako unapofikiria rundo la takataka? Huenda ukakumbuka harufu mbaya na takataka. Hivyo, ni wazi kwamba hauwezi kutarajia kupata kitu chochote chenye thamani, hasa hazina yenye thamani kubwa.

Hata hivyo, karne iliyopita, kitu chenye thamani kubwa kilipatikana katika takataka. Ilikuwa hazina yenye thamani kubwa. Hazina hiyo ilikuwa nini? Kwa nini uvumbuzi huo una maana kwetu leo?

UVUMBUZI USIOTARAJIWA

Mwanzoni mwa karne ya 20, wasomi katika Chuo Kikuu cha Oxford, Bernard P. Grenfell na Arthur S. Hunt, walitembelea Misri. Wakiwa huko, walivumbua vipande kadhaa vya hati za mafunjo vilivyokuwa ndani ya rundo la takataka karibu na Bonde la Mto Nile. Baadaye, katika mwaka wa 1920 wasomi hao walipokuwa wakiorodhesha hati hizo, Grenfell alinunua vipande vingine vya hati vilivyochimbuliwa huko Misri. Alivinunua kwa niaba ya Maktaba ya John Rylands huko Manchester, Uingereza. Hata hivyo, wanaume hao wawili walikufa kabla hawajamaliza kuorodhesha vipande hivyo.

Msomi mwingine wa Chuo Kikuu cha Oxford, Colin H. Roberts, alimalizia orodha hiyo. Alipokuwa akipitia hati hizo, aliona hati moja ndogo ya mafunjo yenye urefu wa sentimeta 9 na upana wa sentimita 6. Alishangaa kuona kwamba hati hiyo ilikuwa na mwandiko wa Kigiriki na alielewa maandishi hayo. Upande mmoja ilikuwa na maneno yanayopatikana kwenye Yohana 18:31-33. Upande ule mwingine ilikuwa na sehemu ya mstari wa 37 na 38. Roberts alitambua kwamba alikuwa amepata kitu chenye thamani kubwa sana.

KUKADIRIA UMRI WAKE

Roberts alihisi kwamba hati hiyo ndogo ya mafunjo ilikuwa ya zamani sana. Hata hivyo, ilikuwa na umri gani? Ili ajue, aliamua kutumia mbinu ya paliografia, ambayo ni uchunguzi wa maandishi ya zamani. Alilinganisha mwandiko kwenye hati hiyo na mwandiko kwenye hati nyingine zenye tarehe. * Kwa kutumia mbinu hiyo, aliweza kukadiria umri wa hati hiyo. Hata hivyo, alitaka kuwa na uhakika. Hivyo, alipiga picha hati hiyo, na kutuma nakala za picha hiyo kwa wataalamu watatu wa mafunjo na kuwaomba wamweleze umri wa hati hiyo. Wataalamu hao walijibuje?

Walipochunguza kwa makini mtindo wa mwandiko wa hati hiyo, wataalamu hao watatu walikubaliana kwa umoja kwamba hati hiyo ilikuwa imeandikwa mwanzoni mwa karne ya pili W.K.—miaka michache baada ya mtume Yohana kufa! Hata hivyo, haimaanishi kwamba huwezi kukosea unapochunguza umri wa hati kwa kutumia mbinu hiyo, kwani hata msomi mmoja anasema kwamba huenda hati hiyo iliandikwa wakati wowote katika karne ya pili. Hata hivyo, kipande hicho kidogo cha hati bado ndicho cha kale zaidi kati ya hati za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambazo zimewahi kupatikana.

KIPANDE CHA HATI YA RYLANDS KINAFUNUA NINI?

Kwa nini kipande hicho cha hati ya Injili ya Yohana ni chenye umuhimu sana kwa wale wanaoipenda Biblia leo? Angalau kuna sababu mbili. Kwanza kabisa, muundo wa hati hiyo unatusaidia kuelewa jinsi Wakristo wa mapema walivyothamini Maandiko.

