Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, UNGEPENDA KUJIFUNZA BIBLIA?

Mpango wa Kujifunza Biblia kwa Ajili ya Watu Wote

Mpango wa Kujifunza Biblia kwa Ajili ya Watu Wote

Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri hadharani. Hata hivyo, je, unajua kwamba sisi hujifunza na watu Biblia duniani pote?

Katika mwaka wa 2014, zaidi ya Mashahidi 8,000,000 katika nchi 240, waliongoza mafunzo ya Biblia, 9,500,000 hivi kila mwezi. * Kwa kweli, idadi ya watu wanaojifunza Biblia pamoja nasi, inazidi idadi ya watu katika nchi 140 hivi!

Ili kufanya kazi hii ya kuelimisha watu, kila mwaka Mashahidi wa Yehova huchapisha Biblia, vitabu, magazeti na machapisho mengine ya Biblia, bilioni moja na nusu hivi katika lugha 700! Jitihada hizo kubwa za kuchapisha zinasaidia watu wajifunze Biblia katika lugha wanayopendelea.

MAJIBU YA MASWALI YANAYOULIZWA MARA NYINGI KUHUSU MPANGO WETU WA KUJIFUNZA BIBLIA

Utaratibu wa kujifunza umepangwa jinsi gani?

Sisi huchukua habari mbalimbali zinazopatikana katika Biblia na kuchunguza mistari ya Biblia inayohusiana na habari hizo. Kwa mfano, Biblia inatoa majibu ya maswali kama vile: Mungu ni nani? Ana utu wa aina gani? Je, ana jina? Anaishi wapi? Je, tunaweza kumkaribia? Watu wengi hupata changamoto ya kujua ni wapi katika Biblia wanaweza kupata majibu.

Ili kuwasaidia watu wapate majibu ya maswali ya Biblia, sisi hutumia kitabu chenye kurasa 224, kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? * Kitabu hicho kimetayarishwa ili kuwasaidia watu kuelewa mafundisho ya msingi ya Biblia. Mafundisho hayo yanatia ndani masomo kuhusu Mungu, Yesu Kristo, kwa nini wanadamu wanateseka, ufufuo, sala, na mengine mengi.

Funzo linaweza kufanywa wakati na mahali gani?

Funzo linaweza kufanywa wakati na mahali panapokufaa.

Vipindi vya kujifunza huchukua muda gani?

Watu wengi hutenga saa moja au zaidi kila juma ili kujifunza Biblia. Hata hivyo, urefu wa kujifunza wa kila kipindi unaweza kubadilika. Tutajifunza kulingana na ratiba yako. Wengine wamejifunza kwa dakika 10 au 15 tu kila juma.

Funzo hilo linagharimu pesa ngapi?

Funzo na machapisho ya kujifunzia hutolewa bila malipo. Hilo linapatana na agizo hili la Yesu alilowapa wanafunzi wake: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8.

Funzo linachukua kipindi gani mpaka kumaliza?

Unaweza kujifunza kwa kipindi cha wakati unachopenda. Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kina masomo 19. Unaweza kumaliza masomo hayo yote kulingana na nafasi yako.

Je, ni lazima niwe Shahidi wa Yehova baada ya kumaliza kujifunza?

Hapana. Tunatambua na tunaheshimu uhuru alionao kila mtu wa kuamua atakachoamini. Hata hivyo, watu waliopata ujuzi wa msingi wa Biblia wanaweza kufanya uamuzi kulingana na ujuzi huo.

Nitapata wapi habari zaidi?

Tovuti ya jw.org/sw inatoa habari sahihi kuhusu imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova.

Ninawezaje kuomba funzo la Biblia?

  • Tuma ombi kupitia www.ps8318.com/sw.

  • Tuma ombi lako ukitumia mojawapo ya anwani zinazopatikana katika ukurasa wa pili wa gazeti hili.

  • Wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio karibu nawe. Unaweza pia kutafuta Mashahidi wa Yehova katika kitabu cha orodha ya simu.

^ fu. 4 Kwa kawaida, mafunzo ya Biblia huongozwa pamoja na watu mmoja-mmoja au vikundi vya watu.

^ fu. 9 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Nakala zaidi ya milioni 230 za kitabu hicho zimechapishwa katika lugha zaidi ya 260.