Kwa nini kipande hiki cha hati ya Injili ya Yohana ni cha maana sana kwa wale wanaoipenda Biblia leo?

Katika karne ya pili W.K., habari iliandikwa katika miundo miwili—kwenye kitabu cha kukunjwa na kwenye kodeksi. Vitabu vya kukunjwa vilitengenezwa kutokana na vipande vya mafunjo au vya ngozi vilivyounganishwa pamoja na kuwa kipande kimoja kikubwa. Kipande hicho kikubwa kingekunjuliwa na kisha kukunjwa baada ya kutumiwa. Kwa kawaida kitabu cha kukunjwa kiliandikwa kwenye upande mmoja tu.

Hata hivyo, kipande kidogo cha hati ambacho Roberts alivumbua kina mwandiko pande zote mbili. Hilo linaonyesha kwamba kilikuwa sehemu ya kodeksi na sio kitabu cha kukunjwa. Kodeksi ilitengenezwa kutoka kwa vipande vya ngozi au mafunjo vilivyounganishwa na kukunjwa pamoja na muundo wake ulikuwa kama wa kitabu.

Kulikuwa na faida gani kwa kutumia kodeksi badala ya kitabu cha kukunjwa? Kumbuka kwamba Wakristo wa mapema walikuwa waeneza-injili. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Walitangaza ujumbe wa Biblia popote walipopata watu, iwe ni nyumbani, sokoni na barabarani. (Matendo 5:42; 17:17; 20:20) Kwa hiyo, ilikuwa rahisi kwao kutumia Maandiko yaliyounganishwa pamoja.

Kodeksi pia ilisaidia watu kunakili Maandiko kwa ajili ya kutumia kutanikoni na pia kwa matumizi ya kibinafsi. Hivyo, vitabu vya Injili vilinakiliwa kwa kurudia na ni wazi kwamba hilo lilisaidia kwa kiasi kikubwa kukua haraka kwa Ukristo.

Kipande cha Hati ya Rylands upande wa mbele na nyuma

Sababu ya pili inayoonyesha umuhimu wa hati ya Rylands kwetu leo, ni kwamba inafunua jinsi maandishi ya mwanzo ya Biblia yalivyonakiliwa kwa usahihi. Ingawa hati hiyo inaonyesha mistari michache tu kutoka kwa Injili ya Yohana, habari iliyomo inakaribiana sana na habari tunayosoma leo katika Biblia zetu. Kipande hicho cha hati ya Rylands kinaonyesha kwamba habari iliyo katika Biblia haijabadilishwa ingawa imenakiliwa tena na tena.

Kwa kweli kipande hicho kidogo cha hati ya Rylands cha Injili ya Yohana, ni sehemu moja tu ya uthibitisho mwingi uliopo katika maelfu ya vipande vya hati unaothibitisha kwamba maandishi ya awali ya Biblia yalinakiliwa kwa usahihi. Katika kitabu chake The Bible as History, Werner Keller, anasema hivi: “Hati hizi za zamani ndizo zinazotoa uthibitisho kabisa kwamba habari tunayosoma katika Biblia zetu ni sahihi na yenye kutegemeka.”

Ni kweli kwamba imani ya Wakristo haitegemei uvumbuzi wa vitu vya kale. Wao wanaamini kwamba “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3: 16) Hata hivyo, inatia moyo kama nini kuona vitu vya kale vyenye thamani vikithibitisha kile ambacho Biblia ilisema tangu zamani kwamba: “Neno la Yehova linadumu milele”!—1 Petro 1: 25.

^ fu. 8 Kulingana na kitabu Manuscripts of the Greek Bible, paliografia “ni mbinu ya kuchunguza maandishi ya kale.” Baada ya muda fulani, mtindo wa mwandiko hubadilika. Mabadiliko hayo yanaweza kusaidia kukadiria umri wa hati za zamani zinapolinganishwa na hati nyingine zenye tarehe.